Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii adhimu ili nami nitoe mchango wangu. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais jinsi anavyokwenda, nasema mwenye macho haambiwi tazama, tunasonga mbele. Pili naipongeza Wizara ya Fedha kwa hotuba yake ya Bajeti Kuu ni bajeti nzuri ya kiwango. Nichangie kidogo tu kwa maana ya kufanya marekebisho madogo, lakini bajeti ni nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza bado Tanzania tunahitaji maji na hasa vijijini. Maeneo makubwa na mengi suala la maji ni shida kubwa. Niungane na ushauri wa Kamati ya Bajeti, moja ya vipengele ambavyo walikuwa wameshauri ni kwamba ile Sh.40/= tuongezee Sh.10/= ifike Sh.50/= ikaungane na ile tuipeleke kule kwenye Mfuko wa Maji. Tafadhali sana naomba ifanyike hivyo, vinginevyo hali ya maji bado ni tatizo kubwa sana hata katika uwekezaji huu bado itakuwa ni shida na hasa kule vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili lake la maji hilo hilo naomba sana Wizara inayohusika na maji igawe rasilimali maji kwa usawa. Kuna maeneo hasa ya vijijini asilimia zile, nimejaribu kuangalia bajeti ya maji ukurasa wa saba walipozungumzia kwamba asilimia 72.58 vijijini wanapata huduma ya maji ndani ya mita 400, inawezekana ni sawa, lakini baadhi ya maeneo, baadhi ya vijiji si sawa, Jimbo ninalotoka mimi la Manyoni Mashariki ni asilimia 18 tu, ndiyo wanaopata huduma ya maji vijijini. Ndio maana nimesema tugawe hizi rasilimali maji.

Mheshimiwa Spika, hii fedha iende sawa kama kuna maeneo yako chini, tuwanyanyue na wenyewe, wale ambao wamefikiwa hiyo asilimia 72 basi sawa, lakini hawa ambao wako chini, wanyanyueni na wenyewe twende kwa pamoja, nataka nilisisitize hilo kwa sababu Manyoni kule hali ni mbaya na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa pili bado nalalamika kwamba miji na vijiji naomba tuvipange kwa maana ya kupanga na kupima, bado hali ni mbaya,

kupanga miji na vijiji kwanza ukusanyaji wa mapato unakuwa rahisi sana, tunaimba property tax, tunaimba land rent, haitakuwa na ubishi inapokuwa tumepanga miji yetu, lakini pia huduma zingine zote. Unapokuwa umepanga mji wako au vijiji vyako huduma zote zinakwenda vizuri na ndio ustaarabu wa kibinadamu hatuwezi kukaa kama nyanya tumerundikana hivi, haiwezekani tupange miji yetu.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Ardhi mimi nasema imeelemewa isaidiwe. Kusaidiwa kwake, tuwape Halmashauri nguvu za kupima vijiji na miji na unapowapa Halmashauri kazi hii maana yake ni kwamba uwawezeshe ile retention ya fedha, makusanyo ya kodi za viwanja zile ile asilimia 30 bado naihitaji ibaki kwenye Halmashauri tuwasaidie Wizara ya Ardhi kupima, wenyewe hawataweza. Kwa mfano, mwaka jana wamefanya kazi kwa asilimia 30 tu ile fedha imetoka asilimia 30 tu. Hawawezi kupanga na kupima miji wao wenyewe, haiwezekani.

Mheshimiwa Spika, wamepeleka wataalam kule kuna Valuer kule kuna Surveyor kule, kuna Maafisa Mipango Miji kule Halmashauri, sasa kwa nini tusiwaachie hii asilimia 30 wapime huko wawasaidie. Wao wabaki tu ku–control? Kwa nini wang’ang’anie kukumbatia hii kazi na hawawezi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu, naomba ufafanuzi kutoka kwa Waziri wa Fedha, ufafanuzi kwenye ukurasa 48 viwango vya kodi za majengo. Hapo kuna utata kidogo. Mimi ni mtaalam, unaposema flat rate kwa maeneo ambayo hayajafanyiwa valuation, sawa sikatai flat rate lakini flat rate ifanane fanane basi. Unaposema Sh.10,000/= kwa majengo ambayo yako chini, hujaweka pia categories ni ya aina gani, kuna watu wamejenga (massions) majumba makubwa lakini yapo chini, ukiangalia jumba kubwa zuri, hamjatenganisha ni biashara au ni ya makazi hii Sh.10,000/=, utakuta kuna gest houses sio za ghorofa lakini ni kubwa zina vyumba karibu 20 – 30 na wenyewe walipe hiyo property tax 10,000? Naomba waifafanue vizuri watumie wataalam wapo, tupo wataalam.

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo machache, niongezee kwenye hiyo property tax. Property tax pia ninavyojua mtalaam inalipwa mijini sheria ile ipo, waitazame ile sheria. Sheria hii tunaiita Local Authority (Rating) Act, 1983 inasema ni mijini. Sasa mnaposema property tax iende mpaka vijijini sijaelewa na imetoa category ya nyumba sio ya tembe iwe nyumba ambayo angalau ya bati kwa mijini, sasa sijaelewa kama property tax tunaenda kuwatoza mpaka vijijini kule kwenye vijumba vya Wagogo vile vya tembe, sijafahamu.

Mheshimiwa Spika, naomba ufafanuzi na watumie wataalam zaidi pia, kwenye flat rate hiyo lakini na kwenye category ya majengo. Hata ghorofa nayo ina category zake, unakuta ghorofa ina vyumba vingi sana, kuna flat za kuishi kuna maghorofa ya biashara sasa ghorofa ipi ambayo itaingia kwenye flat rate kwamba ilipe 50,000; tutapoteza mapato mengi hapa lakini pia tutawaonea watu wengi hapa, naomba waifafanue sana watumie wataalam.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo machache, naunga mkono hoja na naendelea kumpongeza Mheshimiwa Rais, asimame na msimamo ule ule, nchi hii sasa twende mbele.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.