Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Dr. Augustine Philip Mahiga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kuhitimisha mjadala wa hoja yangu kwa kutoa shukrani za pekee kwa Waheshimiwa Wabunge wote wa Bunge hili Tukufu kwa mchango wenu wa maneno na maandishi. Pia naamini kabisa kwamba Wizara yangu itaendelea kutegemea mawazo ya ujumla ya Bunge hili katika kutekeleza sera na mipango yake ya kuendeleza uhusiano na nchi za nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa shukrani za pekee kwa Naibu Waziri wangu ambaye amemaliza kujibu baadhi ya hoja zilizojitokeza. Pia natoa shukrani za pekee kwa wafanyakazi Wizarani kwangu, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, viongozi na wafanyakazi wote ambao tumeshirikiana katika kuandaa hotuba hii na kujibu maswali ambayo yamejitokeza ndani ya Bunge hili Tukufu ambapo jumla ya Waheshimiwa Wabunge zaidi ya 30 wamechangia katika hoja hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kujibu hoja zote zilizowasilishwa ndani ya Bunge lako Tukufu, moja baada ya nyingine lakini kutokana na uchache wa muda hoja zote nitazijibu kwa maandishi kama yatakavyowafikieni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea pale alipoishia Naibu wangu. Je, Serikali haioni kuwa kutosafiri mara kwa mara kwa Mheshimiwa Rais nje ya nchi katika ziara rasmi au kushiriki Mikutano ya Kimataifa kwa kuzingatia kubana matumizi kunadhoofisha ushirikiano na ukuaji wa mahusiano ya kidiplomasia na mataifa mengine? Inapotokea kiongozi anasafiri kutafuta fursa na kujenga mahusiano ya nchi na Mashirika ya Kimataifa panakuwepo na kubezwa sana kwa safari hizi pamoja na maelezo mazuri sana ambayo yamekuwa yanatolewa mara kwa mara na Wizara yangu na Wizara nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande mwingine, inapotokea safari ya kwenda nje na kiongozi akaamua kutuma msaidizi wake kumwakilisha kwenye safari hizo kiongozi huyo anatuhumiwa kwamba anadhoofisha mahusiano. Hapo Wizara yangu inajiuliza, ni lipi jema hasa? Ukisafiri unaitwa mtalii na usiposafari unaua mahusiano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais kama Mwanadiplomasia namba moja anatekeleza majukumu yake kwa ufanisi na mafanikio makubwa. Kwa miaka mingi Tanzania inaheshimika katika medani ya kimataifa. Heshima hiyo imechangiwa sio tu kwa safari za viongozi na Serikali bali kwa kazi nzuri wanazofanya ndani ya nchi, Afrika Mashariki na Balozi zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Awamu hii ya Tano, Tanzania imeshatembelewa na viongozi wengi wa Mataifa makubwa yaliyoendelea na yale yanayoendelea na ambao walioambatana nao, ujumbe mkubwa wa wafanyabiashara hao, wamekuja na kufanya mazungumzo yenye tija kabisa kwa nchi yetu. Lazima ifahamike kwamba watu wanaokuja kututembelea wanaridhika kabisa na mazungumzo baada ya wao kuja kututembelea hapa na yameleta tija kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lingine ni kwa nini michago ya kifedha ya baadhi ya washirika ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki imekuwa haitolewi kwa ukamilifu? Jibu, michango yote ya Tanzania ndani ya Jumuiya hiyo imeshalipwa na hatudaiwi hata senti moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa za Gazeti la nchi ya Kenya la Daily Nation la tarehe 14 Mei, 2017 lilimnukuu Kiongozi wa Bunge katika Bunge la Kenya akitoa shutma kuwa Tanzania inapanga kuingilia