Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Agnes Mathew Marwa

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. AGNESS M. MARWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na Serikali kwa ujumla kwa bajeti hii iliyosheheni weledi na kuonesha kuwajali wananchi na hasa wananchi wa hali ya chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali katika bajeti hii iangalie jinsi ya kupata fedha mahali, shilingi hamsini au arobaini ili kumtua mwanamke ndoo kichwani na hasa mwanamke wa kijijini. Kule kwetu Mkoani Mara inafikia hatua wanawake wa kijijini inapofika jioni wanakosa hata hamu ya kuwapa mapenzi waume zao, kwa hiyo, niiombe sana Serikali ijitahidi kwa hili na iliangalie sana suala la maji na ikiwezekana hii pesa ya makinikia basi itakapokuja suala la kwanza liwe ni maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikumbushie suala la ahadi ya Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli lile la shilingi milioni 50 kwa wajasiriamali. Kwa kweli wananchi wetu wanaiulizia sana hiyo pesa na ninaamini Mheshimiwa Magufuli hadi sasa kafikisha asilimia kama 98 hivi ya utekelezaji wake imebakia hiyo asilimia mbili ambayo ni hiyo shilingi milioni hamsini hamsini, Mheshimiwa Magufuli tunaiomba ili kusudi hawa ndugu zetu walale kabisa vitandani wajue hawana chao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee zaidi naiomba Serikali yangu sikivu ya Chama cha Mapinduzi kwa ajili ya kushughulikia hili suala la kilimo, basi benki ya kilimo ipewe pesa na Serikali ili wapeleke mitaji vijijini, wananchi wangu wa Mkoa wa Mara mara kwa mara wanalalamika vyakula ni kutokana na hali halisi ya uchumi. Lakini pia ni kutokana hali halisi ya kwamba wanakuwa hawana mtaji na hawana vifaa, kwa mfano, wanatakiwa wakopeshwe na Benki ya Kilimo ili wafanye kilimo cha irrigation, kinaweza kusababisha kupunguza shida na matatizo kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilimsikia kaka yangu Mheshimiwa Heche akiongea kuhusu suala la kuwaandamanisha wananchi kule mgodini, ni kweli hakuna asiyejua kwamba wananchi wa Tarime kule mgodini wameumia, wamepata makovu, lakini hili suala Serikali imeshalishughulikia kwa kiasi kikubwa sana, lakini pia Mheshimwia Heche anapaswa kujua yale malipo au zile fidia za wale wananchi Mheshimwa Rais muda si mrefu sana wananchi wote watalipwa na Mheshimiwa Magufuli hakubali wananchi wa hali ya chini wanyanyasike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya labda hana ripoti hiyo na mimi ntakapoenda kule kuwakabidhi wale wananchi malipo yao nitamwita Mheshimwa, kwa sababu Jimbo lake sasa hivi amemwachia Mheshimwa DC wa Tarime ndio mwenye Jimbo anaitwa Mheshimiwa Luoga, ikiwezekana Mheshimiwa Rais muangalie sana huyu umpe hata Ukuu wa Mkoa maana kwa kweli ana kazi kubwa sana ya kufanya kule Ubunge badala ya u-DC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Magufuli kwa kazi nzuri anayoifanya. Hawa wanaombeza Mheshimiwa Rais kwamba ooh! Sijui ananunua ndege! Mlitaka awanunulie magari ma- vogue ili kusudi muendee Majimboni kwenu. Wananchi wa hali ya chini wanapanda hizi ndege na bei au gharama za ndege zimeshuka na sisi Wabunge tuna uwezo wa kwenda Dar es Salaam kufanya shughuli zetu na asubuhi tukarudi Bungeni. Isitoshe hizo ndege ninyi wenyewe mnazipanda, kila siku tunakutana ndani ya hizo ndege, kwa nini msiache kupanda? (Makofi)

Kwa hiyo, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais na kwa taarifa yenu kinakuja kitu kipya tena mwezi ujao. Hiyo ni kuonyesha jinsi gani Mheshimiwa Rais anavyotekeleza utekelezaji wake au kutekeleza Ilani aliyoiahidi. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuhusiana na masuala ya miundombinu hasa barabara. Hivi ni kweli kwamba hamuoni wakati tunawaona huwa mnaondoka hapa siku ya Jumamosi na Jumapili mnarudi hapa na Jumatatu mnakuwa Bungeni tena kwa magari. Zamani mlikuwa mnaenda hivyo kukiwa kuna mabonde?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kutoka hapa Dodoma mpaka Musoma kupitia Singida ilikuwa inatumika siku tatu lakini leo unaondoa asubuhi, jioni unafika na kesho yake unarudi unafika Bungeni na kipindi hicho Mheshimiwa Magufuli alikuwa ni Waziri wa Barabara. Kwa hiyo, mnapaswa kujua kwamba ametekeleza kwa kiasi gani au ametekeleza amefikia hatua gani. Hata wewe ukiamka nyumbani kwako sio kila kitu unachokitekeleza kwa siku moja! Mambo yanaenda taratibu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)