Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya na fursa ya kuchangia leo. Nimpongeze Waziri, Naibu Waziri na Katibu Mkuu na timu yake ya wataalam kwa kazi nzuri sana waliyofanya. Naomba masuala machache yafanyike ili kuboresha huduma ya Wizara ya Ardhi inayoendana na maendeleo ya makazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza jimboni kwangu, Serikali iharakishe kupitia mgogoro wa ardhi ya miaka mingi iliyotutesa na kusababisha migogoro hii kutumika kisiasa wakati wote. Migogoro ya Vijiji vya Ayamango, Gedamar na Gidejabong na TANAPA Tarangire, Serikali ndio iliweka vijiji hivyo hapo katika eneo la hifadhi. Wapatiwe eneo mbadala na pia shamba la Galapo Estate pia lisitolewe viwanja na badala yake iwe eneo la kuwapa hao wanaondolewa katika hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba suala la mashamba ya Bonde la Kisu, migogoro ya ekari 25. Tunaomba pale mapendekezo ya Wilaya na Mkoa zifanyiwe kazi pia Serikali itoe tamko la kuvamia mashamba na kuharibu mali ya wawekezaji ambayo wana haki na wanatimiza wajibu kisheria. Pia tunaomba ardhi ya kilimo ilindwe kisheria ili matumizi ya ardhi ya kilimo isiweze kubadilishwa bila Bunge kupitisha mabadiliko hayo kuwa ya makazi, viwanda au matumizi mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaomba Wizara iandae program ya kila Halmashauri kupata vifaa vya kupima kwa mkopo pamoja na vifaa vya kuweka kumbukumbu ya hati na vifaa vya kuchapa hati. Kwanza tutaweza kulipa ndani ya muda mfupi. Leo Halmashauri nyingi hawana bajeti ya kununua kwa fedha taslim.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaomba Wizara ya Ardhi iangalie namna ya kulipia gharama ya matumizi ya satellite. Hii itafanya upimaji kwa ramani iliyopo inakuwa bora na wa uhakika. Leo hii ramani nyingi zina tatizo sababu hawana fursa ya kutumia hiyo huduma ya satellite.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri pia tuwe na sheria ya kuzuia kuuza kiholela kwa ardhi hasa yenye hati ya kimila ili wenye uwezo wasinunue ardhi nyingi na wasiokuwa na uwezo kukubali kuwa vibarua na mbele ya safari tutakuwa na hatari sawa na Afrika Kusini na nchi zingine kama Kenya ya wachache kuwa na ardhi. Leo kila Mtanzania ana uwezo wa kuwa na ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba Serikali itumie fursa hii kutoa tamko kwa umma na sisi wanasiasa kutumia ardhi kisiasa na kuhamasisha vurugu kwa maslahi ya kisiasa na hasara kwa umma na wamiliki wa ardhi, hifadhi mbalimbali na vyanzo vya maji.