Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na niungane na Wabunge wenzangu kwa kuwapongeza Mawaziri wa Wizara hii Mheshimiwa Waziri Mpango na Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Manaibu Katibu Wakuu, Wakurugenzi pamoja na Kamshina wa Bajeti kwa kazi nzuri wanayoifanya Wizarani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utaanza na Benki ya Maendeleo ya Kilimo na kama nilivyochangia wakati wa uchangiaji wa Wizara ya Kilimo ningeomba sasa benki hii ijikite kwenye mazao ya biashara. Kwanza benki hii ina tatizo la mtaji; kwa hiyo nashauri Serikali sasa iongeze mtaji wa benki hii vilevile bado matawi ni machache, nilishauri kwamba miongoni mwa maeneo ambayo yanatakiwa benki hii sasa ipeleke nguvu zake ni Kanda ya Kusini ambapo kuna uzalishaji mkubwa wa zao la korosho na kama mnavyofahamu zao la korosho mwaka huu ni zao ambalo linaongeza kwa kutuletea fedha za kigeni. Limeingiza zaidi ya dola milioni 700 kwa hiyo ni zao ambalo siyo la kubeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba benki hii sasa ijikite katika kutoa mikopo ya muda mfupi ili wakulima wetu wa korosho waweze kuwa na uwezo wa kununua pembejeo. Mkulima wa korosho anahangaika na shamba lake wakati wa palizi lakini unapofika wakati wa pembejeo anahitaji kupewa msaada. Kwa hiyo, naomba benki hii sasa ifungue matawi Kanda ya Kusini ili itoe mikopo kwa wakulima wa korosho na isijikite tu kwenye mazao ya chakula, kwa sababu ukiangalia kwenye kitabu cha Waziri ambacho amewasilisha kwenye mnyororo wa thamani. Mazao ambayo yameorodheshwa pale ni mazao ya chakula kuna mahindi, mpunga kwa hiyo tunaomba twende sasa kwenye zao la korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namba ya wakulima ambayo wamefaidika na benki hii ni wachache. Kwenye taarifa ya Waziri inaonesha kwamba ni wakulima 2,575, sasa hebu angalia nchi takriban asilimia 75 ya wananchi wanategemea kilimo, kwa kundi hili dogo ambalo limepata msaada ni kiasi kidogo sana. Kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri tuwe na mkakati kwanza tuongeze matawi tuongeze mtaji, lakini tuongeze na idadi ya wananchi ambao watafaidika na benki hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili, utahusika na taasisi ambazo ziko chini ya Wizara hii. Nizungumzie taasisi hiyo ya Uhasibu na nitajikita kwenye taasisi ya Uhasibu kwenye tawi la Mtwara. Taasisi hii ni nyeti na inatoa taaluma ambayo ni muhimu kwa sasa lakini mazingira ya kujifunzia na kujifundishia hasa kwa tawi la Mtwara hayaridhishi, hivyo naomba Wizara itenge fedha za kutosha ili ukarabati mkubwa ufanywe kwenye taasisi hii na hasa tawi la Mtwara ambapo vyumba vya madarasa havitoshi, hawana hosteli za kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto ambao wako pale wanahangaika kupanga mitaani na wanafunzi hususan wa kike si vema sana kwa sababu pale wanatoa certificate. Wengine wamemaliza Form Four juzi tu hawawezi kukaa nje ya familia yao, kwa hiyo wanafunzi wale wanaangaika. Ni vema kukawa na hosteli kubwa inayochukua wanafunzi wengi ili watoto wote ambao watapata udahili pale wakae katika mazingira ya Chuo cha Uhasibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa tatu nitajikita kwenye usimamizi na udhibiti wa matumizi ya fedha za umma, hapa kwenye kitabu chake Mheshimiwa Waziri amesema kwamba atajikita katika kuimarisha Kamati za Ukaguzi kwenye taasisi mbalimbali, lakini nimsihi sio Kamati za Ukaguzi tu, hebu atuelekeze katika kuimarisha vitengo vya ukaguzi wa ndani hasa kwenye mamlaka ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiimarisha vitengo vya ukaguzi wa ndani kwenye mamlaka ya Serikali za Mitaa, tutakuwa tumeokoa mambo mengi sana kwa sababu Mkaguzi wa Ndani ndiyo jicho la kwanza la Afisa Masuuli kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa, hivyo naomba tujikite katika kuimarisha Kamati za Ukaguzi lakini ofisi ya wakaguzi wa ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia hali ilivyo sasa hivi kwa kweli inasikitisha, utakuta kwenye Halmashauri nyingine mkaguzi wa ndani ni mmoja hana gari, hana vifaa vya kufanyia kazi, kwa hiyo hawezi kufanya kazi yake vizuri, akitaka kwenda kukagua usambazaji wa madawa na utoaji wa huduma katika zahanati anamwomba msaada DMO, sasa yule mkaguliwa ndiyo anampa posho, anampa gari, hata nguvu ya kukagua pale inapungua. Kwa hiyo, naomba Wizara sasa ijikite licha ya kuangalia tu Kamati za Ukaguzi tuangalie na kitengo hicho ambacho ni muhimu na nyeti katika kudhibiti matumizi ya fedha zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hiyo tu katika suala la Usimamizi wa Fedha za Serikali tuingalie kwa jicho la pekee Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Mwaka jana tuliona alivyofanya kazi nzuri, alikagua taasisi nyingi lakini fedha hakupewa kwa wakati. Kwa hiyo ilibidi aji-stress, naomba CAG apewe fedha za kutosha lakini siyo za kutosha tu, bali kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukaguzi una misimu yake, ukimpa CAG fedha kuanzia Januari hazimsaidii sana, kwa sababu wakati ule na timu yake wanajifungia mahali kwa ajili ya report writing. Tujitahidi kutoa fedha za kutosha kama ilivyo kwenye bajeti yake kwa kipindi cha Julai hadi Novemba, tukifanya hivyo tutakuwa tumemsaidia CAG na atafanya kazi yake kwa ufanisi na atakuwa amekwenda kuangalia fedha zetu ambazo tumepeleka katika miradi yetu ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu mwingine utajikita kwenye uhakiki na ulipaji wa madeni ya Watumishi wa Umma na Wazabuni. Kama walivyosema wenzangu kwamba tuongeze kasi ya uhakiki wa haya madeni. Kwenye taarifa pale imeonekana kwamba tumeshaanza kulipa madeni ya wazabuni, kwenye deni la trilioni tatu tumelipa milioni 796. Ningeomba Serikali yangu isiwe chanzo cha kuua mitaji ya wafanyabiashara wadogo, tulipe madeni kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tulipe madeni ya Watumishi kwa wakati ili kuongeza morali kwa watumishi. Watumishi wakilipwa stahili zao morali inaongezeka, lakini madeni kwa watumishi yasipolipwa kwa wakati kwanza yanafifisha ari kwa watumishi na hivyo mtumishi anakwenda kazini wakati hana ari ya kufanya kazi. Kwa hiyo, naomba kwenye trilioni tatu kwa sababu tumeana kulipa milioni 796 basi tujitahidi ili tulipe deni hili ili wazabuni waweze kutoa huduma lakini na watumishi waweze kufanya kazi ili tuliyoitarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa mwisho unahusu mfuko wa huduma ndogo za fedha (microfinance) na hii ni taasisi muhimu sana. Nchi za wenzetu wanawapa kipaumbele sana SMEs, kwa hiyo na sisi hizi taasisi za microfinance hebu tuzipatie fedha za kutosha na tupunguze mifuko. Kwenye Mfuko wa Uwezeshaji tumeambiwa kuna mifuko 19, sasa ile mifuko ni mingi sana. Tupunguze tuwe na mifuko miwili au mitatu ambayo itatoa huduma ambayo inajulikana na wananchi watakuwa na taarifa za kutosha. Kwa hiyo, itakuwa wanapohitaji mikopo midogo midogo au uwezeshwaji wanakwenda kwenye taasisi hizo na kuhudumiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuunga mkono hoja na nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.