Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE.STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi. Naomba niendelee kumshukuru Mungu kwa ajili ya muda huu, lakini pia niendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais akisaidiwa na Makamu wa Rais pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa jinsi ambavyo anaendelea kuitekeleza Ilani ya Chama chetu cha Mapinduzi. Pia naomba niendelee kumpongeza sana Waziri mwenye dhamana ya Fedha na Mipango pamoja na Naibu Waziri wake na timu nzima ya Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja naomba niongelee huduma kwa wastaafu. Napenda niipongeze Serikali kwa jinsi ambavyo imeboresha mfumo wa malipo ya pensheni kwa wastaafu wetu, lakini pia naungana na maoni ya Kamati kuhusiana na wastaafu ukurasa wa 21.


Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili nina ushauri ufuatao:-
Serikali ni kweli imeongeza kima cha chini kwa pensheni kwa wastaafu wetu na kufikia laki moja. Kima hiki cha chini ukiangalia na uhalisia wa maisha ya sasa hivi ni kidogo sana. Kwa hiyo, naiomba Serikali ama naishauri Serikali kima hiki kiendane na uhalisia wa maisha. Pia Serikali iangalie kwamba mtu anapokuwa mzee na gharama zinaongezeka. Ndiyo katika umri huu ama muda huu ambapo mtu anakuwa na magonjwa anahitaji kujitibia lakini pia anakuwa anahitaji ale hata lishe bora tofauti na mtu wa kawaida unaweza tu ukala ugali na maharage siku imepita lakini kwa Mzee anahitaji kula vizuri na anahitaji huduma za matibabu. Naomba Serikali iliangalie hili iendee kuboresha pensheni kwa hawa wastaafu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee pia msamaha wa kodi kwa wafanyabiashara wenye ulemavu. Ikumbukwe kwamba watu hawa walio wengi ama walio wachache pia wameamua kujitoa kwenye eneo la utegemezi na kuona kwamba wajishughulishe na biashara, aidha, wameona kwamba wasiwe ombaomba. Kwa hiyo naiomba sana Serikali iondoe kodi kwenye biashara za watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba niongelee suala la zima la kodi kwa vyombo vya moto vinavyotumiwa na watu wenye ulemavu yakiwemo magari ama kama ni bajaji. Katika eneo hili naishukuru Serikali kwamba inatoa exemption kwa vyombo vile ambavyo vimefungwa vifaa maalum vinavyoonesha kwamba chombo hiki kinatumika na mtu mwenye ulemavu, ikumbukwe kwamba kuna mtu mwenye ulemavu mwingine ambaye anaendeshwa ama anasaidiwa kwa mfano ukichukulia mtu ambaye haoni, kwa vyovyote vile lazima ataendeshwa na mtu anayeona, sasa ukimfungia kifaa maalum, halafu atakitumiaje hii inakuwa haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali iangalie tu kwamba kama kifaa hiki kinatumika na mtu mwenye ulemavu isiangalie kwamba lazima hiki chombo kiwe kimefungwa kile kifaa maalum kwa mtu mwenye ulemavu. Kwa mfano, mimi naendesha gari mwenyewe lakini gari yangu haina vile vifaa maalum ambavyo vinatumika na watu wenye ulemavu, kwa hiyo sasa nisinyimwe exemption kwa sababu tu ile gari haijafungwa vile vifaa maalum, naomba sana Serikali iondoe kodi kwenye hivi vyombo vinavyotumika na watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee suala la road licence hata mwaka jana wakati nachangia bajeti hii niliongelea hilo pia. Serikali itoe msamaha wa road licence kwa watu wenye ulemavu. Kwa nini nasema hivyo kwa mfano mtu kama mimi natumia gari ambalo kwangu siyo luxury ni hitaji la lazima. Kwa hiyo Serikali inaponitoza kodi ya road licence kwenye gari yangu ina maana kwamba inalipisha ile miguu. Gari pale inasimama badala ya miguu ya mtu mwenye ulemavu ama inasimama badala ya hata macho kwa mtu mwenye ulemavu. Kwa hiyo, road licence iondolewe kwenye magari ama vyombo vinavyotumika na watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho na si kwa umuhimu natoa rai kwa Watanzania wenzangu, kumuunga mkono Rais wetu katika juhudi za ulipaji wa kodi kwa kudai na kutoa risiti pale ambapo mauzo na manunuzi yanapofanyika. Kwa nini nasema hivyo? Nasema hivyo kwa sababu bado kuna wimbi kubwa la udanganyifu kwenye suala zima la kodi. Unaenda dukani ama kwenye kituo cha mafuta unadai risiti, mtu anakwambia mashine ni mbovu, ukipita tena siku nyingine anakwambia mashine ni mbovu. Hawa wafanyabiashara hizi mashine za EFD wanazo ila wanatumia hii ya kusema kwamba mashine ni mbovu kama ni njia ya ukwepaji wa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali iliangalie hili, kuna wafanyabiashara wanakwepa ulipaji wa kodi kwa kudanganya kwamba mashine ni mbovu. Niwaombe sana Watanzania tuwe na uzalendo katika ulipaji wa kodi. Mambo mengi leo tunaona kwamba hayaendi kwa
sababu makusanyo yanakuwa si mazuri na ni madogo kwa sababu sisi wenyewe hatuwajibiki katika suala zima ya ulipaji wa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja.