Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami uniruhusu pia niwashukuru sana wenzangu kwa kunipa pole pale nilipofiwa. Pamoja na hilo nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema na hata leo naendelea kufunga katika kutimiza ibada ambayo anaisimamia yeye mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianzie pale ambapo ameishia mjomba wangu kutoka Morogoro katika jambo la Ofisi ya CAG. Ni kweli yamesemwa mengi juu ya CAG kwamba zile fedha kwa ajili ya ukaguzi zinachelewa na ushauri mzuri umetolewa, lakini nataka nizungumzie sana kwenye hili suala la Internal Auditors.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Internal Auditors hawawezi kufanya kazi bila maelekezo ya Ofisi ya Mkurugenzi, tukumbuke kwamba huyu anaenda kukaguliwa ndio huyo huyo ambaye anatoa hiyo ruksa kwa ajili ya kukagua hizo fedha. Nataka niseme, kama utaratibu huu utaendelea haya anayoyasema Mheshimiwa Mbunge hapa kwamba unakwenda kuomba OC kwa ajili ya kufanya ukaguzi unaambiwa OC hakuna basi ndivyo ambavyo itakuwa inafanyika kila muda ambapo tunataka ukaguzi ufanyike, lakini kwa nini wanafanya hivyo? Maeneo mengi yanafanyika kwa sababu ofisi za Wakurugenzi na Watendaji wengine wamekuwa wabadhirifu na kwamba wanatumia mgongo wa kutokupatikana kwa OC ili kuficha makosa yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachopenda kupendekeza kwa Serikali yangu, sasa Ofisi ya Internal Auditor iondolewe katika Halmashauri zetu, ziwe moja kwa moja zina mahusiano na Ofisi ya CAG Makao Makuu ili kiasi kwamba wanapokwenda kukagua vitabu basi wawe wanakagua kwa mujibu wa taratibu na authority ambayo wanakuwa nayo kutoka kwenye Ofisi Kuu ya CAG, lakini kuendelea kuziacha hizi ndani ya Halmashauri ni kuendelea kutwanga maji ndani ya kinu na hatuwezi kupata unga tunaoutarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo nishukuru sana kazi kubwa inayoendelea kufanywa na Serikali yangu katika kuhakikisha kwamba inaendelea kuweka fedha nyingi katika maeneo ya kilimo. Nimesoma kupitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri juu ya jitihada kubwa zilizofanyika kupitia Benki ya Kilimo na jinsi ambavyo wameweza kuwafikia watu wengi. Pamoja na hilo, ushauri kwa Serikali yangu ni kuendelea kuangalia maeneo ya kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, katika mwaka uliopita tumeshuhudia katika taarifa mbalimbali ikiwemo taarifa ya Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, kwamba katika mazao ambayo yameiletea fedha nyingi nchi yetu ni pamoja na zao la korosho, pia zao la pamba. Kwangu katika kitabu hiki niliposoma hasa katika eneo la jinsi ambavyo Serikali imeenda kusaidia wakulima, katika kuwapa elimu, fedha katika vikundi mbalimbali kwa ajili ya kujiendeleza, maeneo hayo mawili makubwa sijayaona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atueleze juu ya mkakati wake alionao sasa wa kuangalia jinsi gani anawezesha maeneo haya au wakulima hawa waweze kufaidika. Kwa mfano tumeona wenzetu Morogoro hasa katika eneo lile la kilimo cha mpunga kule Kilombero wameweza kufaidika na mambo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia akumbuke tunalo Bonde kubwa sana la Ruvu ambalo lina accommodate chakula ambacho kinauzwa katika eneo kubwa la Dar es Salaam. Hata hivyo, leo hii tulivyo pale, wakulima wale na vikundi vile vya wakulima havina jinsi wanavyoweza kutunisha mifugo yao. Ninachomwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuelezea kwenye eneo la kilimo basi pia aeleze na matumaini mapya ya wakulima hasa wa Bonde la Ruvu na Bonde la Wami jinsi gani wanaweza wakafaidika na fursa hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo nimkumbushe Mheshimiwa Waziri jambo moja zuri. Mwaka 2009 Wananchi wa Kijiji cha Msata, Kata ya Msata, walitoa eneo lao wakawapa Chuo cha Usimamizi wa Fedha – IFM, mambo ya ajabu yakaanzia hapo. Mwaka 2013 baada ya makelele mengi sana Chuo cha Usimamizi wa Fedha wakalipa fedha kwa ajili ya uendelezaji wa eneo lile, lakini toka mwaka 2013 mpaka leo, hakuna jambo lolote lililofanyika katika eneo lile! Mji wa Msata umeendelea kukua na wananchi ambao walikuwa wamejipanga kwa ajili ya kufanya