Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Risala Said Kabongo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. RISALA S. KABONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii muhimu kwa utoaji huduma katika sekta ya Ardhi. Migogoro ya ardhi nchini ni mikubwa mno hivyo naomba kuendelea kuishauri Serikali, kupitia Wizara hii ya Ardhi kuweka mpango madhubuti, kutenga maeneo ya wakulima na wafugaji ili kuepuka migongano hii ambayo haina tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Nyumba la Taifa (NHC). Kumekuwa na changamoto kubwa ya kodi nyingi kwenye ujenzi wa nyumba za NHC, hivyo kupelekea nyumba hizi kuendelea kuuzwa bei ya juu. Kama Mjumbe wa Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii nimekuwa nikitoa maoni yangu kuhusu Wizara ya Miundombinu, Nishati na Madini,Maji na Umwagiliaji ili kuona ni namna gani ya kupunguza mzigo kwa NHC ambao imekuwa ikiubeba na kugharamia kila kitu na kufanya gharama hizi kwenda kwa mnunuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama kubwa za upimaji wa ardhi; kumekuwa na malalamiko makubwa kwenye suala la upimaji wa ardhi na hivyo kupelekea wananchi wengi kutokupima ardhi zao. Ushauri, Wizara ya Ardhi ishirikishe sekta binafsi katika suala la upimaji. Maeneo mengi kwenye Halmashauri zetu hayajapimwa hivyo kufanya ugumu wa uwekezaji katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri Wizara ya Ardhi kujikita kwenye mikoa mipya na inayokuwa ili kuendelea kupanga mipango miji ambayo ni tatizo kubwa sana katika nchi yetu, sambamba na kujenga maeneo ya uwekezaji kuvutia wawekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Songwe ni mkoa mpya, nashauri Wizara itoe upendeleo wa kipekee kuendeleza Mkoa wa Songwe kwa kupima viwanja, kutenga maeneo ya uwekezaji ili kuvutia wadau mbalimbali kuendeleza mkoa, sambamba na ujenzi bora wa nyumba za kisasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.