Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa jitihada kubwa walizofanya kuleta mabadiliko makubwa ya kiutendaji katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rasilimali ardhi ina umuhimu wa kipekee kwa uhai wa maendeleo ya binadamu, wanyama, mimea na viumbe vyote. Kwa uchumi wa Taifa letu ambalo wananchi walio wengi wanategemea sana kilimo kama sekta muhimu katika kukidhi mahitaji yao ya kila siku; rasilimali ardhi inakuwa na umuhimu wa kipekee, kiasi kwamba ni haki ya kila mwananchi kupata, kuimiliki, kuitumia na kuitunza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wimbi la kuwepo kwa migogoro ya mipaka na uvamizi wa ardhi katika maeneo ya vijiji limeendelea kuwa tatizo kubwa katika nchi yetu. Tatizo hili ni kikwazo kwa maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla. Tumeendelea kushuhudia migogoro hii ikisababisha upotevu wa mali za wananchi, vifo na kuendeleza uhasama kati ya jamii na jamii na hivyo kuwafanya wananchi kubaki maskini na kuishi maisha duni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kasi ndogo ya upimaji ardhi imeendelea kuwa donda ndugu, wataalam wa ardhi kutowashirikisha wananchi wakati wa uwekaji wa mipaka; na kutowaelimisha wananchi juu ya mipaka iliyowekwa, kama Taifa hatuwezi kuiacha hali hii iendelee. Wizara ichukue hatua za makusudi kuhakikisha kuwa wataalam wa ardhi wanawashirikisha na kuwaelimisha wananchi wakati wa uwekaji wa mipaka. Wizara iongeze kasi ya upimaji wakati wa uwekaji wa mipaka. Wizara iongeze kasi ya upimaji ardhi ili kuzuia wajanja wachache kuvamia maeneo pasipo viongozi wa vijiji kujua na hatua kali zichukuliwe kwa viongozi wa vijiji wanaogawa ardhi kinyume na taratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya wakulima na wafugaji imeendelea kuwa chanzo cha machafuko na umwagaji damu nchini. Lazima kasi yetu ya kutenga maeneo maalum ya wafugaji na wakulima iandamane na utunzaji wa sheria kali utakaozuia uvamizi wa maeneo unaofanywa na pande hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, bado mashamba makubwa yasiyoendelezwa yameendelea kuwa chanzo kikubwa cha migogoro ya ardhi nchini. Bado mfumo wetu wa kufuta miliki ya ardhi isiyotumika ipasavyo kwa mujibu wa makusudio ya umiliki wa ardhi husika umeendelea kutoa mwanya wa watu wachache kuhodhi ardhi bila kuitumia na kuwaacha wananchi wengi wakitaabika kwa kukosa ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kufanya mapitio ya Sheria ya Umiliki Ardhi na kanuni zake ili tupunguze urasimu katika mfumo wetu ili mashamba yaliyotelekezwa yaweze kufutiwa hati za umiliki mara tu yanapothibitika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara nyingine nilete kilio cha muda mrefu cha wananchi wa Wilaya ya Mkinga, ambayo ni miongoni mwa wilaya zinazokabiliwa na migogoro ya umiliki wa ardhi na mashamba yaliyotelekezwa kwa muda mrefu. Licha ya jitihada kadhaa ambazo kwa nyakati tofauti Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mkinga na mimi binafsi tumewasilisha Wizara ya Ardhi mapendekezo ya Wilaya kuhusu utatuzi wa migogoro hiyo; bado utatuzi wa migogoro hii umekwama kupata majawabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mapendekezo ya Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mkinga yaliwasilishwa Wizara ya Ardhi tangu mapema mwaka 2007 wakati huo Mkinga ikiwa bado ni sehemu ya Wilaya ya Muheza; ofisi yangu iliwasilisha tena maombi hayo kupitia mchango wangu wa maandishi wakati wa Bunge la Bajeti mwaka jana na kufuatiwa na barua kwa Waziri wa Ardhi yenye Kumb. Na. MB/MKN/Ardh 01/2016 ya tarehe 30 Mei, 2016. Napenda kuikumbusha Wizara juu ya maombi haya ambayo kimsingi yamechukua muda mrefu kupatiwa ufumbuzi.

