Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya Fedha. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu aliyenipa afya na uzima tumekutana siku ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa mchango wangu nitajielekeza kwenye milioni 50 za kila kijiji. Mheshimiwa Waziri wa Fedha mwaka jana wakati alipokuja hapa alikuja na mpango mzuri na Bunge lako hili lilitenga zaidi ya shilingi milioni 59 kwa ajili ya kutekeleza azma hii ya kupeleka milioni 50 kila kijiji. Hata hivyo, mpaka muda huu tunaongea kutokana na ripoti ya Kamati na hali halisi hata kule kwenye vijiji vyangu, hakuna kijiji chochote ambacho kimeshapata milioni 50. Moja ya changamoto kubwa ambayo tunakutana nayo sasa hivi tukienda kwenye Majimbo swali la kwanza utaulizwa milioni 50 zitakuja lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shida kubwa sana kule vijijini kwa sababu, niwapongeze sana UWT upande wa akinamama walifanya kazi kubwa sana pamoja na Wabunge kuhamasisha vikundi vingi sana vimeanzishwa kwa matarajio kwamba kuna milioni 50 zitakuja, kwa sababu tuliwaambia kwamba tutapitishia kwenye vikundi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali wakati inakuja kufunga mjadala huu ni vizuri ikaja na kauli thabiti ya Serikali kwamba hizi fedha zitatoka au zimebadlishwa mpango mwingine ili tuwe na jibu la Serikali na Wabunge kuwapelekea wananchi wote tuwe na msimamo mmoja badala ya sasa hivi wananchi hawatuelewi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nikikumbuka ile bajeti ya mwaka jana Mheshimiwa Waziri alisema tumetenga milioni 59, mwaka huu tungepeleka labda milioni 50, mwakani 50 mpaka miaka mitano vijiji vyote tungevimaliza. Sasa mwaka jana hatukupeleka hata senti tano, lakini bajeti ya mwaka huu inakuja na milioni 60. Nilitegemea kwa sababu hatukupeleka mwaka jana bajeti ya mwaka huu ingekuja na mia au zaidi ya mia ili twende na mipango ambayo Serikali ilipanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nijielekeze kwenye mapato. Tatizo kubwa la nchi yetu hasa nchi hizi za dunia tatu ikiwemo na Tanzania tuna mahitaji makubwa sana lakini mapato yetu ni madogo. Katika hili niipongeze sana Serikali ya Awamu ya Tano, watu wengi walikuwa wanalaumu kwa nini tumepokea mpaka sasa asilimia 34 ya fedha za miradi ya maendeleo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza kwa sababu kabla haijaingia madarakani Serikali ya Awamu ya Tano zaidi ya miaka miwili, Serikali Kuu ilishindwa kupeleka hela za maendeleo katika Halmashauri zetu. Sasa leo tumepata asilimia 34, kutoka sifuri unapata asilimia 34 ni suala la kupongeza sio kubeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kusema katika hili ni ukweli usiopingika, hali ya biashara sasa hivi nchini siyo nzuri, biashara nyingi zinafungwa. Maana ya biashara kufungwa ni kwamba ajira za Watanzania zinapotea, mapato ya mtu mmoja mmoja na wafanyabiashara yanapotea, mapato ya Serikali yanapungua. Huko mbele tusipochukua tahadhari ya kuongeza tax base ya walipa kodi nchi hii inawezekana walipa kodi watapungua na mapato ya Serikali yatapungua sana. Baadaye hata haya tuliyofikia sasa yatakuwa yanapungua, kwa sababu athari nyingine itakuja, tutawakandamiza wale wachache walipa kodi, tuwaongezee viwango badala ya kuisambaza hii kodi kwa watu wengi zaidi ili waweze kulipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika hili, nimeona katika ukurasa wa 77 wa kitabu cha Mheshimiwa Waziri amesema kwamba, miongoni mwa mikakati yao ni pamoja na kurasimisha biashara nyingi zisizokuwa katika mfumo rasmi kuja kwenye mfumo rasmi wa kodi. Leo hii tuna tatizo katika nchi yetu, Mtanzania mfanyabiashara akisikia biashara yake imetembelewa na Polisi au imetembelewa na TRA anapumua zaidi ikitembelewa na Polisi kuliko TRA. Anajua leo sijui kuna shida gani? Au leo umaskini sasa umeshaingia kwenye biashara yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika hili, niombe kama kweli tunataka kuwarasimisha na kupanua tax base katika hili, tupate walipa kodi wengi