Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la kuridhia Mkataba (Intergovernmental Agreement – IGA) baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamuhuri ya Uganda kuhusu Mradi wa Ujenzi wa Bomba la Kusafirisha Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (East Africa Crude Oil Pipeline – EACOP) kutoka Hoima (Uganda) hadi Tanga (Tanzania)

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la kuridhia Mkataba (Intergovernmental Agreement – IGA) baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamuhuri ya Uganda kuhusu Mradi wa Ujenzi wa Bomba la Kusafirisha Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (East Africa Crude Oil Pipeline – EACOP) kutoka Hoima (Uganda) hadi Tanga (Tanzania)

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO (K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA): Mheshimiwa naibu Spika, nianze kwa kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuonesha kupitia michango yao mbalimbali hapa, kwa kweli mshikamano na Serikali katika suala hili kimsingi simuoni hata mmoja ambaye anaona kwamba huu mradi hauna tija kwetu. Wote wanaunga mkono, na ni maeneo machache tu ambayo Waheshimiwa Wabunge wanataka kufanyike fine tuning (marekebisho ya uboreshaji) na kuipa Serikali tahadhari hapa na pale, hayo tunayapokea. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge waliochangia hoja hii ni saba, sita kwa kuongea na mmoja kwa maandishi; na hoja kubwa ambayo nimeiona katika michango yote hapa, pengine nianze na Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini; ni kuwa mkataba huu ukiuangalia kwa umakini unakinzana na Sheria yetu ya mamlaka ya nchi kuhusiana na umiliki wa rasilimali na maliasili na unaiona hoja hiyo hiyo ikitolewa na Kambi Rasmi ya Upinzani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba niiongelee kwa kifupi hoja hiyo. Naomba nianze kusisitiza kwamba Sheria yetu hii ya Maliasili na Rasilimali tuliyoipitisha, ya sovereignty inahusu maliasili zetu. Katika mkataba huu na mradi huu, tunachokiongelea hapa ni mafuta ya Uganda. Sisi ni wasafirishaji, sisi tuna lori lakini mikungu ya ndizi iliyoko ndani tunayoitoa Kyela kuileta Dar es Salaam si yetu ndiyo maana naona maudhui ya sasa hayaoani na yale ya Sheria ya permanent sovereignty.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukumbuke kwa mfano juzi hapa tumepitisha Sheria hapa ya Azimio la Bonde la Mto Songwe lililetwa tena hilo suala. Sasa hizi ni shared resources, sasa wakati tunakuta nchi mbili zenye sovereignty zimekaa pamoja, lakini sisi sheria yetu ndiyo ikachukua pre-dorminants na ikawa na over-riding effect kupita sheria zao wenyewe pia wenzetu upande wa pili hilo katika sheria za kimataifa sijawahi kuliona. Mnakaa chini mnajadiliana na mkataba huu ni zao la makubaliano kati ya nchi mbili zenye sovereignty. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tunafaidika na kodi, kwa ajira pamoja biashara kadhaa zitakazojitokeza. Mimi pengine niungane na Profesa Tibaijuka hapa amesisitiza pia. Hebu tuone tofauti kati ya mkataba, tuna mikataba ya madini na Serikali, ni tofauti na mikataba kati ya Serikali na Serikali ambazo ni international treaties ipo tofauti kubwa naomba tusiichanganye. Mimi nakushukuru sana Profesa Tibaijuka kwahuo mchango wako.