mchakato wa uchaguzi wa nchi hiyo. Je, Serikali haioni kuwa taarifa hiyo itaathiri mahusiano kati yetu na nchi ya Kenya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati natoa hotuba yangu nilisema moja ya malengo ya Sera ya Mambo ya Nchi za Nje ya Tanzania ni kutoingilia mambo ya ndani ya nchi nyingine. Tanzania imekuwa nchi inayofuata na kuheshimu misingi ya demokrasia, utawala bora, ujirani mwema na uhuru wa nchi nyingine hasa majirani zetu. Tanzania inaheshimu maamuzi ya nchi nyingine ya kujiamulia mambo yao wenyewe na kuchagua viongozi wanaowataka kama ambavyo sisi tumefanya kwa awamu zote tano tangu ya Mwalimu Nyerere hadi ya sasa ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Tanzania imekuwa mstari wa mbele katika kusuluhisha migogoro kwenye Bara la Afrika na hasa nchi zinazotuzunguka ikiwemo Jamhuri ya Kenya mwaka 2007 ilipoingia kwenye machafuko ya kisiasa baada ya uchaguzi. Ni kwa misingi hiyo, Wizara inapenda kuweka bayana kuwa Tanzania haijaingilia na haitakaa iingilie masuala ya ndani ya nchi nyingine. Ni vema waandishi wa habari wakaandika habari za kweli na kuacha kuzichonganisha nchi majirani na ndugu kama vile sisi na ndugu zetu Wakenya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, ni upi msimamo wa Tanzania kuhusu nchi za Morocco na Sahara Magharibi. Tanzania ni mojawapo wa NchiWwanachama wa Umoja wa Afrika waliounga mkono ombi la Morocco kurejea katika Umoja wa Afrika ikiamini suluhu ya mgogoro uliopo wa Sahrawi ya Magharibi utazungumzwa. Nifafanue kwamba

katika sera yetu ya kutofungamana na nchi yoyote tumeamua kuwa na mahusiano na Morocco kwa sababu Morocco ikiwa ni nchi ya tano yenye uchumi mkubwa katika Afrika tutakuwa tunajinyima fursa ya kufanya biashara na uwekezaji na nchi hii. Kuisusa siyo suluhu ya mgogoro wa Sahrawi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaamini kabisa kwamba ili kuisaidia Sahrawi, misingi yetu inayojulikana ya kulinda uhuru na heshima wa watu na makundi, suluhu inaweza kupatikana kwa mazungumzo. Baada ya miaka karibu 40 bila kupata suluhu tunaamini kwamba suluhu kati ya Morocco na Sahrawi itapatikana kwa mazungumzo ndani ya Umoja wa Nchi za Kiafrika ambapo Morocco imerudi na Tanzania itashiriki kikamilifu katika mijadala hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inataka Serikali kueleza msimamo wa nchi kuhusu mgogoro uliopo Syria, mgogoro kati ya India na Pakstan juu ya Kashmir pamoja na mgogoro kati ya nchi ya Marekani na washiriki wake dhidi ya nchi za Korea Kaskazini. Kwa misingi ile ile kwamba sisi hatufungamani na nchi zozote na suala hili la India na Pakstan ni la zaidi ya miaka 50 na wala halizungumzwi hata katika Umoja wa Mataifa. Nadhani hili ni suala ambalo nchi hizo mbili zinaweza kulizungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Syria itakumbukwa kwamba katika mageuzi ya Mashariki ya Kati yaliyoanzia Tunisia yakaenda Libya yakaikumba Misri yalifika Syria pale yakakwama. Sasa hivi ushindani kati ya upinzani na Serikali na vikundi mbalimbali vya upinzani imepelekea mataifa makubwa kuchukua nafasi tofauti zinazokingana. Katika hili, Tanzania inapendekeza kwamba suluhu ipatikane kwa mazungumzo. Kwa kuzingatia siasa yetu ya kutofungamana na upande wowote, sisi hatuwezi kuingilia mvutano huo wa ndani ya Syria na makundi yale ambayo yanaunga vikundi hivyo yakiongozwa na mataifa makubwa ya duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kugusia suala lingine ambalo limeulizwa na Mheshimiwa Profesa Anna Kajumulo Tibaijuka. Anasema mpaka baina ya Tanzania na Uganda haupo vizuri na Serikali imejipangaje kuliweka vizuri suala hili ili pawe na maelewano na mkataba kwenye mpaka huu pamoja na mingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuwakumbusheni kwamba mipaka ya nchi za Kiafrika inatokana na maamuzi ya nchi za Kiafrika kwamba isibadilike na sisi nia yetu siyo kubadilisha mpaka huo lakini kuna wakati ambapo ni lazima tujaribu kufanya marekebisho kwa sababu wananchi wa pande zote mbili wanaoishi katika nchi hizi mara kwa mara wamekuwa hawaoni mstari ambao unatenganisha nchi hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baina yetu na Uganda tumeshafanya kikao huko Bukoba kuzungumzia suala hili ambapo katika pande mbili za mpaka kuna Waganda na Watanzania ambao wamevuka mpaka. Majadiliano haya yaliingia pia katika Tume ya Pamoja ya mazungumzo kati ya Uganda na Tanzania na tutaendelea kuyazungumza tena na tumepanga ndani ya mwezi ujao wa Juni tutaendelea kuzungumza. Nia siyo kubadilisha mpaka lakini ni kuwasaidia wananchi wa pande zote mbili kuelewa mpaka ulipo na kuleta tija zaidi katika ushirikiano na udugu wa nchi hizo. Nadhani hili linaeleweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nataka kumhakikishia Mheshimiwa Profesa Tibaijuka kwamba katika hotuba yangu nimeeleza kwamba Tanzania inachukua kila fursa ya majukwaa ya kimataifa kuzungumzia masuala ya uchumi. Kati ya majukwaa muhimu ya Umoja wa Mataifa ni Jukwaa la UNCTAD. Tumekuwa tukishiriki kikamilifu tangu mwaka 1964 na mazungumzo yanayoendelea pale ni ya tija kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala ambayo yanajitokeza sasa tutaendelea kuyaweka katika ajenda ya UNCTAD. UNCTAD itaendelea kuwa ni chombo muhimu cha nchi zinazoendelea na hasa pale inapokuwa kati ya mahusiano ya sisi tunaoendelea na nchi za nje. Kama vile ilivyo WTO (World Trade Organization), Jukwaa la UNCTAD ni muhimu kwa Tanzania. Kama alivyogusia Mheshimiwa kwa kuleta ajenda zetu pale masuala mengi ya mahusiano ya kibiashara na uwekezaji yanaweza kutatuliwa kwa kutumia chombo kile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la EPA, napenda ifahamike kwamba huu ni mkataba ambao Ulaya walitaka nchi za Afrika Mashariki kwa umoja wao waweke saini lakini baada ya uchambuzi tumeona kwamba kuna upungufu katika mkataba huo. Tatizo linalokuja ni kwamba katika nchi za Afrika Mashariki, nchi tano zinaendelea kufanya biashara na Ulaya na kupeleka bidhaa bila vikwazo lakini nchi moja ambayo ni Kenya yenye uchumi wa wastani, Ulaya walisema ifikapo Oktoba mwaka jana wao hawatanufaika na kile kipengele cha kuondolewa ushuru kama sisi wengine. Wakasema Kenya haiwezi kuendelea lakini sisi wote kwa pamoja lazima tuweke saini ili kuinusuru Kenya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukaiambia Kenya kwamba itakuwa vigumu kwa sisi kama mkataba huu ulivyo kwa sasa. Kuna haja ya kuchambua zaidi lakini tunaiambia Jumuiya ya Ulaya kwamba ivute subira na isiiwekee vikwazo Kenya kwa sababu Kenya ikisaini peke yake makubaliano hayakubaliki, hata ikisaini Kenya peke yake haikubaliki mpaka Kenya isaini pamoja na wenzake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwenye mkutano wa juzi wa nchi za Afrika Mashariki tumeamua kwamba kwa Umoja wetu wa Afrika Mashariki