(i) Shamba la Kilulu; shamba hili ndipo palipojengwa Makao Makuu ya Wilaya ya Mkinga. Shamba hili kwa mara ya kwanza lilimilikishwa kwa Bwana Van Brandis na Bibi Mary Van Brandis hadi tarehe 31 Oktoba,1959 ambapo umiliki ulihamia kwenda ama Bwana Akberali Walli Jiwa. Mmiliki huyu hakuendeleza shamba hili lenye ukubwa wa ekari 5,699.9 hadi umiliki wake ukafutwa mwaka 1972. Baada ya kufuta umiliki, Serikali ililipa fidia na shamba likawa chini ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadaye Wilaya ya Muheza ilipokea maombi ya kumilikishwa shamba hilo toka Kampuni ya M/S Arusha Farms Limited (CHAVDA). Taratibu zote zilizofanyika na alimilikishwa ekari 2,699.9 na ekari 3,000 walipewa wananchi wa vijiji jirani vya Vuo, Mwachala na Parungu Kasera waliokuwa na shida ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, M/S Arusha Farms Limited walipewa barua ya toleo (Letter of Right of Occupancy) ya tarehe 10 Mei, 1991 ambayo ilisajiliwa na Msajili wa hati tarehe 10 Mei, 1991 ambayo ilisajiliwa na Msajili wa hati tarehe 13 Mei, 1990 kwa Land Office Number 125127.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mmiliki huyu aliomba mkopo kutoka CRDB Bank kwa kuweka rehani barua ya toleo. Aidha, alishindwa kurejesha mkopo huo na CRDB waliuza shamba kwa M/S Mbegu Technologies Limited tarehe 27 Juni, 2004 ambao walilipa mkopo huo. Hata hivyo, pia hakuweza kuliendeleza shamba hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bwana Akberali Jiwa licha ya kunyang’anywa shamba hilo na kulipwa fidia aliwasilisha ombi lake la kurejeshewa umiliki wa shamba hilo. Ombi lake liliwasilishwa katika Kikao cha Kamati ya Kugawa Ardhi tarehe 10 Oktoba, 1996 na iliazimiwa liwasilishwe katika Kamati ya Ushauri wa Ardhi Mkoa. Kamati hiyo chini ya Uenyeviti wa Mkuu wa Mkoa iliridhia Bwana Akberali Jiwa apewe shamba hilo kwa vile M/S Arusha Farms Limited ameshindwa kuliendeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Muheza ilitoa barua ya toleo kwa miliki ya miaka 99 kuanzia tarehe 1 Oktoba, 1998 kwa Akberali Jiwa kwa jina la Kampuni ya Kilulu (2000) Limited. Baada ya tatizo hilo la double allocation kujitokeza, Halmashauri ya Muheza iliandika barua Kumb. Na. MUDF/3844/63 ya tarehe 2 Aprili, 2007 kwenda kwa Kamishna wa Ardhi kwa ajili ya kuomba kufuta miliki hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, licha ya ufuatiliaji uliofanywa wa mara kwa mara, kwa mujibu wa taarifa ya Halmashauri hadi leo Halmashauri haijapata hati yoyote inayoonesha kufutwa milki ya shamba tajwa. Kikao cha RCC kilichofanyika mwaka jana kiliridhia hati ya shamba tajwa ifutwe; hivyo kuagiza taratibu za kutoa notice zifanyike. Hata hivyo, tangu wakati huo kumekuwa na urasimu mkubwa wa utoaji notice tajwa. Naiomba Wizara ifuatilie jambo hili.

