Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Othman Omar Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Gando

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. OTHMAN OMAR HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naanza kwa kuipongeza hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani kwa ushauri uliotolewa kwa Serikali. Mchango wangu uko katika Shirika la AICC ambalo inamilikiwa au liko chini ya Wizara ya Mambo ya Nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, AICC ni Shirika la Muungano ambalo kwa kipindi cha miaka 39 toka kuanzishwa kwake limefanikiwa kufanya uwekezaji wa kutosha kwa upande mmoja tu wa Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na miradi ambayo tayari imeshaelekezwa, bado AICC inatarajia kutekeleza miradi mipya kama vile ujenzi wa Taasisi ya Kimataifa eneo la Lakilaki (Arumeru), hospitali ya kisasa, maonesho, shughuli za mikutano na burudani. Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Kilimanjaro International Convention Centre (KICC), Convention Centers’ katika Miji ya Mwanza, Mtwara na Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji unalenga kutengeneza ajira na hivyo kunyanyua shughuli za kiuchumi kwa maeneo husika. Hivyo basi, ni kwa namna gani Zanzibar inafaidika na uwekezaji unaofanywa na Shirika la AICC?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema Zanzibar ni sehemu ya Shirika la AICC, je, ni kwa nini Shirika bado halijafikiria kufanya uwekezaji katika visiwa vya Zanzibar wakati uchumi wa visiwa hivi unayumba?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na Zanzibar kuwa na uchumi usioridhisha, lakini Zanzibar ina mazingira mazuri ya kuvutia biashara ya utalii, biashara ambayo shirika ndiyo kiini cha shughuli zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kikao cha Kumi katika Mkutano wa Sita cha tarehe 10/02/2017, Mheshimiwa Naibu Waziri wa Mambo ya Nje alijibu swali la msingi Na.110 lililohusu gawio la Zanzibar. Mheshimiwa Naibu Waziri alisema kuwa gawio linapelekwa katika Mfuko Mkuu wa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya majibu hayo, Mheshimiwa Waziri wa Fedha alinyanyuka na akasema kwamba AICC haijawahi kupata gawio na kwamba Joint Finance Commission na Ofisi ya Msajili wa Hazina wameunda kikosi kazi ili kusaidia kituo kupata faida na kuleta gawio Serikalini kuanzia mwaka ujao wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha yanakizana na yale ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na kwa hiyo, yamelenga kuwadanganya Wazanzibari kuhusiana na mapato ya AICC. Mbali na hayo, majibu ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha pia yanakinzana na taarifa ya Msajili wa Hazina, lakini pia na taarifa ya Shirika wenyewe la AICC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ya AICC inasema, nanukuu; “AICC kwa kipindi kirefu imekuwa ikijiendesha kwa faida bila kutegemea ruzuku ya Serikali na imekuwa ikichangia ruzuku ya Serikali na imekuwa ikichangia Mfuko Mkuu wa Serikali kwa kuzingatia maelekezo ya Msajili wa Hazina.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na mgongano huu wa taarifa zinazohusu faida zinazotokana na Shirika la AICC kati ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Shirika la AICC, binafsi ninaomba maelezo ya kina na yanayojitosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.