na Mwenyekiti wetu mpya Yoweri Museveni ataongoza ujumbe maalum kwenda Brussels mwezi ujao na kuiambia Jumuiya ya Ulaya kwamba wasubiri wasiweke vikwazo kwa Kenya mpaka hapo tutakapokubaliana sisi wanachama wa Jumuiya kutazama upya masuala ambayo yanatukera. Ndiyo maana Bunge hili Tukufu lilitoa ushauri ambao unaheshimika kabisa kwa Serikali yetu na kwa Mheshimiwa Rais kwamba tusiweke saini mkataba ule kwa sababu una upungufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na maamuzi ya juzi, Museveni atakwenda kufanya mambo matatu. La kwanza ni kuiambia Jumuiya ya Ulaya kwamba vuteni subira, msiiwekee vikwazo au msiifungie biashara Kenya. La pili, chini ya Uenyekiti wa President Museveni sisi Wanajumuiya ya Afrika Mashariki tutakaa tena kutazama upya kipengele kwa kipengele mahali ambapo panahitaji marekebisho na Ulaya watusubiri tukubaliane kwa sababu nchi moja hata ikisaini, haina tija, haina nguvu mpaka wote tusaini mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu ni kwamba endapo hiyo itashindikana kuna kipengele katika Mkataba wa East Africa ambacho kinaruhusu kitu kinaitwa variable-geometry. Variable-geometry ni kwamba ninyi wanachama mnamruhusu mwenzenu aendelee kuweka saini mkataba ninyi wengine mkiwa bado mnajipanga. Hata hivyo, dhamira ya nchi za Afrika Mashariki ni kwamba tuweke mkataba huu kwa pamoja na mpaka tufike kwenye variable- geometry itakuwa baada ya kwamba tumeshindwa kuwaambia Ulaya kwamba wavute subira ili tuweze kurekebisha mapatano hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ndani ya mwezi ujao ni matarajio yetu kwamba Umoja wa Ulaya hautaiwekea Kenya vipingamizi vya biashara. Sisi tutaendelea kutazama mkataba ule na pale ambapo Kenya inaona umuhimu wa kuendelea sisi tutaridhia kwamba mwenzetu aendelee kwa kutumia kipengele kinachoitwa variable- geometry huku tukiendelea kuzungumza ili hatimaye sisi wote tuweze kuweka mkataba huo kwa pamoja. Nadhani hilo linaeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mengine Mheshimiwa Fatma Hassan Toufiq ameshauri Serikali iwe na majengo yake kwenye Ofisi za Balozi nje ya nchi ili kupunguza gharama za kulipia kodi za pango. Aidha, Wizara iwe na mkakati wa muda mrefu na mfupi, kuendeleza viwanja ambavyo Serikali imepewa nje ya nchi kupitia Balozi zetu na kutumia utaratibu wa mikopo ya benki ya hire purchase na mortgage finance ili iweze kuviendeleza viwanja hivyo kwa kujenga majengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kuendeleza na kukarabati majengo ya ofisi na makazi ya watumishi Balozini na imekuwa ikitekeleza jukumu hilo kwa kutumia fedha za bajeti ya maendeleo zinazopangwa katika kila kipindi cha mwaka wa fedha. Mpango wa Wizara wa miaka 15 wa ujenzi, ununuzi na ukarabati wa majengo ya ofisi na makazi ya watumishi Ubalozini ulianza kutekelezwa mwaka wa fedha 2012/2013.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara imefanikiwa kutekeleza miradi mbalimbali kwenye Balozi zetu kama vile kufanikisha ujenzi wa jengo la Ofisi ya Ubalozi wa Tanzania New Delhi India; ununuzi wa jengo la Ofisi ya Ubalozi wa Tanzania Washington DC – Marekani; ununuzi wa jengo la Ofisi ya Ubalozi wa Tanzania New York – Marekani; ununuzi wa Jengo la Ofisi na Makazi ya Balozi, Ubalozi wa Tanzania Paris – Ufaransa; ukarabati wa makazi ya Ubalozi wa Tanzania Nairobi – Kenya na ukarabati wa makazi ya Balozi wa Tanzania Tokyo – Japan.