(ii) Shamba la Moa; shamba hili lina ukubwa wa ekari 15,739.60 na linamilikiwa na Mkomazi Plantations Limited wa S.L.P. 2520 Dar es Salaam kwa hati Na. 4268,9780 &9781. Halmashauri ya Wilaya ilituma notisi ya kuwafutia hati miliki yao kwa kutoendeleza na kutolipia kodi. Baada ya hapo Halmashauri ya Wilaya iliwasilisha barua ya Mapendekezo kwa Kamishna wa Ardhi yenye Kumb. Na MKG/LD/F/2/54 ya tarehe 28 Julai, 2009.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taratibu za ufutaji hati miliki ziliendelea Wizarani, lakini Halmashauri ilipokea barua ya mmiliki akieleza kuwa jina la umiliki lilibadilika na kuwa Moa Plantation & Aquaculture wa S.L.P. 364 Dar es Salaam na kwamba wanataka kuendeleza shamba hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ilishawasilisha Wizarani barua ya mapendekezo ya kufuta hati miliki, ililazimika kumwandikia Kamishna wa Ardhi barua yenye Kumb. Na. MKG/LD/F/2/56 ya tarehe 9 Juni, 2011 kumweleza kupokea barua hiyo na kwamba shamba hilo lina vijiji vinne ambavyo vimeanzishwa na kusajiliwa (Moa, Ndumbani, Mayomboni na Mhandakini).

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, vijiji hivyo tayari vina huduma za jamii kama shule, zahanati, barabara na kadhalika katika maeneo hayo; hivyo aendelee na taratibu za ufutaji hati miliki au kama atasitisha ufutaji basi wamiliki wakubali kumega maeneo yanayokaliwa na vijiji na kuendelezwa na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati hali ikiwa hivyo, mwaka 2013 mmiliki wa shamba atengeneze PP na kuomba kubadilisha matumizi ya sehemu ya shamba ili kupima viwanja 450 vya makazi. Hata hivyo, viwanja hivyo havikuwahi kupimwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatilia ucheleweshaji usioeleweka wa kufuta hati ya shamba hili, mnamo mwezi Oktoba, 2016 mmiliki wa shamba alitumia mwanya huo kutengeneza PP nyingine ya eneo lote la shamba ili kupima viwanja. Aidha, amekabidhi hati ya shamba tajwa ili ipelekwe kwa Afisa Ardhi Mteule-Moshi ili taratibu zinazokusudiwa ziweze kufanywa. Naiomba Wizara iingilie kati mchakato huu ili ardhi tajwa irejeshwe mikononi mwa Halmashauri ya Wilaya.

(iii) Mwele Seed Farm; shamba hili lina ikubwa wa hekta 954. Mmliki ni Wizara ya Kilimo. Wakati ambapo shamba hili lilikusudiwa kuwa shamba la kuzalisha mbegu, hali halisi ni kwamba kwa kipindi cha takribani miaka 15 sasa shamba hili limeshindwa kutumika kama ilivyokusudiwa na sehemu kubwa kubaki kuwa pori.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa vijiji vinavyozunguka shamba hili Mbambakofi, Maramba A, Maramba B na Lugongo ndio wamekuwa nguvukazi ya kulifanyia usafi shamba hili pale wanaporuhusiwa kufungua mashamba mapya na kulima mazao ya muda mfupi kila msimu mpya wa kilimo unapowadia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo tarehe 21 Septemba, 2007, Halmashauri ya Wilaya iliandika barua kwa Kamishna wa Ardhi Kumb. Na. MUD/ASF/VOL.VI/35 ikipendekeza kumegwa kwa shamba hili na kugawiwa kwa wananchi wa vijiji jirani kutokana na uendelezaji wake kuwa mdogo sana na kodi kutolipwa. Hata hivyo, maombi haya hayakuwahi kupatiwa majibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba hili lilipakana na Kijiji cha Mbambakofi chenye takriban kaya 500 zenye