Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kushika kalamu na kutoa mchango wangu kwa njia hii ya maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze mchango wangu kujadili juu ya Mashirika ya Umma yaliyouzwa kwa bei ya kutupwa. Hapa nitajikita zaidi kwenye Shirika lililokuwa la Usagishaji la Taifa (NMC). Shirika hili lilikuwa na Matawi karibu katika kila mkoa lakini uuzwaji wake haukuzingatia thamani ya mali za shirika hilo. Mfano, kiwanda cha mahindi cha Plot 33 hadi leo hakijulikani kama kimeuzwa au hakijauzwa. Ndugu Amani na Ndugu Mwaipopo walikuwa Wakurugenzi wa Shirika hilo wamehodhi kiwanda hiki kwa faida yao, mpaka sasa mgogoro mkubwa baina ya hao niliowataja na mnunuzi wa awali ambaye alishinda tenda ya shilingi milioni mia sita (600,000,000/=).

Mheshimiwa Mwenyekiti, malipo kwa wastaafu, Serikali imekuwa na kigugumizi kikubwa juu ya kulipa wastaafu hasa kwa wale waliokuwa katika mashirika yaliyouzwa. Mfano, wafanyakazi waliokuwa Shirika la NMC Tawi la Kurasini hadi leo Serikali imeshindwa kuwalipa madai yao ingawa kesi yao imekwishaamuliwa. Hata hivyo, wafanyakazi wa TTCL nao wanaidai Serikali mapunjo yao, nao hadi leo hakuna kinachoendelea. Hawa ni watu walioitumikia nchi hii kwa uadilifu mkubwa. Hivyo ni bora Serikali ikamaliza na watu hawa kwa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mafao kwa wazee ambao hawakuwa wakifanya kazi katika mashirika au Serikalini, hawa ni wakulima je, Serikali ina mpango gani na wazee hawa ambao wakati wao walitulisha kwa chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu wingi wa kodi, bidhaa zinazotengenezwa hapa nchini zinashindwa kushindana kwenye soko kwa kuwa gharama za uzalishaji ni kubwa sana zinazochangiwa kwa kiasi kikubwa na wingi wa kodi na wingi wa mamlaka zinazofanya kazi zinazofanana. Mfano, TFDA, TBS, OSHA, FIRE na kadhalika, jambo hili ni muhimu sana kuangaliwa upya, Wawekezaji wanashindwa kuja kuwekeza kwa wingi huu wa kodi na mamlaka za usimamzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekezaji katika kilimo; sekta hii haijapewa kipaumbele kama inavyostahili shida kubwa hapa ni upatikanaji ardhi kwa wawekezaji. Jambo la uhaulishaji wa ardhi imekuwa ni kikwazo. Mfano, katika Halmashauri ya Liwale imepata mwekezaji wa kilimo cha alizeti lakini hadi leo anahangaika kupata ardhi, ni miaka miwili sasa. Sasa ni kwa namna gani tunaweza kuingia katika uchumi wa kati wakati sekta ya kilimo ambayo inaajiri watu wengi hatuko tayari kuwekeza katika kilimo.