Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Bupe Nelson Mwakang'ata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia bajeti hii muhimu.

Awali ya yote namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika bajeti hii muhimu. Pia naomba nimpongeze Waziri Mheshimiwa Dkt. Mpango na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Kijaji kwa kazi nzuri wanazozifanya pamoja na Makatibu Wakuu wote wa Wizara hii nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee naomba nimpongeze Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anazozifanya na nina salamu zake nyingi sana kutoka Mkoa wa Rukwa. Wanawake wa Mkoa wa Rukwa wanampongeza sana Mheshimiwa Rais, wanasema sehemu zingine wamezoea kumuandalia Rais ng’ombe, kuku na ndama lakini wanawake wa Mkoa wa Rukwa wamenituma wanasema hivi wa kazi nzuri alizozifanya Dkt. Pombe Magufuli, wamemwandalia mgolole, watambeba na mbeleko ya mgolole. Watambeba mgongoni kwa kazi nzuri anazozifanya, Mungu ambariki huko aliko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze kwenye maji. Wanawake wa Mkoa wa Rukwa hawana maji, karibu asilimia 20 wana maji, ukienda vijijini wanawake wanapata shida sana ya maji lakini Wilaya ya Sumbawanga Mjini ninaishukuru Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli imesimamisha matenki, maji watapata ya uhakika. Ninaishauri kule vijijini wanawake wanapata shida, maji yaende kule, ile shilingi 40 ya mafuta naungana na bajeti kwamba iende kwenye maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie kwenye suala la barabara. Mkoa wa Rukwa ni Mkoa ambao unalima mazao na yanakubali, una mvua za uhakika, lakini barabara ya Wilaya ambapo mazao yanatoka mengi, barabara inayotoka Kibaoni inapita Muze, Mtowisa na inaishia Mlowo ile barabara ni muhimu sana, imejengwa kwa kiwango cha kokoto, lakini bado madaraja yake ni shida. Kutokana na umuhimu wa barabara hii, ningeomba bajeti ya safari hii iweke kiwango cha lami kwa sababu ufuta, mpunga, ulezi na matunda yanatoka kule, ninaomba kwa bajeti hii ikumbuke hiyo barabara ijengwe kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze kwenye suala la elimu. Mkoa wa Rukwa hauna Chuo cha VETA, vijana wanapata shida sana. Suala la VETA limeongelewa muda mrefu sana na naipongeza Serikali katika bajeti yake imeongea kwamba itajenga Chuo cha VETA, ninaomba iipe kipaumbele Mkoa wa Rukwa kujenga hicho chuo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna chuo kingine ambacho amejenga mwanamke/mama ambaye hajasoma lakini amediriki kujenga Chuo cha Wauguzi, amejenga Chuo cha Ualimu na Chuo cha Kilimo, lakini Chuo cha Wauguzi kimefungwa bila sababu za msingi. Naomba Dkt. Mpango atakapokuja kutoa majumuisho hapa anieleze hicho chuo ni kwa nini kimefungwa? Chuo ambacho ni cha mwanamke ambaye hajawahi kwenda shule, ameamua kuanzisha chuo, kwa nini kifungwe bila sababu za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze kwenye suala la afya Mkoa wa Rukwa karibu Wilaya zake zote hazina Hospitali ya Wilaya. Ninaipongeza Serikali kwamba pale Mkoa wa Rukwa, Sumbawanga Mjini ile hospitali iliyokuwa ya Mkoa imepandishwa kuwa ya rufaa lakini hakuna Hospitali ya Wilaya. Wanawake na watoto wanapata shida sana wanapotaka kujifungua, wanaambiwa kwamba mkaanzie kwenye vituo vya afya na vituo vya afya kule wanaambiwa hatuna bajeti za mtoto na mama kujifungua bure. Ninaomba bajeti hii ikawasaidie kujenga Hospitali ya Wilaya ya Sumbawanga Mjini, Nkasi na Kalambo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana na ninaunga mkono hoja.