jumla ya wananchi wapatao 3173. Mbambakofi ni kijiji pekee katika Wilaya ya Mkinga ambacho kimekosa hata eneo la kujenga huduma muhimu za kijamii kama shule ya msingi na zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, shamba hili limepakana na Mji Mdogo wa Maramba ambao unakua kwa kasi kubwa, ukiwa na takriban watu 30,000 na kuzungukwa na mashamba makubwa ya Maramba JKT, hekta 2,445; Lugongo Estate, hekta 6,040; Kauzeni Estate, hekta 189.66; na Mtapwa Estate, hekta 476.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya kutekelezwa kwa shamba hili imezidi kuwa mbaya sana sasa kuliko ilivyokuwa mwaka 2007, wakati Halmashauri ya Wilaya ilipoomba kwa mara ya kwanza kumegwa kwa shamba hili. Kwa sasa hali imekuwa mbaya kiasi kwamba hata majengo mengi yaliyokuwepo yameanguka na machache yaliyosalia yamekuwa magofu, mashine na mitambo yote ya kilimo iliyokuwepo shambani hapo imeharibika na michache iliyosalia imehamishiwa Morogoro. Kwa sasa shamba limebaki na wafanyakazi wasiozidi watatu kutoka ishirini na vibarua thelathini waliokuwepo miaka ya 1988 – 1995.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Halmashauri ya Wilaya kusubiri kwa muda mrefu jibu la Kamishna wa Ardhi bila mafanikio, kikao cha RCC kiliiagiza Halmashauri kuandaa maelezo kuhusiana na shamba hili ili Mkuu wa Mkoa aweze kuandikia Wizara husika kuomba rasmi Halmashauri kukabidhiwa eneo tajwa. Tayari Halmashauri imetekeleza maagizo haya. Naiomba Wizara ya Ardhi isaidie katika utatuzi wa kero hii ambayo inawasumbua sana wananchi.

(iv) Kwamtili Estate; shamba hili lina ukubwa wa hekta 1,150 na linamilikiwa na Kwamtili Estate Limited yenye Certificate of Incorporation Na. 2649 iliyosajiliwa tarehe 9 Januari, 1961 ikiwa na wanahisa wafuatao:-

S/N JINA LA MWENYE HISA ANAPOISHI MAELEZO
1 DENNIS Martin Fielder 4 Market Square Tenbery,Wells Worcestershinre –UK Amerudi Uingereza
2 National Aggriculture
& Food Corporation (NAFCO Box 903 Dar es Salaam Shirika limefutwa
3 Handrick Tjails Scheen CI/30 Algamines Bank, Amsterdam, Netherland Amefariki
4 Louis Van Wagenburg Laycsan Ag Vaghel, Holland Amefariki
5 Schoonmarkers Bart Vandrbug De Congqabsen,163 Schikher, Holland Amefariki
6 Tracey Elan Allison The Willos Terrigton, Herefordenshire, UK Amefariki
7 Juvent Magoggo 42 Block S. Mikanjuni Box 5855 Tanga Anaishi Tanga
8 W.J. Tame Ltd Box 118 Tanga Amefariki
9 Jacobus Cornelius Josephus Moris Logtamburg Vaghel Holland Amefariki

Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba hili lililopo katika eneo la Kwamtili, Kata ya Bosha Wilaya ya Mkinga, lilitumika kwa kilimo cha kibiashara cha zao la kakau. Hata hivyo, kwa muda wa miaka takriban 26 sasa shughuli za kilimo cha zao la kakau zimesimama baada ya iliyokuwa Menejimenti ya Kampuni chini ya Ndugu Dennis Fielder kutelekeza shamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, baada ya shamba kutelekezwa, mmoja wa wanahisa Ndugu Juvent Magoggo amekuwa akifanya shughuli ndogo ndogo ikiwemo kuvuna miti ndani ya shamba hili kwa lengo la kupata fedha za kufanyia uzalishaji mdogo mdogo; na hali kadhalika kuruhusu wananchi wanaozunguka shamba hilo kulima mazao ambayo si ya kudumu. Hata hivyo, kwa sasa ndugu Magoggo ameshindwa kuendelea