Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii na mimi niweze kutoa mchango wangu katika mpango huu. Kwanza nitangulize tu kutoa shukrani zangu kwa Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Magufuli, amefanya mambo makubwa na kila mtu anaona. Kwa mfano, kwangu kule Manyoni hatukuwa na miradi ya maji, lakini sasa tuna miradi ya maji, fedha imeanza kutoka tunashukuru sana angalau mradi hata mkubwa wa wastani mmoja unaendelea. Sina budi kutoa shukrani zangu kwa niaba ya wananchi wa Manyoni Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nizungumzie jambo fupi tu. Tulikabidhiwa Ilani ya Chama cha Mapinduzi, Wabunge wa Chama cha Mapinduzi, lakini pia hata wenzetu wanatumia Ilani hiyo. Katika Ilani hiyo nimeigawa katika makundi makubwa mawili ya kusimamia. Eneo la kwanza ni la huduma za jamii, tunapozungumzia maji, afya, elimu, miundombinu, hizo ni huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti,eo nizungumzie suala la kuboresha uchumi kwa wananchi wetu, wamepata maji sawa, natoa mfano, lakini uchumi wao ukoje? Vile vikundi vyetu vya ujasiriamali vikoje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na maoni ya Kamati katika ukurasa ule wa tano, kipengele cha pili kinasema, “Kuzingatia maeneo yanayogusa wananchi walio wengi kwa ajili ya kukuza kipato na kupunguza umaskini, hususan kilimo, uvuvi, upatikanaji wa pembejeo na mitaji.” Mimi nijikite kwenye eneo la kilimo. Manyoni kwa mfano, Mbunge pamoja na Madiwani wenzangu tunalala na kusugua vichwa ni namna gani tupate kuwawezesha wananchi wetu kupata ajira, tufanye nini, lakini tumekuja na tunayo mambo matatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza; hivi ninavyozungumza Manyoni Mashariki eneo linaloitwa Masigati tumetenga ekari 3,200 kwa ajili ya kuanza ukulima wa korosho baada ya wataalam kutoka Naliendele kupima ule udongo na kutuambia mkilima korosho hapa mtapata korosho nyingi na bora kuliko zile za Lindi na Mtwara. Tumeshatenga ekari 3,000 hivi ninavyozungumza tunachangishana fedha kwa ajili ya kupata grader la kufyeka ule msitu, ili tuanze kupanda korosho na miche imeshaanza kuoteshwa kwenye vitalu, ekari 3,000. Tumeshachanga fedha shilingi milioni 36 mpaka sasa hivi kwa ajili ya mafuta, ila hatujui grader tulipate wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa bajeti hii inayokuja tukitenga fedha kidogo angalau kuwaunga mkono wananchi, Serikali tunaomba ipitishe ile bajeti ya watu wa Manyoni kwenye eneo hili la kilimo, ili tuweze kuajiri watu wengi zaidi pale Manyoni. Kama kiongozi, lazima tulale na kuota namna gani tutaweza kuongeza ajira kwa watu wetu. Manyoni tumeanza na tunaendelea, tunaomba Serikali ituunge mkono kwa hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika msimu huu sasa tungefurahi kusikia Serikali inasema angalau kuna kafedha ka dharura au kuna grader ambalo lipo mahali fulani kwenye Wizara labda ya Ujenzi, fedha tumeshakusanya ya mafuta, wakatusaidie kufyeka ule msitu tupande korosho, tutaajiri watu wengi sana kwenye eneo hilo, zaidi ya watu 3,000 watapata ajira Manyoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine hapo Manyoni kuna Kijiji kinaitwa Solya, ni katika kupambana tu kutafutia watu ajira, kuna eneo tumelitenga ni la mfano tunataka tuanze shamba darasa, tuna heka 10 pale. Tumeshachimba mabwawa ya urefu wa mita 10 kwa 20 yapo nane ya samaki. Pia tuna heka mbili tumeshaanza ni shamba darasa kwa ajili ya bustani, tunataka vijana wote ambao hawana ajira kwenye eneo lile waanze kupata ajira. Shamba darasa lile litasaidia sana kwa vijana wa Manyoni na maeneo mengine yote watakuwa wanajifunza pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalo tatizo, maji yale ni ya kuchimba chini, tumechimba kisima kwenye shamba darasa pale na umeme tumevuta kwa nguvu zetu wenyewe. Hata hivyo, lakini kuna eneo ambalo tumelitenga ni kubwa pia la hekari 20, tunahitaji visima vitatu na wameshapima visima maji yapo lakini hatuna uwezo wa kuchimba vile visima. Kikubwa miundombinu ya umeme kwa sababu lile eneo ni nje kidogo ya kijiji. Tungeomba Serikali ituunge mkono, itusaidie zile nguzo zitoke pale, ni kama kilometa