Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Salma Rashid Kikwete

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mchinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu. Sambamba na hilo, nitoe pongezi zangu za dhati kabisa kwa Serikali yetu inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya. Kazi hizi nzuri zinazofanywa tukiziainisha hapa ni nyingi na kwa wingi wake huo kumekuwa na mafanikio makubwa sana ndani ya kipindi chake cha uongozi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, niwapongeze Mawaziri wetu wa Wizara ya Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mpango na Naibu wake kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya. Kwa ujumla bajeti hii ya Serikali imegusa kila sehemu yaani bajeti ya wananchi. Wananchi wamepunguziwa kwa kiasi kikubwa sana na bajeti inayoonyesha muelekeo na mwelekeo huu ni ushindi wa mwaka 2020 na hatimaye kuelekea kule mbele ya safari 2025, ongezeni hizo juhudi ili tufike 2025, na hatimaye tuzidi kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita kwenye maeneo kama mawili/matatu hivi. Eneo la kwanza, wakati Waziri anasoma bajeti ya Wizara ya Fedha alielezea suala la kinu cha kuchakata gesi pale Lindi ambacho kinu hiki kiko eneo linaitwa Likong’o. Baada ya hapo kwa kweli nilipiga sana makofi na nilipiga hili benchi nafikiri watu wengi walisikia. Msingi wangu mkubwa ni kwamba kinu kile kikipelekwa pale matokeo yake tunazungumzia hii nchi ni nchi ya viwanda, na ikiwa ni nchi ya viwanda na wananchi wa Lindi wale watafaidika na kauli mbiu hii ya Awamu ya Tano kwamba iwe ni nchi ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nini limetokea? Wakati anaisoma hii bajeti ya Serikali ambayo ndio inayotoa mwelekeo nini kinafanyika ndani ya Taifa, hakukuwa na jambo lolote lililojitokeza juu ya kinu kile na wananchi wa Lindi wanasubiri. Hata kama sio leo au kesho, lakini wapewe mwelekeo ni nini kinafanyika. Kikubwa zaidi hii ni gesi na gesi itaongeza uchumi wa Lindi, kiwanda kile kikijengwa Lindi kama Lindi hakuna kiwanda hata kimoja. Wananchi wa Lindi ni maskini lakini sio maskini kwa sababu hakuna rasilimali, ni kwa sababu mimi naamini wakati ulikuwa haujafika na sasa wakati umefika na wananchi wale wa Lindi kufurahia matunda ya nchi yao. Naomba atakapokuja Mheshimiwa Waziri anipe mwelekeo nini hatima ya kinu kile cha kuchakata gesi ndani ya Mkoa wetu wa Lindi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maji. Nilizungumzia suala la maji, sasa ninachosubiri hapa ni matokeo. Je, kati ya tarehe 3 mpaka 10 mwezi wa saba maji haya yatapatikana au hayatapatikana, kwa sababu maji ni kilio kikubwa sana ndani ya Mkoa wa Lindi hasa Wilaya ya Lindi Mjini na maeneo yake ya jirani. Tanzania tumejaliwa tuna mito, mabonde na tuna maziwa, kama tukiwekeza vizuri matatizo haya yatapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niende kwenye eneo la elimu. Mimi kwa taaluma ni mwalimu, sasa hii naiomba niishauri Serikali. Unajua sisi tuna senti, inaanzia senti tano hatukuanzia na senti moja mpaka senti mia moja. Ninachoishauri mimi kama mwalimu nilikuwa napata changamoto na hii changamoto inazidi kuendelea. Wakati zinatengenezwa zile fedha zitengenezwe hizi senti tano, ukiingia leo darasani kumfundisha mwanafunzi senti tano, senti 20 na senti 50 zinafananaje. Ni lazima tumuonyeshe kitu kwa uhalisia, tupeleke vitu wanafunzi wajifunze, hili ni muhimu sana ili wanafunzi waweze kutambua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la elimu kwa kweli tumepiga hatua, tumefanya mambo mengi sana kwenye elimu kwa kipindi kifupi. Tumeboresha shule zote zina madawati, upande wa walimu wa sanaa wote wamejaa, lakini tatizo sasa ni baadhi ya walimu kwenye maeneo ya sayansi. Sasa hapa ni lazima tuwekeze vya kutosha ili watoto wetu wafanye kazi kwa vitendo, halafu hii nitairudia tena na walimu wale ambao wamejifunza na hatimaye wakapata aidha Shahada au Diploma zao wasiendelee kwenda kwenye vyuo kwa sababu lengo ni kuboresha elimu, wabaki kwenye shule zile za msingi, jambo kubwa hapa waboreshewe mahitaji yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tatizo lingine kubwa, kuna suala zima la nyumba za walimu bado hapa tupo nyuma. Kwa kuwa tuna tatizo la nyumba za walimu, vijana wengi hapa wamezaliwa katika mazingira ambayo sisi tunayajua, sasa kijana aliyezaliwa na kukulia Dar es Salaam leo hii umpeleke kule Chikonje ambako mimi ndio nilianzia ile kazi yangu kwa mara ya kwanza, akifika akiangalia, akisikia yale mabundi na wanyama wengine wanalia mwalimu anakusanya na anaondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja, lakini nitakuwa ni mtovu wa fadhila… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)