Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Ardhi katika maisha ya mwanadamu ndiyo rasilimali msingi katika maendeleo ya mwanadamu kwa vile miundomisingi yote hufanyika juu ya uso wa nchi. Uso wa asili, maji, barabara, Maziwa, reli, makazi na shughuli za kilimo, wanyama wa kufugwa pamoja na pori la akiba na hifadhi zote ziko juu ya uso wa nchi na kwa ajili hiyo basi ni vema Serikali kupitia Wizara hii ikajipanga kikamilifu kupata mipango miji iliyosanifiwa kikamilifu na kuendelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo changamoto mbalimbali zinazoikabili Sekta ya Ardhi nchini ikiwemo kubwa kabisa uhaba wa wataalam pamoja na vitendea kazi hali inayopelekea kutokuwepo kwa matumizi bora na endelevu ya ardhi mjini na vijijini. Ongezeko la watu pamoja na mifugo ni changamoto nyingine kubwa inayopelekea mwingiliano wa shughuli za kibinadamu kwa maana ya wakulima na wafugaji pamoja na changamoto ya ucheleweshwaji wa malipo ya fidia kwa wananchi ambao ardhi yao inatwaliwa kwa ajili ya shughuli za uwekezaji. Katika sekta mbalimbali ikiwemo kilimo, viwanda maeneo ya kimkakati kama vile, special economic zone na kadhalika. Uharibifu wa mazingira vile vile hufanyika juu ya uso wa nchi. Hivyo basi, ipo haja kwa Wizara hii kuwezeshwa kiutendaji kwa kuongezewa bajeti yake ili iweze kuajiri wataalam wengi zaidi pamoja na vitendea kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya yetu ya Mbogwe tunayo nafasi nzuri sana ya kuweza kujipanga vizuri katika Sekta hii ya Ardhi kwa vile wilaya yetu ni mpya kabisa hata ujenzi holela haujawa wa kiwango cha juu. Tunachohitaji Wilaya na Halmashauri ya Mbogwe ni kuunga mkono katika jitihada za kuipima ardhi yetu. Hivyo basi, tunaiomba Wizara ituangalie wananchi wa Mbogwe kutupatia Afisa Mipango Miji ili asaidie katika kupanga kitaalam wilaya yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa jitihada za kupata maendeleo katika shughuli za upimaji Wilayani Mbogwe Mfuko wa Jimbo umechangia ununuzi wa kifaa cha upimaji kiitwacho Total Station, kinachotakiwa kingine kiitwacho differential ili tuweze kukamilisha uchapishaji wa upimaji wa ardhi hasa viwanja na mashamba ya wananchi na hatimaye waweze kumilikishwa kisheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalipongeza kwa dhati Shirika la Nyumba NHC kwa kazi nzuri sana linazozifanya. Naishauri Serikali kuliwezesha Shirika hili ili liweze kujenga nyumba nyingi zaidi nchini ikiwepo Wilayani Mbogwe. Naunga mkono juhudi na jitihada zinazoendelea kufanywa na Wizara hii. Ombi, letu Mbogwe ni kupewa Afisa Mipango Miji katika Halmashauri ya Wilaya Mbogwe pale Wizara itakapoanza kuajiri watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.