moja na nusu hivi zitoke kwenye sehemu ya umeme watupelekee umeme kwenye eneo hilo la shamba. Tunaomba sana Serikali itusaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo ni mbinu ambazo Kiongozi yeyote ambaye anaweza kuona mbele, lazima afikirie kuongeza ajira na kutafuta ajira kwa watu wake na hasa vijana, akinamama na watu wote. Manyoni viongozi tunakosa usingizi kwa ajili ya kuongeza ajira, kumsaidia Mheshimiwa Rais anahangaika sana, Serikali mtuunge mkono, Manyoni tumeanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalo eneo pia la machimbo ya chumvi, eneo linaitwa Kijiji cha Kinangali, tunayo chumvi nyingi sana, tunaomba sana msaada kwenye mambo ya kitaalam namna ya kuchakata ile chumvi, tunatumia mbinu za kizamani, tunakata miti sasa tunaharibu mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana Serikali mtusaidie utalaam, tumejaribu sana lakini tunaomba sana Serikali hasa sehemu ya Wizara inayohusika na mambo ya ajira na vijana, hebu watusaidie wataalam ile chumvi inavyochakatwa hasa kwa njia za kitaalam, tunayo chumvi nyingi sana. Tutasaidia ajira vijana wengi sana na akinamama kwenye lile eneo. Manyoni sisi tumeanza, tunaomba Serikali ituunge mkono kwenye maeneo haya ambayo nimeyataja hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikihama kwenye eneo hilo la kuongeza ajira kwa watu wetu, labda la mwisho tu. Jamani ndugu zangu haiwezekani katika nchi hii kila mahali ikawa ni sehemu ya kuishi, msitu mnene unakuta umefunga, mtu anatoka atokako anakaa katikati ya msitu. Kule Manyoni wanatuvamia watu wahamiaji, anakaa katikati ya msitu, miti minene ile imekua kwa miaka mingi, karne na karne mizuri katikati ya msitu anaanza kufyeka anajenga, anafyeka shamba na sehemu ya kulishia mifugo. Haiwezekani kila mahali pakawa pa kujenga tu, lazima tutunze mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia ule mpango wa matumizi ya ardhi ambao tumeusema tangu mwaka juzi, mpango huu unachelewa mno. Naomba Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi mtusaidie kuharakisha huu mpango jamani, wakulima na wafugaji wapate maeneo yao, sehemu ya kujenga na viwanda pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tuipime Tanzania, tuhifadhi mazingira jamani, ni sawa na mtu ambaye amepanda juu ya mti, amekalia tawi anafyeka kwenye shina kule, likidondoka lile tawi anatangulia yeye chini. Hawezi mtu kukaa katikati ya msitu anaanza kufyeka eti natafuta shamba ama anatafuta sehemu ya kujenga, haiwezekani. Anaacha vijiji vingi tu anaruka anakuja kujenga katikati ya msitu, haiwezekani! Tuipime Tanzania katika mpango huu wa matumizi bora ya ardhi, tuiokoe nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulisema hata mwaka jana nilisema hivi kwa mfano, hata hii migogoro ya mkulima na mfugaji tulisema tupime, sijui mpango umeishia wapi? Kwamba tupime, kuna maeneo mengi tu tunawanyanyasa wafugaji bure, kuna maeneo mengi ambayo tukijipanga vizuri tukayapima kila mmoja atakaa sehemu na mifugo yake kwa raha mustarehe wala haina shida, eneo tunalo kubwa tunakosa mpango tu. Ni mpango tu ndugu zangu tunaokosa ndio maana tunagombana, haiwezekani mfugaji au mkulima anakuja anachukua heka 1,000, wengine wanapata wapi? Ni lazima kila mmoja apate eneo ambalo atakaa nalo kwa kudumu pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo hifadhi za misitu au za wanyama ambazo zimekuwa redundant ambazo zimekosa sifa, zile tungezipima tukazigawa hata kwa wakulima na wafugaji. Tunazo ranchi zetu ambazo zimekuwa redundant tuzipime tuweke miundombinu, malambo, mabwawa na wataalam wa mifugo ili watu wafuge kule. Jenga hata viwanda vya kuchakata/kusindika nyama kule; tunayo maeneo makubwa tunakosa mpango tu, utaratibu mzuri wa kupima, tuipime Tanzania jamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo mafupi, mimi sina cha zaidi, naunga mkono mpango huu, tuyazingatie haya mawili niliyoyazungumza, tulale na kufikiria kuwatafutia watu wetu ajira. Serikali ituunge mkono lakini tukaipime Tanzania kila mmoja apate mahali pa kufanyia kazi bila kugombana, kuharibu mazingira wala vyanzo vya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.