maendeleo wakipata support na chuo kile, wakaanza kukata tamaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachokiona kama Mbunge wao ndani ya Kitabu cha Hotuba ni maneno ya kwamba, sasa ndio mnajipanga katika mpango mkakati wa kuanza kuchora ramani ya eneo lile. Mheshimiwa Waziri binafsi nikwambie kuchoshwa kwa wananchi wangu kusubiri hicho, lakini pia kuchoshwa kwa Chama cha Mapinduzi kwa ahadi ambazo zinaonekana kwamba, hazitekelezeki. Ninachomwomba Mheshimiwa Waziri kabla wananachi wale wa Msata hawajakikataa Chama chake kilichompa nafasi yeye kuwa Waziri wa Fedha, hebu aje na majibu mazuri ya kimkakati juu ya jinsi gani amejiandaa kuweka fedha kujenga majengo yale na maendeleo ya wananchi kuendelea kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, lakini sio mwisho kwa umuhimu Mheshimiwa Waziri, ni ushauri juu ya mwenendo wa fedha katika Serikali yangu. Mheshimiwa Waziri tumeona katika lugha zinazosemwa kwa yeye na Serikali yangu, mara nyingi lugha inapozungumzwa ya maendeleo ni lugha ya kodi. Wameeleza wengi waliotangulia kwamba, watu sasa wamefikia sehemu wanafunga biashara wanapowaona Maafisa wa TRA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo mimi kwa usomi wangu mdogo natambua kwamba, ziko means nyingi sana za kuweza kujipatia fedha, mojawapo kuna vitu vinaitwa Municipal Bond, kuna vitu vinaitwa Infrastructure Bond, leo hii tunahangaikaje kuwaminya Watanzania maskini na wanaendelea kuumia wakati tunazo njia ambazo yeye kama msomi wa mipango anazijua vizuri na anaweza kuzisimamia vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano hatuoni sababu kwa nini miradi mikubwa kwa mfano kama hii ya Bwawa la Kidunda ambayo nategemea kwamba, ndio litatuletea maji na nguvu ya umeme katika maeneo yetu ya Dar-es-Salaam, Mkoa wa Pwani na maeneo mengine ya Tanzania, tunaendelea kukusanya hela kupitia nguvu za wanyonge wakati tunaweza kutengeneza taratibu ambazo zinaweza zikatusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo nimkumbushe Mheshimiwa Waziri, katika maeneo mengi panapotokea matatizo ya kiuchumi Benki za Kimaendeleo zimekuwa ndio kimbilio. Tumeshuhudia wakifanya hivyo Wajerumani, tumeshudia wakifanya hivyo Wajapani, lakini tumeshuhudia pia nchi mbalimbali ikiwemo Marekani jinsi ambavyo wameweza kupitia vyanzo mbalimbali na kuweza kukusanya pesa na kuweza kusaidia miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo njia ambayo kiuchumi au kifedha wanaita reveragies, ambazo benki inaweza ika-raise hela mara tano ya kile kiwango ambacho kinatakiwa ili kusaidia kunyanyua kiwango cha pesa kuweza ku-finance miradi mikubwa. Mheshimiwa Waziri ni kwa nini mpaka leo hii Wizara yake imeendelea kumshauri Rais wangu, imeendelea kuwaumiza Watanzania kupitia mianya ya kodi wakati tunazo njia kupitia reveragies ambazo zinaweza zikawasaidia kupata hela nyingi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atakaposimama atuambie Watanzania, amejipangaje kuweza kusaidia kunyanyua fedha kwa ajili ya kusaidia miradi mikubwa ya Serikali, lakini pia kupunguza huu ugumu na machungu kwa wananchi wetu. Maana tunatambua tunayo Benki kama TIB, tunayo Benki kama TADB, hizi zote kama zitawezeshwa kupitia fursa hizi za ku-raise hela ambazo zinaweza zikasadia kupunguza makali kwa wananchi wetu nina hakika kabisa yale malengo mazuri tuliyoahidi katika ilani tutaweza kuyafanikisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo Mheshimiwa Waziri nimpongeze tena yeye anavyoendelea kukamilisha na kusimamia shughuli mbalimbali za Wizara, malalamiko mengi ya wananchi yamekuwa katika kuangalia kwamba, huku Serikalini wanajidai, wanatamba kwamba, uchumi unaendelea vizuri wakati maendeleo katika mifuko ya wananchi yameendelea kuwa mabaya zaidi. Mheshimiwa Waziri namwomba sana tafsiri ya maendeleo, tafsiri ya uchumi, tafsiri ya maisha yaliyo bora kwa Watanzania ni maendeleo yanayofanana na hali halisi ya maisha wanayoishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niunge mkono sana mipango hii, lakini namwomba Mheshimiwa Waziri atambue kwamba, huko mtaani maisha ya wananchi ni magumu na malalamiko ni mengi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.