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka wa fedha wa 2016/2017, Wizara itakamilisha ukarabati wa jengo la ghorofa tisa la Ofisi na Makazi lililopo Ubalozi wa Tanzania Maputo – Msumbiji; ukarabati wa makazi ya Balozi na nyumba za watumishi zilizoko Ubalozi wa Tanzania Stockholm - Sweden na ukarabati wa Jengo la Ofisi na makazi ya Balozi yaliyoko Khartoum - Sudan. Hivi sasa Wizara inaandaa mpango mwingine wa miaka 15 wa ujenzi, ununuzi na ukarabati wa majengo ya Ofisi na Makazi ya watumishi Ubalozini utakaoanza kutekelezwa mwaka 2017/2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya miradi itakayotekelezwa ni ukarabati wa jengo la ofisi na makazi ya watumishi kwenye Balozi za Tanzania Harare – Zimbabwe; Kampala – Uganda; Beijing - China, Pretoria – Afrika Kusini na Cairo – Misri. Vilevile ukarabati wa nyumba za Ubalozi zilizoko kwenye Ubalozi wa Tanzania Lilongwe – Malawi na Kinshasa – DRC; ukarabati wa jengo la zamani la Ofisi ya Ubalozi ulioko Washington – DC; ukarabati wa miundombinu ya Chuo cha Diplomasia kilichopo Kurasini na ujenzi wa makazi ya Balozi, Ubalozi wa Tanzania Addis Ababa – Ethiopia na Ofisi ya Ubalozi wa Tanzania Muscat, Oman.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikakati ya kutekeleza mpango huu ni kuendelea kutumia bajeti ya maendeleo ya Serikali, kuishirikisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kama vile Taasisi ya Miradi ya Maendeleo ya Miundombinu (UTT-PID) na kwa kutumia utaratibu wa karadha katika kutoa mikopo ya kutekeleza miradi ya maendeleo Ubalozini kwenye nchi za uwakilishi ambapo utaratibu huo unaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kuwaonyesha kwamba tuna mkakati na kutoa mifano halisi ingawa ombi letu ni kwamba Bunge hili Tukufu litusaidie kupitisha maombi yetu ili tuweze kuanza kutekeleza haraka. Hii pia inajibu hoja kwamba tunachelewa kupeleka pesa kwenye Balozi zetu, kama Hazina ikitupatia pesa kwa wakati tutajitahidi kupeleka pesa hizo ili zikafanye kazi inayotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine linahusu upungufu wa wafanyakazi kwenye Ofisi za Balozi ambapo hakuna wataalam mbalimbali kama Wachumi, Wanasheria, wataalam wa utalii na Maafisa Uhamiaji ili kufanikisha Diplomasia ya Uchumi. Wizara imerejesha kiasi kikubwa cha watumishi waliomaliza muda wao katika Balozi zetu nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa tupo katika hatua ya kurejesha waliobaki ili kutekeleza hatua ya pili ya kupeleka watumishi nje kulingana na mahitaji. Tuko katikati ya mchakato huo, hatuwezi kupeleka watu kabla ya hatujarudisha watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara na taasisi zote zilizo chini ya Wizara zina tovuti na mtandao wa kijamii ambao una taarifa muhimu kuhusu huduma zinazotolewa na Wizara au taasisi husika zikiwemo taarifa za uwekezaji. Aidha, taarifa hizo zinapatikana kwa upana katika tovuti zinazohusika na taarifa zaidi kuhusu kazi zinazoendelea katika Balozi zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Cosato Chumi ameuliza na kwa kweli ametoa ushauri, Wizara kwa kushirikiana na mamlaka nyingine isimamie suala la makubaliano ya kutoza kodi mara mbili baina ya nchi yetu na nchi nyingine yaani double taxation na kulinda wawekezaji wa nje nchini (protection of investment). Wizara inapokea ushauri wa Mheshimiwa Mbunge na tutalifanyia kazi pendekezo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia anashauri Wizara ijenge majengo yake yenyewe katika viwanja, nadhani hilo nimeshalijibu. Kuhusu upungufu wa wafanyakazi, hilo pia nimeshatoa majibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeulizwa, ni lini Wizara itapeleka Balozi wa Heshima Lubumbashi, Jamhuri ya Demokrasia ya Congo. Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na wawakilisha kamili wa Ubalozi wenye makazi katika nchi mbalimbali duniani na Konseli kuu katika maeneo ya kimkakati. Kutokana na mwingiliano mkubwa wa biashara baina ya wafanyabiashara wa Tanzania na Mashariki mwa Congo, Wizara imeanza utaratibu wa kupata Mwakilishi wa Heshima ambaye atakidhi mahitaji ya Watanzania wanaoishi Mashariki mwa Congo pamoja na wafanyabiashara watokao Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivi sasa Serikali imefungua Balozi sita mpya ambazo nilizitaja, lakini tutaendelea pia kutazama maeneo mengine ambayo ni muhimu na hasa kwa vile Mabalozi wanasimamia nchi nyingi na kuna umuhimu wa kuwa na Konseli Jenerali na hilo katika mwaka ujao tutalipa kipaumbele, siyo tu katika DRC lakini kuna nchi nyingine ambazo tumeona umuhimu wa kuwa na Konseli Jenerali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeulizwa kuhusu kunyanyaswa kwa Watanzania wanaokwenda kufanya kazi katika nchi za Uarabuni hususan Oman. Wameomba kupata taarifa juu ya kifo cha Mtanzania huyu anayesemekana kuwa aliuawa nchini humo. Aidha, wameshauri Wizara ishirikiane na Wizara ya Kazi na Ajira ili kuwepo na utaratibu ambao utaondoa unyanyasaji huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 14 Machi, 2017, Wizara ilipokea taarifa kutoka Ubalozi wetu nchini Oman kuhusu kifo cha kutatanisha cha Mtanzania Bi. Husna Issa Abdallah, mwenye umri wa miaka 28 aliyekuwa akifanya kazi za ndani. Taarifa hiyo imeeleza sababu za kifo hicho kwamba marehemu alijirusha na kuanguka kutoka ghorofa ya kwanza ya nyumba ya mwajiri wake huku mwajiri na familia yake wakiwa wameketi sebuleni. Aidha, taarifa ya Serikali ya Oman imeeleza kuwa kifo hicho kimetokana na yeye mwenyewe kujiua kwa kujirusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kupokea taarifa hiyo, Ubalozi ulichukua hatua ya kuwasiliana na ndugu wa marehemu ili kupanga mipango ya kusafirisha mwili. Aidha, Ubalozi ulisaidia kushughulikia documentation zote zinazohusiana na usafirishaji wa mwili wa marehemu. Kwa upande wake, aliyekuwa mwajiri wa marehemu alijitolea kulipa gharama zote za kusafirisha mwili hadi kijijini kwao na pia kugharamia gharama za mazishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Wizara ilipokea barua kwa mtu aliyejitambulisha kuwa ni ndugu wa marehemu kudai kuwa yeye ana nyaraka zinazoonyesha taarifa tofauti na ile tuliyonayo. Tulimwandikia barua ya kuomba nakala ya document hizo ili tuweze kufuatilia kupitia Ubalozi wetu mpaka sasa hatujapata jibu kutoka kwa ndugu huyu wa marehemu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, ili kupata suluhu ya kudumu kuhusu changamoto zinazowakuta Watanzania wanaokwenda kufanya kazi nje ya Mashariki ya Kati, Wizara inaendelea kusisitiza Watanzania wanaoenda kufanya kazi nje ya nchi hususani katika eneo la Mashariki ya Kati, wafuate taratibu zilizowekwa na Wakala wa Ajira Tanzania (TaESA) kwa kutumia mawakala waliosajiliwa rasmi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa baadhi ya watumishi wanaotoka Balozini