Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote na mimi ningependa kuanza kuunga mkono hoja, kwa sababu kama sikuunga mkono hoja, maana yake mipango hii ambayo tunahubiri hapa haitaweza kufanikiwa.

Pamoja na hilo na mimi nichukue nafasi hii kuendelea kumpongeza Mheshimiwa Rais wangu kwa jinsi anavyofanya kazi kubwa, kazi inayoonekana, na kwamba sisi wengine tunapokwenda misikitini ni kumuombea Mungu tu, ili Mungu aendelee kumtia ujasiri, nguvu na maarifa zaidi katika kuendelea kuwapigania Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mchango wangu wa leo, kubwa zaidi litakuwa ni ushauri tu, kwa sababu mambo mengi kule yanaendelea kufanyika. Nipende tu kuwaambia taarifa kwamba Wabunge watakaopenda kuungana nami, siku ya tarehe 22 Mheshimiwa Rais wetu mpendwa John Pombe Magufuli atakuwepo katika eneo la Halmashauri ya Chalinze akifungua viwanda, kuangalia barabara na maendeleo kwa ujumla wake, lakini pia atapata nafasi ya kuongea na Watanzania na kuwajulisha mambo mazuri yanayoendelea katika nchi ya Tanzania. (Makofi)

Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge nawakaribisheni sana; na kwa kuwa siku hiyo itakuwa ni siku ambayo Bunge nafikili linakwenda katika break ya sikukuu, kwa hiyo, ni vema mkaja Chalinze ili mpate maneno mazuri ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu leo nianze katika eneo la uchumi wa viwanda. Mambo mengi yanafanyika, lakini mimi nina ushauri mmoja hasa katika eneo la biashara ya ngozi.

Mheshimiwa Waziri Mwijage anafanya kazi nzuri sana, lakini Mheshimiwa zile chapa zilizoletwa na zinazopigwa ubavuni kwenye mifugo yetu zinafanya ngozi za ng’ombe wetu zinaendelea kupoteza ubora. Na malalamiko yamekuwa mengi sana katika viwanda vya huko nje kiasi kwamba hata tunapohubiri kuweka viwanda ndani tutakabiliana na changamoto ya kwamba bidhaa tunazopeleka nje ziko chini ya kiwango kama kama kinavyotakiwa na hivyo tutakuwa tunakabiliana na changamoto ya kutonunulika kwa bidhaa zinazotoka Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu Wizara iangalie jinsi ya kuja na utaratibu mzuri hata kama ni chapa hiyo hiyo iwekwe, basi iwe chapa ambayo inakaa katika maeneo ambayo hayataweza kufanya athari kubwa katika ngozi za ng’ombe wetu na ubora ukapotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia niendelee kuishukuru Serikali imefanya jambo kubwa sana katika kutoa ushuru wa mazao yanayosafirishwa. Hata hivyo, tunapozungumza kuondoa ushuru wa mazao pia tukumbuke kuongeza au kuweka mazingira mazuri ya upataikanaji wa mbolea zilizo nzuri, mbolea zilizo bora ili mazao yanayotoka yawe yenye ubora zaidi. Maana isiwe tu kwamba tunaondoa ushuru wa mazao lakini ule unaobakia nao unakuwa ni sehemu ya mzigo mkubwa kwa wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua yako mapunguzo makubwa hasa katika tani ambazo ziko chini ya tani moja kwa yale mazao yanayotoka mashambani kwenda masokoni. Mimi najua kwamba leo hata kama mimi ninakwenda Mbeya siwezi kwenda Mbeya kuchukua tani moja ya mchele ili wananchi wangu wa Chalinze wakale mchele mzuri wa Mbeya. Kinachofanyika ni kwamba nitakwenda Mbeya nitachukua tani zaidi ya nne ili nizipeleke katika masoko niweze kufanya biashara nzuri. Tutakapofanya majumuisho ningependa mliangalie tena jambo hili la upungufu wa ushuru, ule ambao unaozidi tani moja kwa sababu si kama kweli ile nia nzuri ya kusaidia wakulima wetu mauzo ya mazao yao wanaweza kufanikisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuipongeza Wizara kwa kuendelea na mkakati wake wa kumalizia na kuendelea kulipa yale mafao ambayo yalikuwa yanatakiwa yalipwe kwa wale ambao wanapisha ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo. Mheshimiwa Waziri nimeona katika kitabu chako na nimekusikiliza vizuri katika hotuba ya bajeti kubwa, ni kweli kwamba mmedhamilia kufanya jambo hilo. Ninachokuomba Mheshimiwa Waziri baada ya kupitisha bajeti yako jambo hili la Bandari ya Bagamoyo mlifanyie liwe kipaumbele chenu kikubwa. Kwa sababu kama hamtofanya hivyo hii mipango yote mizuri, yale mafao yalishalipwa na mambo mazuri ambayo mmeyapanga hayatoweza kufanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika eneo la madini. Pamoja na juhudi kubwa ambazo zimeshafanyika, na juhudi kubwa ambazo Mheshimiwa Rais wetu anaendelea kuzifanya, ikiwemo kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata malipo ambayo yamekuwa yakikosekana katika muda wote. Mimi nina jambo dogo la kuomba Serikali yangu, Serikali ifanye haraka kuleta hiyo Sheria ya madini hapa tuifanyie marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka kipindi hiko kabla sijakuwa Mbunge iliundwa kamati hapa, kamati ya Mheshimiwa Bomani akiwepo kaka yangu Ezekiel Maige, walikwenda wakafanya uchambuzi na wakaja na mapendekezo, lakini sijui mapendekezo yale yamefikia wapi. Hata leo tunamuona profesa wangu, rafiki yetu Bwana Osoro naye amekuja na mapendekezo yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachokiomba, tuielekeze Serikali yetu ilete mapema iwezekanavyo sheria hiyo ya madini ili tuweze kuiweka sawa na ili Watanzania wafaidike na kile ambacho tumekuwa tunahisi kwamba kinapotea siku zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabadiliko hayo ya Sheria ya Madini yaje pia kutatua tatizo kubwa lililopo sasa hivi; kwamba kila mtu ana pembe, inapofika katika suala la kutoa haki ya matumizi ya ardhi ya madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa takribani miaka miwili nimekuwa nikipiga kelele katika Bunge hili, lakini pia nimezungumza na Mheshimiwa Waziri na maafisa wa wizarani juu ya mgogoro uliopo katika kijiji cha Kinzagu na Makombe pale Chalinze. Unakumbuka niliwahi kusema hapa kwamba…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana.