Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Flatei Gregory Massay

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema ya leo kuchangia katika bajeti hii ambayo kimsingi nadhani itakuwa ya kihistoria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo mambo machache ya kuishauri Serikali katika bajeti hii. Yako mambo ambayo kimsingi nimeyasoma katika bajeti hii ya Mheshimiwa Waziri ambayo kwa kweli naona tu nielezee kidogo. Masuala haya ya mipango mkakati, katika miradi ya mkakati ambayo Mheshimiwa Mpango umeeleza kwenye mipango yako, nikuombe basi kwa kuwa umeeleza miradi hii ya kiuchumi ya vipaumbele
...

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa Mchuchuma ambao umeonekana kipaumbele katika bajeti yako, mradi wa mitambo ya kusindika gesi, Mradi wa Biashara ya Kurasini, mradi wa uwekezaji wa Bagamoyo, mradi wa Mtwara, miradi hii ambayo inaonekana kwenye mpango wako kwa kuwa umeweka miradi hii kama eneo la mkakati wa kuinua uchumi wa Serikali na nchi yetu basi maeneo haya nishauri tu, miradi hii sasa ifike mahali kwa pesa nilizoziona zimetengwa humu. Kwa mfano Mradi wa Biashara ya Kurasini iko bilioni 109 ambayo imeshalipwa fidia pale, pesa zimekaa pale. Niombe kutokana na mkakati huu Serikali ipange namna gani nzuri ya kuendelea na mipango hii ili walau Tanzania ikaweza kuendelea kutokana na mipango hii ambayo tumejiwekea yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kushauri katika eneo hili la maeneo hasa ya maji vijijini. Maji vijijini ukiangalia kwenye bajeti iliyopita fedha za maji vijijini imeenda kwa asilimia 19. Niombe kwa kuwa umeonesha kwenye mpango wako huu kiwango hiki cha maji basi iende kadiri ilivyopangwa katika bajeti ya mwaka huu wa fedha. Pia angalia maji vijijini tunahitaji sana kwa sababu tozo ya maji haipo sasa na Wabunge tunapendekeza tozo hii iweze kuingia humu, Serikali ikubali basi ushauri huu ili walau maji yaweze kwenda vijijini. Hakuna eneo lolote unaweza kumwambia mtu katika eneo la vijijini hatuna maji kwahiyo tuangalie katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni habari ya REA. REA imeonekana kuchukua kasi yake na wananchi wanaifurahia, lakini nikuombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, pamoja na Waziri wa Nishati naamini Kalemani umefika kwenye eneo langu. Mbulu Vijijini tunahitaji umeme wa REA, hakuna viwanda bila umeme. Kwa hiyo nikuombe katika bajeti hii utuone vizuri sana sisi wananchi wa Mbulu Vijijini. Pia barabara hatuna, nimeamua kusema harakahara haya ili yaeleweke. Sisi kule barabara hatuna na umepita kule. (Makofi)

Mheshimiwa Kalemani ulifika Mbulu, ukaiona barabara ile, ulisema kabisa kwa maneno yako nanukuu; “mngeniambia barabra hii iko mbaya namna hii ningetafuta barabara nyingine” haya ni maneno yako Mheshimiwa Waziri. Sasa nikuombe kitu kimoja kwa ajili hii basi miradi hii tunayoiomba pesa ziende. Mheshimiwa Mpango anafahamu nimeleta maombo yangu kwake kuhusiana na msamaha wa kodi ya VAT katika grand ambayo tumepewa.