kufanya shughuli hizo baada ya kunyimwa vibali vya kuvuna miti kusafirisha magogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na kuwepo kwa ombi la umiliki wa shamba hili, yamezuka makundi ya watu yanayodai kuwa na haki ya kumiliki shamba hili na hivyo kuwakodisha wananchi wanaozunguka shamba hili maeneo ya kulima kwa kuwalipisha sehemu ya mavuno yatokanayo na matumizi ya ardhi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kumekuwa na wimbi la kujitokeza raia wa kigeni kwa kutumia kivuli cha aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa shamba na kulitekeleza Ndugu.Dennis Fielder kufanya uharibifu wa mali za kampuni, ikiwemo upasuaji wa mbao na kuanzishwa michakato ya kujimilikisha ardhi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili, wananchi wanainyooshea kidole Ofisi ya Wakala wa Hifadhi ya Misitu, Wilaya ya Mkinga kutaka kujiingiza katika kufanya udalali wa ardhi hii. Wananchi bado wanakumbukumbu nzuri ya jinsi watumishi hawa wa TFC Wilayani Mkinga walivyotumika kuwezesha mwekezaji wa Kiitaliano aliyejaribu kupatiwa ardhi ya Mkinga takriban hekta 25,000 kinyume na taratibu ili kulima Jatropher.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Serikali haijaweza kulipatia ufumbuzi tatizo lingine ambalo kimsingi limeanzishwa na TFC kutaka kupora ardhi ya wananchi katika shamba la Segoma, TFC hiyo hiyo inataka kuzalisha mgogoro mwingine wa kupora ardhi nyingine katika Wilaya ya Mkinga.

Hatupo tayari kuona hili likitokea hasa ikizingatiwa kuwa Kwamtili inakabiliwa na tatizo kubwa la ardhi. Tunaiomba Serikali kutumia busara kuacha jambo hili na kuirejesha ardhi hii kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kwamtili na Kata ya Bosha kwa ujumla wamebaki katika umaskini wa kutupa baada ya shughuli za kilimo cha kakau katika shamba la Kwamtili ambacho ndicho kilitoa ajira kwao kusitishwa. Nusura pekee kwa wananchi hawa ni kupatiwa maeneo katika shamba hili ili kwa kutumia utaratibu wa wakulima wadogo waweze kufanya shughuli ya kilimo na hivyo kujikimu kimaisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali ifanye uamuzi wa kufuta hati ya shamba la Kwamtili na kisha kuligawa kwa wananchi kwa ajili ya kilimo na sehemu nyingine kwa wananchi kuwa hifadhi ya msitu wa kijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua changamoto kubwa inayowakabili wananchi wa Kwamtili, RCC iliagiza mmiliki wa shamba hili kupewa notice ili taratibu za kufutiwa hati ziweze kufanyika. Kwa masikitiko makubwa kumekuwa na urasimu mkubwa wa taratibu wa kutolewa notice tajwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya Afisa Ardhi Mteule toka Ofisi ya Kanda-Moshi kuja Mkinga kufanya zoezi la uhakiki mwanzoni mwa mwezi Aprili hadi leo hakuna kinachoendelea licha ya kukumbushwa mara kadhaa kwa simu na Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Mkinga. Naiomba Wizara iingilie kati jambo hili ili ujanja ujanja usitumike kuvuruga mchakato wa kuwapatia haki wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo haya, naunga mkono hoja. Aidha, naomba Wizara ya Ardhi kwa kushirikiana na TAMISEMI itusaidie Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga tuweze kuajiri Afisa Ardhi Mteule ili atusaidie kuondoa migogoro.