Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia mawazo ya Wanaigalula katika bajeti hii ambayo ni nzuri, ambayo Wanaigalula wanaiunga mkono kwa sababu kwa asilimia kubwa inatatua matatizo na mambo ambayo wanadhani ni shida kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri ambayo wameifanya katika bajeti ya mwaka huu. Yako mambo ambayo tuliyashauri mwaka jana tulidhani hayajafanyiwa kazi kumbe walikuwa wanajipa muda wa kutafakari na sasa wameyaweka na kuyafanyia kazi katika bajeti ya mwaka huu. Mimi nataka niungane na wale wote wanaoipongeza bajeti hii kwa sababu yale yote yaliyozungumzwa katika bajeti ya mwaka huu mengi tuliyashauri katika bajeti ya mwaka jana na mengi tumekuwa tukiyashauri siku hadi siku. Nina hakika kwa asilimia kubwa yamefanyiwa kazi na yamewekwa katika bajeti ya mwaka huu. Natoa pongezi kubwa sana kwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri mnayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mwizi wa fadhila nisipompongeza Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ambaye ni Rais msikivu. Wamekaa pamoja na Waziri wa Fedha wamekubaliana na wametuletea bajeti ambayo nina uhakika kama itatekelezwa vizuri itakwenda kutatua kero na changamoto nyingi tulizonazo katika majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti hii ni nzuri lakini yapo mambo ambayo tunaendelea kuishauri Serikali yetu iyafanyie kazi ili kuendelea kuiboresha zaidi bajeti yetu iwe nzuri zaidi. Kwanza kabisa nianze kuzungumzia reli. Naipongeza Serikali kwa uamuzi wa kujenga standard gauge, reli ambayo itatusaidia sisi wana-Igalula na mikoa mingine katika usafiri na usafirishaji wa mazao yetu. Tulikuwa tunasafirisha tumbaku
yetu kwa malori kwa gharama kubwa, sasa nina uhakika standard gauge ikikamilika usafiri wa tumbaku yetu toka Tabora kuja sokoni utakuwa ni wa rahisi na kutusaidia kuongeza faida katika zao letu la tumbaku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maendeleo yoyote changamoto lazima ziwepo. Wakati tunaanza kujenga standard gauge, kuna wananchi maeneo mengi wanalalamika wanaanza kuvunjiwa nyumba zao bila utaratibu. Niombe Wizara husika ikakae na wananchi wetu katika maeneo itakapopita reli hii ambapo wananchi wote wanakubali ujenzi wake ili waelimishwe wafanye uhakiki mzuri ili wale wanaostahili kuvunjiwa maeneo wavunjiwe wakiwa wanajua taratibu zimekamilika na ziko sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kuhusu barabara. Naomba niipongeze Serikali baada ya kusikia kilio chetu sisi wana-Igalula cha barabara ya Chaya - Nyahua, tumepata shilingi bilioni 110 kutoka Kuwait Fund itakayoenda kujenga barabara ile. Barabara hii kwa asilimia 100 inapita katika Jimbo la Igalula lakini inaunganisha Mikoa ya Tabora na Singida, Tabora na Kigoma na Tabora na Katavi, barabara hii ni muhimu sana. Unapozungumzia kipande hiki cha barabara cha kilometa 89 kitasaidia sana usafiri na usafirishaji katika maeneo ya mikoa hii niliyoitaja lakini sisi wana-Igalula tutanufaika kwa asilimia kubwa kwa sababu asilimia 100 barabara hii inapita katika Jimbo la Igalula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukipata kikubwa na kidogo pia unaomba, tuna barabara tuliomba ipandishwe hadhi ya kutoka Buhekela - Miswaki - Loya ambapo tuna kilimo kikubwa cha mpunga. Tunaposema wananchi wetu wawe wakulima wazuri, tusipowatengenezea miundombinu iliyo bora ya kufanya wapate faida ya mazao yao tunakuwa hatujawasaidia. Barabara hii haipitiki kipindi kikubwa kwa sababu ni mbovu. Tuliomba ipandishwe hadhi ili wananchi wa kule wanaolima mpunga waweze kupata faida kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la maji. Sisi Mkoa wa Tabora tunaipongeza tena Serikali kwa uamuzi wake wa kuyatoa maji toka Ziwa Victoria kuyaleta katika Mkoa wetu wa Tabora. Najua kuna baadhi ya maeneo mradi huu wa Ziwa Victoria hautafika ikiwemo Urambo, Kaliua, Ulyankulu na sisi Igalula. Najua ipo mipango inafanyika kupata maji ya uhakika katika maeneo haya lakini kipindi hiki ambacho tunasubiri mipango hiyo, tunaomba taratibu za kupata maji ikiwemo kuchimbiwa visima virefu, mabwawa ili tuweze kupata maji ya uhakika katika baadhi ya maeneo yetu ifanyike. Sisi Igalula tuliahidiwa kujengewa bwawa kubwa katika Kata ya Goweko na Loya lakini mwaka wa fedha uliopita havikutekelezeka. Naomba katika mwaka huu wa fedha tuweze kusaidiwa kupata maji katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na mawazo ya Mheshimiwa Ndassa aliyesema zile shilingi 40 ziongezwe na shilingi 50 ya mwaka jana ziwe shilingi 90 zikatatue kero ya maji katika maeneo yetu. Bajeti kubwa ya mwaka jana ya Wizara ya Maji ya kutekeleza miradi mingi ya maendeleo ilitokana na shilingi 50 tuliyoipitisha sisi hapa ndani. Kama ikiongezwa shilingi 40 ile, nina uhakika miradi mingi ya maji katika maeneo yetu itakwenda kutekelezeka. Wale wanaopinga kuongezeka shilingi 40 nadhani hawawatakii mema wananchi wetu wanaopata taabu ya maji katika maeneo yetu mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda nizungumzie kidogo suala la kilimo cha tumbaku, tunashukuru juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali yetu katika kutatua kero za tumbaku katika maeneo yetu. Unapozungumzia tumbaku ni uchumi wa wananchi wetu wa Igalula na Mkoa wa Tabora. Unapozungumzia tumbaku, ni uchumi wa nchi kwa sababu nchi inapata kodi kubwa katika zao la tumbaku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo yanatakiwa yaendelee kufanyiwa kazi ikiwemo soko la tumbaku na tuondolewe grades mbalimbali katika zao la tumbaku ili iweze kupata bei nzuri, lakini kikubwa Serikali sasa ifikirie kujenga kiwanda cha tumbaku katika Mkoa wa Tabora linapozalishwa zao hili la tumbaku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hotuba ni nzuri, naomba na mimi niungane na wale wote wanaosema bajeti hii ni nzuri. Tunachoshauri sasa yakatekelezwe yale yote ambayo yameahidiwa katika bajeti hii ikiwemo na mawazo sasa ya Waheshimiwa Wabunge ambayo wanaongezea katika kuiboresha zaidi bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naunga mkono hoja, ahsante sana.