Narudia tusaidie basi katika mabadiliko ya sheria ambayo yanatakiwa kuja Bungeni, naomba sasa sijaona vizuri humu ulete mpango huo ili walau sheria hii ibadilishwe, pawe na mwanya wa kusamehe kodi kwa fedha za wafadhili mmoja wanaotaka kufadhili kujenga madaraja ya kwetu. Nafikiri hili unalifahamu na utaamua kulifanyia kazi na sisi Wabunge tuangalie maeneo haya, kwa sababu mfadhili anatusaidia na sisi tunasaidiwa katika bajeti yetu basi tuone namna gani sheria iruhusu kusamehe kodi kwa maeneo haya ya wafadhili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nishauri jambo moja, wenzangu wengi wameongelea sana kuhusu madini, nimeona pia katika kitabu chako cha hotuba yako Mheshimiwa Mpango ukurasa wa 49 umeandika kwamba Serikali haitaruhusu usafirishaji wa madini kwenda nje yaani kutoka kwenye mgodi kwenda nje, hili sina tatizo nalo. Nataka nishauri kitu kimoja, ukitaka kuzuia hii madini tuanzishe soko la madini, liwepo hapa nchini ili walau soko hili likitambulika Serikali ni rahisi kukusanya mapato katika soko. Tatizo letu lililoko hapa watu wakichimba madini katika maeneo yetu wanakwenda kwa njia za panya wanauza nje kwa sababu kuna soko huko nje. Kwa hiyo, ninashauri Serikali ianzishe soko la madini yetu yote yanayoonekana yanapatikana nchini ili wananchi wasitoroshe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi naomba niongee leo kama ushuhuda. Sisi wote tumeingia humu kuwakilisha wananchi wetu, lakini pia Serikali imeanza kazi na nimshukuru sana na niseme kabisa namuombea Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa sababu ameonesha nia ya kuisaidia Tanzania kwa kujitoa muhanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninajua hakuna anayeweza kusema anamuombea kwa upande fulani ninaoufahamu, lakini nimshukuru sana leo Mheshimiwa Mbatia amesema hapa mwenyewe kwa kauli yake na nimtaja kwa jina kwa sababu Hansard zinarekodi, anamuunga mkono Rais kwa suala hili la madini na ule mchanga ambao umesemwa sana sitaku kuusemea zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Biblia inasema kila mtu atabeba msalaba wake mwenyewe, na sisi naomba Waheshimiwa Wabunge nataka niwahamasihe jambo moja. Kubeba msalaba wake mwenyewe kwa siye tunaoabudu kwa dini ya Kikristo na Waislamu ambao wamefunga mwezi huu wa Ramadhani tumuunge mkono Rais wetu, sheria zitakapoletwa Bungeni tuanze kuweka vizuri mipango yetu ili katika haya Mheshimiwa Rais amejilipua, anahitaji kutusaidia na ameomba ridhaa wananchi tumempa. Habari ya kwamba ametoka chama gani, chama A, chama B tumeingia kwa vyama lakini ukiangali research inaonyesha tuangalie maslahi ya nchi, kwa sababu wanachama wetu wa vyama vyote hawafiki hata robo ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tutee Tanzania, tumeingia humu kwa vyama vyetu lakini sasa tutee mama yetu Tanzania. Kila mtu ameapa hapa na tumeapa kuitetea Tanzania, tunateteaje sasa? Nimesikia mchangiaji mmoja akisema hapa bado wakati wa kumpongeza Rais Magufuli. Unasemaje bado wakati mwenzako ameonesha nia? Mimi ninamsikitikia sana ndugu yangu Lissu, akionyesha nia mtu mmoja mshangilie kwa nia hiyo baadaye uhoji matokeo. Lakini nikuombe kaka yangu, mtani wa Singida tumtetee huyu ndugu aliyeonyesha nia kwa sababu ni Rais hakuna Rais mwingine zaidi ya huyu. Tukimtetea kwa nia aliyoonyesha atasonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wote wanahitaji maendeleo, na sasa tumeibiwa kwenye madini, tunaona tumeibiwa kwenye madini, na nimuombe Rais asiishie kwenye haya maeneo tu aende kwenye maeneo yote ya uchimbaji wa madini akadhibiti huko kabisa kwenye migodi ili migodi hii ionekane, iingize pesa za kigeni ili Tanzania tupate maji, barabara pia tupate vitu vingine vya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ndio nilitaka niseme ili watu waelewe na Waheshimiwa Wabunge waelewe kutoka CCM na kutoka CHADEMA kwamba Mheshimiwa Rais amesema kwamba analeta sheria ya mabadiliko ya madini huku tukasaidie hali hii kwa kutumia uwingi wetu humu.
Uwingi maana yake nini? Sisi Wabunge kwa sababu ndio tunaobadilisha sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda mbele zaidi ninajua kwenye hotuba hii ya Mheshimiwa Mpango kwanza nimshukuru sana amejitahidi sana kuelezea maeneo mengi sana lakini Serikali itusaidie katika maeneo haya ambayo imeanzisha tawala mbalimbali imeelekeza maeneo haya ya vipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vipaumbele ni kweli lazima tuviendee lakini kuna tozo ambayo sisi tunaiomba kama Wabunge kuongeza kwenye mafuta shilingi 40 tu. Najua yataongezeka, najua kuna tatizo kupanda na kushuka bei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja tu Serikali ikubali tuongeze jambo hili la ongezeko la tozo kwenye mafuta ili tupate maji vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina jinsi kwa sababu muda umekwisha naunga mkono hoja.