wamekuwa wakipelekwa na Serikali katika Ofisi mbalimbali ili kupata ujuzi katika sekta hizo lakini pia ili kupeleka ujuzi walionao. Suala hili pia limezungumzwa kwa kirefu katika hotuba yangu na lipo kwenye kitabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ni kutoka kwa Mheshimiwa Haji Khatib, ili kumaliza tatizo la kukamatwa na kufungwa kwa wavuvi wetu nchini Kenya, ni vema Serikali ya Tanzania na Kenya ikarudi kwenye mkataba uliosainiwa na Mawaziri wa Mambo ya Nje wa nchi hizi mbili mwaka 1975. Wizara kwa kutumia mahusiano yake mazuri na nchi rafiki imeingia makubaliano na Serikali na Wizara hii itahakikisha kwamba tunazungumza tena na kutazama mkataba huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipokuwa kule Pemba tukitoa mafunzo na semina, suala hili tulilipokea na tunaahidi kwamba tutaendelea kulifanyia kazi na hasa katika kuzingatia mahusiano ya biashara na usafiri kati ya wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki yaani Tanzania na Kenya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeambiwa pia kwamba Wizara ifanye maboresho katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha, hususani upande wa vyoo vya watu mashuhuri (VIP) na vyoo vingine vya kawaida. Tunachukua ushauri huo. Ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itoe maelezo juu ya uvumi kuhusu unyanyasaji wa Watanzania katika nchi nyingine ambazo tuna uhusiano nao. Majibu ni yaleyale tuhakikishe kwamba tunatoa elimu kwa vijana wetu ili wanapokwenda huko waweze kuwa wamepewa kibali na wanasimamiwa na agency ambazo zimewekwa za kupeleka watu kufanya kazi nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Maria Ndila Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum, anasema kuwe na sera moja ya Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki zinazotumia Ziwa Victoria juu ya uvuvi na forodha. Kwa utaratibu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, sheria inayoweza kutumiwa na nchi zote za Jumuiya hujadiliwa kwa pamoja na nchi wanachama zikachukua vipengele vinavyovitaka katika kila nchi. Hivyo, Sheria ya Uvuvi ya Tanzania ikirekebishwa haitakuwa kigezo cha kutumika katika nchi zote wanachama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa namna gani Zanzibar inanufaika na uwekezaji unaofanywa na Shirika la AICC kule Arusha. Ni kweli AICC ni Shirika la Muungano kwa kuwa liko chini ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambayo ni Wizara ya Muungano. Uwekezaji unaofanywa na AICC unanufaisha wananchi pande zote za Muungano. Hii ni kutokana na ukweli kuwa gawio linalopatikana linawasilishwa Wizara ya Fedha na Mipango ambayo yenyewe ina mamlaka ya kutoa gawio Zanzibar kulingana na utaratibu uliopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mary Deo Muro, Mbunge wa Viti Maalum, alishauri Serikali ipeleke …

MWENYEKITI: Dakika moja.

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Fedha zilizoidhinishwa na Bunge kwa wakati Balozini. Nadhani hili tumeshalizungumza na itategemea uhusiano wetu baada ya ninyi kutusaidia katika kuidhinisha pesa husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna masuala kadhaa ambayo yameulizwa hapa, mengi tutayajibu kwa maandishi na tunatoa heshima ya pekee kwa mchango huu. Masuala mengi ni ya kuchangia kuboresha utendaji kazi wa Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani huu ndiyo mwisho, naomba kutoa hoja.