Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru pia kwa kunipa nafasi niweze kuchangia machache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nachukua nafasi hii kuwapongeza Mawaziri kwa kazi nzuri wanayoifanya, lakini vilevile nawapongeza kwa dhati Serikali ya Awamu ya Tano kwa jitihada kubwa ambazo imezifanya katika kukuza diplomasia ya kiuchumi na hatimaye kufanikisha kufungua Balozi sita ambazo ni Balozi mahususi kwa ajili ya kukuza biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo moja; nimeshangazwa sana na uchangiaji wa baadhi ya Wabunge humu ndani. Walipinga ndani ya Bunge hili wakisema kwamba Serikali ya Chama cha Mapinduzi Rais wake ni dhaifu. Leo hii tumempata Rais ambaye ni mchapakazi, tumempata Rais ambaye anasimamia maslahi ya umma, maslahi ya Watanzania masikini, wamegeuka na kusema kwamba anafanya maamuzi ambayo ni ya hovyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda kwanza nichukue nafasi kuweza kuwakumbusha, wanasema ukiwa mwongo usiwe msahaulifu. Ni wewe mwenyewe kaka yangu Mheshimiwa Lissu ulisimama na kusema kwamba CCM imempa fomu ya kugombea Urais fisadi Lowassa, lakini ni wewe mwenyewe ambaye ulizunguka kumnadi Lowassa katika nchi hii. Sasa naomba niulize swali, je, kuna maamuzi ya hovyo kama hayo kusema mtu ni fisadi na baadaye mzunguke kuanza kumnadi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kaka yangu Lema alisema kwamba ni heshima kwa Mungu kumzomea na kumpiga mawe mtu kama Lowassa, lakini wewe ndio ulizunguka nchi nzima kumnadi. Jamani mnapoongea maneno, msiwe wepesi kusahau. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niseme jambo moja, hawa watu wameshazoea sana kila kitu kinachofanywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi wamekuwa wakikipinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila kitu ambacho Serikali hii inafanya wao wamekuwa ni wapondaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sijashangaa kuona hawa wenzetu wawili wanaponda jitihada za Mheshimiwa Rais Magufuli, kwa sababu hawa kila kitu kinachofanywa wao wamekuwa ni wapondaji; wamejipa vyeo vya kuwa mtoto wa kambo kwamba kila kitu lazima wao walalamike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii inahitaji Rais kama Magufuli. Hata kama, hatuwezi kuona kwamba tunakuza diplomasia ya kiuchumi wakati tunaendelea kuibiwa. Kwa hiyo, huu utaratibu wa kuendelea kutetea wezi, tumeshauzoea, ninyi wenzetu kazi yenu kutetea wezi na ndiyo maana mko tayari kwamba Taifa hili liendelee kuibiwa dhahabu eti kwa sababu tu tunakuza diplomasia ya kiuchumi. Hilo jambo haliwezi kukubalika na tunaomba tumpe nafasi kama Rais aweze kutimiza majukumu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea kwamba mngekuja kushauri, lakini ninyi mmekuwa watu wa kulalamika. Kwa hiyo, napenda kusema kwamba Mheshimiwa Rais aendelee kuchapa kazi, huu ni wakati wetu wa sisi kuchapa kazi na hawa wenzetu waliojipa vyeo vya watoto wa kambo tuwaache waendelee kulalamika, hapa kazi tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba sasa niweze kuzungumzia suala la uhaba wa Maafisa katika Balozi zetu. Balozi zetu zinakabiliwa na uhaba mkubwa sana wa Maafisa… (Kicheko/Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)