katika nyanja hizi, basi Serikali inapaswa itoe elimu ya kutosha kwa walipa kodi na Watanzania kwa ujumla, umuhimu wa kulipa kodi, manufaa kwa nchi na kwenye hii biashara yenyewe, watu waelewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kutoa incentive maalum kwa wajasiriamali wa ndani. Kuwaambia mtu yeyote yuko huru kurasimisha biashara yake kuingia kwenye mfumo wa kodi, tutaanza kudai kodi hapo alipoanza kurasimisha kwenda mbele. Tatizo sasa hivi zinafungwa biashara nyingi, sio kwamba hawapati faida, wakati mwingine mtu anaona anakuwa salama zaidi kufunga biashara aachane na Serikali kuliko aje ajitangaze kurasimisha anapewa madeni kuanzia miaka ilipoanza hiyo biashara, akija kuangalia uwezo wa kulipa hana, matokeo yake biashara inakuwa hohehahe na anafilisiwa kabisa. Sasa kwa nini mtu aje ajirasimishe kwa nini asifunge tu aachane nayo atafungua biashara nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali kama kweli tuna dhamira ya kuwasaidia wajasiriamali na kweli tuna dhamira ya Watanzania walipe kodi bila kushurutishwa basi ni vizuri tutoe incentive. Tuseme miezi sita au mwaka mtu yeyote tutaanzia kulipa kodi pale unapoanza kurasimisha biashara yako kwenda mbele. Nilishawahi kusema humu ndani tuchukue mfumo kama wa Wizara ya Ardhi inavyofanya, leo nikipima ardhi yangu mimi naanza kulipa leo, huwezi kusema kwamba miaka yote unatumia ardhi hii lazima ulipe, hakuna mtu atakuwa na huo uwezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kwenye matumizi. Ni kweli mwenzangu mmoja alizungumza huku, sisi tuna tatizo kubwa sana la mapato ni madogo lakini hata hayo mapato yenyewe madogo, Serikali inajibana, TRA wanajibana yakifika kwenye Halmashauri zetu au taasisi zetu hayatumiki kwa makusudio ya Serikali iliyopanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa mfano kwenye Halmashauri yangu ya Morogoro, kuna miradi kwa mfano miradi ya maji pale Kiroka na Tuluwakongo, hela zimekuja tangu 2015 milioni 700 mpaka zimeanza kutumika leo kwa mbinde kwelikweli, kwa sababu zile pesa zinatakiwa Mkandarasi zisimamiwe kule vijijini, sasa watu wa halmashauri hawana maslahi binafsi ya asilimia 10, kwa hiyo hawaoni umuhimu wowote wa kusaidia hilo jambo liende. Wako radhi wananchi wakose hiyo huduma kwa vile tu wao hawana maslahi binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni vizuri Serikali mkaweka mifumo sahihi ya ufuatiliaji ili mjue fedha mlizozipeleka kule zinatumika? Kwa sababu sisi Madiwani tunadanyanywa sana na hawa wataalam na wao wanasema kila kitu tuwaachie wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapeni mfano mwingine. Kwenye hiyo hiyo Halmashauri juzi tu tumetoka kwenye Kamati ya Fedha, walileta pale pesa walizoleta zaidi ya milioni 360 kwa ajili ya miradi ya maendeleo lakini wakatuletea sisi shilingi milioni 170 wakasema zingine hamna, na bank statement wanakuletea kabisa unaambiwa haipo. Baada ya kubanana sana zikaja ikaletwa tena, tulizisahau milioni 190. Sasa mambo kama haya wakati mwingine kama mnavyofahamu wasimamizi wakubwa ni madiwani, lakini madiwani wenyewe hawa hawana mishahara. Sasa akirubuniwa kidogo ni rahisi sana kupitisha kwa sababu anajiangalia yeye na maslahi binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ushauri wangu ni kwamba, kwa sababu Madiwani ndio wasimamizi wakubwa wa Serikali kule chini wa pesa za wananchi, ni vizuri Serikali ikaangalia namna gani ya kuwalipa mishahara Madiwani ili waweze kusimamia pesa za umma zitumike kama zilivyopangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao Wakaguzi wa Ndani kule kwenye Halmashauri, kila akitaka kwenda kukagua miradi anaambiwa hatuna pesa Serikali haijagawa OC. Hizo pesa wakati mapato ya ndani yapo! Morogoro DC tumekusanya zaidi ya bilioni 1.6, haijawahi kufikiwa tangu uhuru ianze, tulikuwa tunaishia milioni 500, 600, lakini leo Mkaguzi wa Ndani anaaambiwa kwamba hakuna OC huwezi kwenda kukagua ile miradi, kwa sababu wanaficha mambo yao waliyoyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.