Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana naomba nichukue furasa hii kwanza kumpongeza Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu nzima ya Wizara ya Ardhi kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya na kuleta matumaini makubwa. Migogoro mingi imeendelea kupungua na tunaendelea kuomba kwamba waendelee kufanya kazi hiyo kubwa ili migogoro ya ardhi sasa hapa nchini iishe. Tunaomba ile migogoro hasa ile ya Babati ambayo Wabunge wenzangu wote tumekubaliana kila anayepata fursa aisemee, ile ya vijiji vya Ayamango, Gedamar na Gidejabug wale wananchi wapatiwe maeneo mbadala kuna mapendekezo tumeshaleta, Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu ifanyie kazi ili Wizara ya Ardhi iweze kutoa vibali, lakini pia ile migogoro ya mashamba ya kule Kiru yafanyiwe kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muhimu Mheshimiwa Waziri ninaomba utuletee sheria mpya hapa ndani ya hii Sheria ya Ardhi kipengele cha kuzuia matumizi ya ardhi ya kilimo ilindwe kisheria ili ukitaka kubadilisha matumizi ya ardhi ya kilimo ije hapa Bungeni kwa sababu maeneo mengi yenye rutuba Tanzania yamebadilika matumizi sasa yamekuwa makazi, viwanda na matumizi mengine ambapo hayo matumizi mengine tungeweza kuyapangilia yakawa katika maeneo mbadala na italinda ardhi yetu ya kilimo, kwa sababu hatuna uwezo kama Serikali kuandaa maeneo mapya ya kilimo katika maeneo ya jangwa au maeneo ambayo hayana rutuba kuwa ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningeomba kwamba la Wabunge wote wamelalamikia suala la kupatiwa vifaa, mpango wenu mzuri wa kuweka vifaa vya kupima kwenye Kanda haitoshelezi, tunaomba muwe na mpango, mtukopeshe wala hatuhitaji kwamba Serikali iweke bajeti ituletee bure, kila Halmashauri tukopeshwe vifaa ili sisi tutaendelea kulipa hilo deni la vifaa vya kupimia ardhi zetu, ili tupime viwanja vya watu, mashamba ya watu lakini pia vifaa vya kutolea hati miliki zile za kimila huko katika Halmashauri zetu. Hiyo itatupunguzia sehemu kubwa ya matatizo ili wananchi wote waweze kupata huduma ile muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine hapo naomba kwamba kuna ile asilimia ambayo kodi ya ardhi inapolipwa ile Wizara basi iwe badala ya kufika Hazina na huko Halmashauri iweze kukata moja kwa moja ili tuweze kuyapangia matumizi ya ile fedha ambayo tunawasaidia Wizara kukusanya ile kodi ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna migogoro mingi ambayo sasa hivi kwa sababu Serikali haijatoa tamko maalumu kwamba watu kuvamia maeneo ya hifadhi, kuvamia maeneo mbalimbali na katika mali za watu Serikali iweke msimamo kwamba nini maamuzi ya Serikali na mahali ambapo Serikali huko nyuma tayari ilishakosea kwa kuanzisha vijiji ndani ya maeneo ambapo ni hifadhi au ni mashamba mengine ya lease, basi mgogoro huo utatuliwe mapema ili kila mmoja aweze kuishi kwa amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine pia naomba iangaliwe namna kwa wale waliokuwa Watanzania ambao sasa wamebadilisha uraia wao kwenda nchi zingine ili huko wapate haki, pawe na mpango maalum. Najua Wizara ya Ardhi mnao mpango masuala ya derivative rights, lakini waweze kurudi nyumbani angalau kama wanataka kuwekeza kujenga nyumba na kadhalika, waweze kuwa na haki hiyo kwa sababu kuna diaspora kubwa ambao wana uraia wa kule lakini ni Watanzania kiasili na wao waweze kupata haki yao kuja kuwekeza hapa nyumbani bila kuwa kupitia TIC. Labda anataka kuweka nyumba tu ya kuishi na nini na wengine wana ndugu zao ambao wapo hapa, lakini wakirithishwa ile mali ni haki yake kurithi ya mzazi wake au baba yake au babu yake, akija hapa inakuwa ni mgogoro kwa sababu yeye tayari anao uraia wa nchi nyingine. Watanzania wengi wanakosa fursa hiyo naomba muangalie namna kwa wale ambao walikuwa Watanzania wameenda wamebadilika sasa kuwa raia wa nchi nyingine aendelee kuwa na haki maalum, kuna haki zingine wasipewe lakini angalau hii ya kwao ya kuja kuwekeza humu nchini basi pawe na mfumo mzuri waweze kuja na kuwekeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muhimu na ninaendelea kusisitiza kwamba hivi vifaa tumeona pale nje mmetuletea aina nyingi, pawe na mpango maalum tuweze kukopa kila Halmashauri kwanza itakuwa fursa ya kumaliza migogoro ya watu kupatiwa hati miliki na hati za kimila, lakini pia maeneo mengi yatakuwa yamepimwa, muhimu ni coordination baina ya Halmashauri zetu na Wizara, namna ya kuelekeza Maafisa Mipango Miji na namna ya kupanga makazi hata huko vijijini tunahitaji kupanga matumizi bora ya ardhi ili huko mbele tunakoelekea migogoro isiendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na ninaunga mkono hoja.