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tumepokea hoja nzuri tu kutoka kwa Kambi Rasmi ya Upinzani lakini kuhusu kifungu cha pili kiko katika ukurasa wa tatu wa hotuba ya Kambi ya Upinzani; kwamba kifungu hiki kinazuia taarifa na kwamba inafanana kabisa na mikataba inayoingiwa kisirisiri na mpaka hata Bunge hili linanyimwa hizo taarifa. Nilitaka tu kusema kuwa kifungu hiki hakizuii utoaji wa taarifa, bali kinaweka utaratibu bora tu wa kutoa taarifa hiyo kwa kuitaarifu nchi iliyotoa taarifa nayo iweze kutoa taarifa yake, ni heshima tu. Ni sawa na kusema leo hii sisi Wabunge tuna haki ya kuwa na mikataba, lakini huendi tu wewe mwenyewe moja kwa moja kwenda kuchukua, unapitia kwa Spika. Sasa huo utaratibu wa kupitia kwa Spika ikaonekana ni kizuizi hilo itakuwa ni tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka kusema tu kwamba, haya tu ni makubaliano kati ya nchi na nchi, ni utaratibu tu kama ule ambao tumejiwekea hapa hata wa mikataba, hebu pata ridhaa basi ya nchi mwenzako. Mwenzano amekupa taarifa sasa wewe unaisambaza tu maan taarifa inahitajika na Bunge. Mimi nina uhakika kwa ushirikiano tulionao, Uganda si nchi ya kigeni, si nchi iliyo nje ya bara hili, ni majirani zetu, wote tuko chini ya East African Community mimi nina uhakika mambo yatakuwa mazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile si kweli kuwa tumetoa uhuru mkubwa mno kwa Uganda kiasi cha kwamba tumewapa hata umilikiwa wa Chongoleani ya Tanga, habana. Tulichofanya sisi ni kuipa Uganda haki ambazo zinasimamiwa na sheria za kimataifa. Uganda ni land locked state na land locked state zote duniani zina haki zao sawa hasa ukisoma Sheria yetu hii UN Convention on the Law of the Sea, wana haki ya kupewa treatment ya kupitisha mizigo yao, kuwapa haki sawa, wasijisikie kwamba wanapoteza kwa kufanya hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo wameongea wote wanaoguswa na bomba, nimefurahi sana. Mheshimiwa Mussa Mbarouk anasema tuwe waangalifu na fidia ya ardhi kwa wananchi wetu. Mimi nafikiri hili ni wazo zuri, tumelipokea na tunaomba sasa Serikali haina mikono mingi, sisi wawakilishi wa wananchi bomba litapita kwenye maeneo yetu, sisi tuwe mstari wa mbele kutetea haki za wananchi wetu hasa upande wa ardhi. Serikali itaweza kuchukua hatua tukisikia wawakilishi wa wananchi mko mstari wa mbele na kusema hapana, hapa kunaonekana kuna hitilafu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna hoja ya kuwapa priority aliyotoa Mheshimiwa Mbarouk, kwamba tutoe priority ya ajira kwa wale wanaopitiwa na mradi, hiyo ni sahihi kabisa, hili ni suala la utekelezaji. Hata hivyo naomba nisisitize kwamba mradi huu tumesema unatekelezwa na private sector ambayo inahitaji efficiency, inahitaji kukimbilia fursa. Huwezi tu umekaa chini ya mwembe sasa wewe kwa sababu unapita kwako basi ubembelezwe ili ukafanye kazi pale. Tuchangamkie fursa na Waheshimiwa Wabunge tuwe mstari wa mbele kuchangamkia fursa kwa niaba ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Profesa Tibaijuka kwa kweli nakushukuru sana kwa michango yako. Mimi nafikiri…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waziri subiri kidogo. Waheshimiwa Wabunge kwa mujibu wa Kanuni ya 28(2) nataka kuongeza muda wa nusu saa ili tumalizie hoja hii ya Mheshimiwa Waziri hapa. Kwa hivyo nitawahoji maana fasili hii inaitaka niwahoji.

(Hoja Ilitolewa Iamuliwe) (Hoja Iliamuliwa na Kuafikiwa)

NAIBU SPIKA: Sawa, ili kumbukumbu zikae sawa sawa, Wabunge wamehojiwa kuongeza nusu saa na wamekubali. Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO (K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa ongezeko hili la muda ingawa sijawatendea haki wale wa mwanzo nilikuwa nakimbia kwa sababu najua muda ulikuwa umekwisha. Hata hivyo, naomba tu nimshukuru sana Mheshimiwa Profesa Tibaijuka, ameongelea suala la ulinzi. Kwa kweli suala la ulinzi ni kitu muhimu sana kwetu wote Watanzania. Bomba hili ambalo linalopita nchini kwetu lina faida, lina tija kwa Taifa na kama alivyosema, ni wajibu wetu mkubwa Watanzania wote kuhakikisha usalama wa hili bomba.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Nkamia naye vilevile kama ilivyo kwa Mbarouk, kama ilivyo kwa Profesa Tibaijuka, wote wamepitiwa na hili bomba na Mheshimiwa Nkamia amesisitiza kuhusu ulipwaji wa fidia stahili na kwa muda muafaka. Mimi nafikiri hili ni suala la muhimu, tunalipokea kama Serikali, ni masuala haya ya utekelezaji ambayo lazima angalizo tulichukue. Lakini vilevile kuna kitu kimoja ambacho ningependa nikiongelee kidogo, ameongelea kuhusu suala la kiwango cha pesa tutakachopata kila siku, amesema ni kikubwa sana. Najua tunafaidika, lakini tusije tuka-exaggerate kiasi cha kupata tukafika mahali ambapo sasa kesho asubuhi tukadaiwa kila mtu anunuliwe bajaj.

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwango cha pesa tutakachopata, tukisoma vizuri maelezo niliyoyatoa ni kwamba kila pipa lita-generate dola 12.2; sawa, kwa siku kutakuwa na mapipa 216,000 lakini pesa hiyo si kwamba yote inakuja Tanzania, kisome vizuri kile kifungu, tukisoma vizuri kile kifungu ni pesa inatosha kwa sababu hapa tunaongelea economies of scale, hatimaye tunapata pesa ya kutosha; lakini si kwa kiasi ambacho kilioneshwa na Mheshimiwa Nkamia kwamba hiyo yote sasa inakuja kwetu hapana! Itakwenda in proportion na hisa zetu. Naomba tuisome vizuri hiyo provision, itakwenda in proportion na hisa. Pamoja na angalizo hilo bado pesa ni nzuri, tunafaidika at the end of the day.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Vedastus Manyinyi ambaye kwa kweli ni kama amerudia tu hoja za wenzako zote. Hata hivyo nisisitize kitu kimoja; kwamba mradi huu haujadondoka kwetu kama zawadi au kama embe dodo tu umekaa chini ya mti likadondoka, tumeupigania kama Taifa. Ndiyo maana tumemshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa aliyofanya ya kidiplomasia kuweza kushawishi nchi jirani kwamba njia bora kupitisha bomba hilo ni Tanzania na faida ni kubwa sana, na ndiyo maana hata ukiisoma hotuba ya upinzani hilo imekubali kabisa kwamba kwa kweli huu mradi una tija kubwa kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe wito tu kwa Watanzania kwamba lazima maeneo ambayo mradi unapita na vilevile Mkoa wa Tanga wenyewe ambapo ndiyo hatma ya hilo bomba kuishia naomba jamani tuzichangamkie fursa tele ambazo zinajitokeza. Nilipokuwa Tanga kwenye mkutano wa biashara tulikuwa na Mheshimiwa Mbarouk, nilitoa taarifa kwamba tayari kuna watu (agents) wapo Tanga na Dar es Salaam wakishawishi makampuni yatakayokuwa based Tanga pale kwamba aah! Sehemu nzuri kukaa ni jirani tu hapa, kuna mahoteli mazuri mnakuja kwa gari asubuhi au kwa helikopta. Sasa hiyo Watanzania tumeshajifunza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna sehemu tulikuwa tunachoronga kule Songosongo, watu walikuwa wanakuja na ndege asubuhi kulala. Ni fursa sasa kujenga mahoteli ya kutosha, fursa sasa kujenga miundombinu ya maisha ya kila siku kwa sababu watakaokuwepo Tanga wana watoto watahitaji kwenda shule, wana familia zitahitaji hospitali, wana familia zitahitaji hospitali, maduka ya dawa mazuri na huduma mbalimbali. Ndiyo maana nasema, la msingi kabisa hapa si Serikali tena, ni sisi Watanzania kuchangamkia fursa zilizopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.