Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2017/2018

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2017/2018

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi, ili na mimi niweze kuchangia Wizara ya Nishati na Madini. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa uwasilishaji mzuri wa bajeti ya Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi ambavyo amechukua hatua za makusudi kuweza kutetea na kuangalia changamoto mbalimbali zinazogusa wachimbaji wadogo wa madini Tanzania. Mwanzoni kulikuwa na unyanyasaji mkubwa sana wa wachimbaji wa madini, lakini tumemwona Mheshimiwa Rais akiwa Ikulu akiona wachimbaji wakinyanyaswa anatoa maagizo na maelekezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitumie fursa hii kwa niaba ya Wachimbaji wadogo wa Tanzania kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kuhusiana na suala la ile Tume iliyochunguza mchanga unaosafirishwa nje ya nchi. Mimi binafsi natoka sehemu ambako madini yako kwa wingi ya dhahabu. Kweli, nitumie fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais na kumpongeza kwa hatua aliyochukua, kwa kweli, imetupa moyo sisi pamoja na wananchi kwani ilikuwa ni kero kubwa sana, hasa kwa sisi ambao tunatokea maeneo haya ya wawekezaji wakubwa wa dhahabu. Wananchi walikuwa kila wakati wakiuliza, inakuwaje mchanga unasafirishwa, walisema sisi hatuoni hata faida yoyote ya kuwa karibu na wawekezaji hawa wakubwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa hatua ambayo Mheshimiwa Rais ameichukua mimi binafsi nimefarijika na wananchi wamefurahi sana; na tunamwambia Mheshimiwa Rais aendelee na kasi hii na mikataba iangaliwe upya ili kuona jinsi ambavyo wananchi tunaweza kunufaika zaidi kutokana na madini ambayo Mwenyezi Mungu ametupatia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizo, binafsi napenda kuzungumzia kwenye madini. Jimbo la Busanda ni jimbo ambalo limebarikiwa na Mwenyezi Mungu, siku zote huwa nasimama hapa nasema tunayo madini ya kutosha. Nilipokuwa nikiangalia bajeti ya Mheshimiwa Waziri sijaona chochote kuhusiana na Jimbo la Busanda kwa kweli, japokuwa ndiko ambako madini mengi yanatokea, hasa wachimbaji wadogo wako wengi sana kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda Mheshimiwa Waziri atakapo-wind up aniambie maeneo ya Nyarugusu, hajazungumzia maeneo ya Rwamgasa, pamoja na Mgusu na sehemu mbalimbali za wachimbaji. Naomba azungumzie atakapo-wind up kwa sababu kwenye bajeti sijaona chochote kuhusiana na maeneo hayo niliyoyataja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo kuna eneo la STAMICO ambalo limekuwa ni kilio cha muda mrefu sana kwa wananchi wa Nyarugusu na Mheshimiwa Waziri mwaka uliopita alisema kwenye bajeti kwamba analishughulikia na ataweza kulitafutia ufumbuzi suala hili, lakini mpaka sasa hata kwenye bajeti sijona akizungumzia hata kidogo. Kwa hiyo, naomba atakapo-wind up aniambie na wananchi waweze kusikia kwa sababu wanasikiliza na hata hivyo wako kwenye TV wanaangalia ili kuona kwamba, je, suala hili limeweza kushughulikiwa? Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri aliangalie suala hili na aweze kulifuatilia.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo pale Rwamgasa mwaka 2015, paliteuliwa kuwa sehemu maalum kwa ajili ya uanzishwaji wa eneo la uchenjuaji wa dhahabu wa mfano. Hata hivyo nimesikitika kwamba kwenye Kitabu cha Bajeti, ukurasa wa 103, kati ya vituo saba vya mfano vya kuchenjua dhahabu Rwamgasa haijatajwa tena; sasa napenda kuuliza, je, imeondolewa kwenye huo utaratibu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2015, Benki ya Dunia ilikuja kuzindua rasmi mradi huo pale Rwamgasa na hata leo hakuna chochote kinachoendelea na wananchi wanaendelea kuulizia juu ya suala hili. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atueleze, wawaeleze wananchi wa Rwamgasa kuhusiana na suala hili, kwa sababu Serikali ni kwa muda mrefu imeteua Rwamgasa kuwa Kituo Maalum kwa ajili ya uchenjuaji wa dhahabu lakini leo hii Rwamgasa haipo kwenye bajeti kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile maeneo ya Buckreef ni maeneo ambapo Serikali pamoja na TANZAM wamefanya uwekezaji, lakini sisi wananchi hatuoni faida yoyote kutokana na huo mgodi. Kwa nini Serikali isiangalie upya mkataba huo ili ikiwezekana wapewe wananchi maeneo hayo waweze kuchimba na kunufaika na rasilimali za Taifa zilizopo katika nchi ya Tanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile TANZAM wamechukua eneo Rwamgasa, wakulima wamenyang’anywa maeneo na mpaka sasa hawajapewa fidia yoyote. Naomba Mheshimiwa Waziri aniambie, kwa sababu maeneo hayo wananchi hawaruhusiwi kulima wala kufanya kazi yoyote pale, lakini hawajapewa fidia yoyote. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri wazungumzie suala hili, ili wananchi waweze kujua hatma yao kuhusiana na suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi binafsi napenda kuishauri Serikali kwamba Mkataba huu wa Buckreef na TANZAM uangaliwe upya na ikiwezekana eneo hili wapewe wananchi ili waendelee kuchimba dhahabu na kuweka mchango wao kwenye pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kwa upande wa umeme; nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali japokuwa tunaona Serikali inaendelea kupeleka umeme hasa katika Miji mbalimbali. Kwa mfano Katoro mpaka sasa hivi wanasambaza kwa kasi umeme, lakini bado jitihada zinahitajika zaidi kwa sababu wananchi wanahitaji umeme. Kati ya Kata zangu 22 ni kata 10 tu ndizo zilizofikiwa. Kwa hiyo, niombe Serikali iwekeze nguvu zaidi, ikiwezekana REA iongezewe fedha zaidi ili wananchi hasa walio wengi walioko vijijini waendelee kupata umeme wa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo niangalie kwa habari ya mafuta. Kuna vinasaba ambavyo vimekuwa vikilipiwa dola 14 kwa lita 1,000. Hivi vinasaba kwa nchi ya Tanzania kwa kweli, vinaongeza gharama ya mafuta. Naiomba Serikali iondoe hii gharama, ifute kabisa vinasaba hivi kwa sababu sasa hivi bei ya mafuta ya dizeli na bei ya mafuta ya petroli na mafuta ya taa karibu zinalingana, kwa hiyo uchakachuaji haupo tena umepungua kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba kwa kuwa, katika nchi nyingine za Afrika Mashariki kama Kenya vinasaba hivi gharama yake ni dola tatu mpaka nne, lakini sisi ni dola 14, kwa nini inakuwa hivyo sisi katika nchi ya Tanzania? Ndio maana sasa mafuta yanakuwa na bei ya juu zaidi kuliko nchi nyingine wakati sisi tuna bandari hapa hapa Tanzania. Kwa nini bei ya mafuta iwe juu ukilinganisha na nchi nyingine wakati sisi tumebarikiwa pia kuwa na bandari katika nchi ya Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo sasa nichukue nafasi hii kuiomba sasa Serikali iangalie kiundani habari ya wachimbaji wadogo wadogo ambao nimewazungumzia kwa miaka mingi, iangalie namna ya kutatua changamoto zao sasa, kwa sababu imekuwa ni kipindi kirefu wananchi wanahangaika, wanalia, wanahitaji kupewa maeneo ya uchimbaji. Hatuwezi kufikia uchumi wa kati bila ya kuwawezesha hawa wachimbaji wadogo wa madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo wakati ule ambapo Mheshimiwa Profesa Muhongo alikuwa Waziri alikuja Geita akatoa maelekezo kwamba ziangaliwe zile leseni ambazo hazifanyi kazi waweze kupewa wananchi. Mkoa wa Geita tu tuna zaidi ya leseni 1,700 ambazo ni za utafiti pamoja na wachimbaji wadogo wadogo na wa kati. Hata hivyo, kati ya leseni hizo zinazofanya kazi ni leseni 30 tu, kwa hiyo leseni nyingi hazifanyi kazi. Nitumie fursa hii kuiomba Wizara iangalie namna ya kuwapatia wananchi leseni hizi ambazo hazifanyi kazi, hasa vikundi vya wachimbaji wadogo ambao wanafanya shughuli mbalimbali za uchimbaji. Kwa hiyo...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana.