Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, kwanza kabisa kwa dhati ya moyo wangu nimshukuru sana Naibu Waziri wangu Suleiman Said Jafo, ananipa ushirikiano mkubwa, ananiheshimu, tunafanya kazi vizuri na kwa raha sana.
Pili, namshukuru sana Katibu Mkuu Engineer Iyombe na Manaibu wake, Deo Mtasiwa anayeshughulikia masuala ya afya na Benard Makali ambaye anashughulikia masuala ya elimu pamoja na Wakurugenzi na Watumishi wote wa Wizara ya TAMISEMI; wanatupa ushirikiano mzuri na tunafanya kazi vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo nipate fursa ya kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Kibakwe kwa kuniamini, lakini kwa kuendelea kunivumilia wakati naendelea kutekeleza majukumu ya Serikali. Nataka niwafahamishe kwamba nawapenda na baada ya Bajeti hii nitakwenda kuonana nao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu imepata wachangiaji wengi sana. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote wa pande zote za Bunge kwa kutoa michango mingi yenye tija na maudhui mbalimbali katika kuboresha utekelezaji wa Serikali katika Wizara yangu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimepata wachangiaji na nikushukuru pia wewe na Wenyeviti wote mliosimamia Wizara yangu, kusimamia uchangiaji wa waliozungumza 140, si jambo dogo; na walioandika kwa maandishi 60 na wenyewe wamenipa michango yao, nawashukuru sana. Michango hii mingi pamoja na uzuri wake na aina na staili mbalimbali ambavyo imetolewa mimi kwangu nilikuwa nachukua yale muhimu yanayonisaidia katika kufanya maisha ya Watanzania yawe bora. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naamini hata ambao hawakusema, nao wangependa waseme, hata ambao hawakuandika nao wangependa waandike, lakini itoshe tu kwamba hawa wachache waliosema wametosha kuwakilisha wote na kwa hivyo, wote ndani ya Bunge hili mmesema juu ya Wizara yangu. Nawashukuruni sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, siyo rahisi sana kujibu hoja zote kadri zilivyotolewa maana ni nyingi mno. Tutaandaa matrix maalum itakayokuwa inazungumza aliyesema na aliyeuliza jambo na ufafanuzi wake tulivyoutoa katika kabrasha maalum ambalo tutawapatia kabla hatujaondoka hapa Bungeni, ili kila mmoja ajue hoja atakazosema mtu mwingine ili aweze ku-refer katika hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, zile chache nitakazobahatika kuzijibu, basi kama nitajaliwa kusema, nitazisema. Hata hivyo, ninazo nyingi sana hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu mwaka 2015 tukiwa kwenye uchaguzi, Watanzania wengi waliomba kwa dini zao mbalimbali, kwa ibada mbalimbali wakiiombea nchi hii ipate kiongozi atakayewapeleka mbele. Ni imani yangu kwamba Mwenyezi Mungu aliyapokea maombi ya Watanzania wengi na ndiyo maana tumempata Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, ambaye ameanza kutupeleka mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Rais Magufuli ni nani? Rais Magufuli ni mtu anayechukia rushwa, ufisadi, ubadhirifu, matumizi mabaya ya madaraka, lakini anakusudia kukusanya kodi. Pia akishakusanya kodi anataka kubana matumizi. Dhamira yake ni ili kupunguza gap tuliloacha wanyonge na maskini wanaoishi maisha ya tabu katika nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mifumo ya kisiasa katika dunia inatofautiana. Iko mifumo ya kijamaa na fikra na dhana za kijamaa, lakini iko mifumo ya kibepari na fikra na dhana za kibepari. Mtu anajitokeza na kujipambanua kama kiongozi wa watu; asipowazungumzia na kuwapenda maskini walioko chini, kuwanyanyua wakaribie walioko juu, huyu dhana yake na fikra yake ni ya kibepari. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, misingi ya Taifa letu imejengwa katika fikra na mawazo ya Mwalimu Nyerere, ambaye aliheshimu usawa, haki na umoja. Usawa kwa kipato, usawa kwa hadhi. Kadri tunavyoacha gap kuwa kubwa kati ya maskini na wenyenacho, hatujengi Taifa sustainable. Taifa hili litakufa na mara moja litaondoka katika amani na utulivu, vitu ambavyo tumevijenga kwa muda mrefu sana wa nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa maono haya anayoyafanya katika kuhakikisha kwamba nchi yetu inarudi kwenye mstari sahihi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Singapore, chini ya Waziri Mkuu Lee Kuan Yew, mwaka 1999 alipoichukua nchi ile ali-dedicate kuhakikisha kwamba anapunguza na kuondoa unyonge wa watu masikini. Matajiri hawa huwa wapo tu, lakini kazi ya kiongozi ni kuwachukua maskini, kuwasukuma, kuwaleta juu. Walikuwa na Sera kama zetu na wao walikuwa non-aligned movement, lakini leo wamefika mbali sana kwa sababu wamekubaliana wote na ni akili ya mtu huyu mmoja ndiyo imewafikisha hapo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, China, mwaka 1949 hadi 1980 chini ya Chama cha Kikomunisti, China imetoka ilipokuwa chini ya mawazo ya Mao Tse Tung na rafiki yake Biao ambao waliitoa China ilipo na walipewa fursa ya mawazo yao ku-prevail wakaifikisha China ilipofika. Nawaomba sana Watanzania, tumpe ruhusa Rais, Mheshimiwa Dkt. Magufuli, ana dhamira ya dhati, anatupeleka ambapo wote tunaona ni sahihi. Nami niseme pande zote mbili, dhana hiyo na sense hiyo inaonekana hata pamoja na msimamo ya Vyama vyetu, tukubaliane kwamba Rais wetu anaenda vizuri. Tuache afanye kazi, ashughulikie huu upungufu ambao upo?
Mheshimiwa Naibu Spika, wako watu kwa namna tunavyokuwa tunajenga Taifa linalopotea; utaona linaanza kuwa na madalali wengi na watu waacha kufanya kazi; Taifa linalopotea utaona watu wanakubaliana katika kupata fedha bila kufanya kazi; Taifa linalopotea utaona wenye nguvu wanaacha kufanya kazi, wanyonge na wasio na afya nzuri ndio wanaofanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukitoka leo kuanzia Dodoma mpaka kufika Dar es Salaam, miezi ya kilimo utakaowaona wanafanya kazi mashambani ni wazee na watoto. Vijana hawafanyi kazi. Ni lazima uamuzi wa dhati ufanyike na tukubaliane wote kama Taifa kwa sababu hata hizi siasa tunazozifanya leo, ni kwa sababu ya amani na utulivu na hiyo gap kati ya wenye nacho na wasio nacho imekuwa ikishughulikiwa kwa muda mrefu kwa miongo ya viongozi waliopita tangu tumepata uhuru mpaka sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunahitaji mawazo mapya, nami naamini mawazo sahihi ni ya Rais Magufuli. Rais wa namna hiyo anayetaka kuleta mabadiliko katika nchi yoyote ile duniani na hasa tulizoziona zikibadilika duniani, Rais wa namna hiyo huwa hataki urafiki na mtu, hataki aonekane kama ana kundi na ndivyo alivyo Mheshimiwa Rais Magufuli. Hana rafiki, hana swahiba, yeye ameipeleka nchi mbele; ukileta mchezo, anatuambia tunasonga mbele, wewe unabaki, tunasonga mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba Waheshimiwa Wabunge wa pande zote, wale tunaomuunga mkono Mheshimiwa Dkt. Magufuli tumfuate na tusonge mbele. Kura alizopigiwa Mheshimiwa Rais wala hazikutoka kwa misingi ya pande hizi mbili. Alizikuta kura za watu wanaonung‟unika na maumivu mengi hawajui cha kufanya; wakitusikiliza upande huu hawatuelewi, wakitusikiliza upande huu hawatuelewi. Tuwaache Watanzania wamfuate Mheshimiwa Dkt. Magufuli na sisi tuwaunge mkono na tusaidie Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Magufuli kwa haya tunayoyafanya hapa ndani ya kupitisha Bajeti ili mambo yaweze kutekelezeka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema, zimechangiwa hoja nyingi sana, lakini nianze kujibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge. Lilizungumzwa hapa suala la mgawanyo wa fedha ya Jimbo. Ni kweli nikiri kwamba tulifanya makosa katika mgawanyo wa fedha za kichocheo cha maendeleo ya Majimbo na kuzipeleka kwenye Halmashauri badala ya kuzipeleka kwenye Majimbo. Ndugu zangu, ndiyo tumetoka kwenye uchaguzi, tulikuwa tumewekana sawa, lakini basi imetokea kwa bahati mbaya, mtuwie radhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumetoa waraka kwa Wakurugenzi wote nchini. Kwanza, tumewaambia wasimamishe na kama wamefanya, basi warudishe na kuhakikisha kwamba wanazigawa kwa misingi ya Majimbo, hizo hizo zilizokwenda kwa sababu hapa tuna changamoto tatu. Moja, ni kwamba kuna maeneo ambapo yamezaliwa Majimbo mapya, lakini fedha imepelekwa inataja Jimbo la zamani. Kwa hiyo, Jimbo lingine hili linapata shida.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili nalijua, kwa mfano, kule Bunda kuna rafiki yangu Boni halafu kuna Ester Bulaya. Kwa hiyo, unakuta pale sasa hawajui ni nani anachukua kipi? Tumetoa maelekezo mazuri, naamini watafanya masahihisho na vigezo vinavyotumika ni vile tulivyovisema hapa siku moja kwamba asilimia 25 ya fedha hiyo inayokuwa imepangwa kama ni fedha ya Mfuko wa Jimbo, huwa inagawanywa sawasawa (pro-rata). Asilimia 75 inayobakiwa inagawanywa kwa misingi ya ukubwa wa eneo, kiwango cha umaskini, lakini pia inagawanywa kwa kuzingatia kigezo cha idadi ya watu.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vigezo kwa mchumi aliyebobea ambao tunawaweka kwenye Halmashauri zetu, haviwasumbui katika kupiga hesabu. Hata hivyo, tunawasimamia kwa karibu ili tuweze kuona wanapiga hesabu vizuri na Majimbo yote yanagawanywa; kama ni ndogo, basi wote tupate kidogo kidogo, kama tutajipanga upya kwa mwaka unaokuja, tuje na hesabu nzuri zaidi ya bajeti ya kutosha kwa ajili ya Majimbo.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni suala la Viti Maalum, kuwa Wajumbe wa Kamati za Mipango na Fedha kwenye Halmashauri. Jambo hili lina logic, lina sense, hakuna namna unaweza ukalipinga hivi na unaweza ukaonekana mtu wa ajabu ukilipinga bila kutoa sababu za maana. Maana hawa Wabunge wa Viti Maalum ni Wawakilishi wa wananchi. Kikao cha Kamati ya Fedha kinaalika Wajumbe mbalimbali na kikao kile wanachotoa pale ni mawazo, wala Mbunge hawi Mwenyekiti; wote ni Wajumbe tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kuingia mle akatoa mawazo yake juu ya rasilimali zilizopelekwa kwenye Halmashauri, ubaya uko wapi? Mimi mwenzenu siuoni! Hata hivyo, masuala ya Kiserikali yanakwenda kwa mabadiliko ya kimaandishi. Kwa sababu jambo hili lilikuwepo, acha tulichukue tukalifanyie kazi na baadaye tutakuja na msimamo wa Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Walimu kutopandishwa madaraja, wengi wamesema. Haya yamesemwa kwenye maoni ya Kamati lakini Wajumbe wengi wamesema. Mniwie radhi kwamba siyo rahisi kuwataja majina, maana vinginevyo nitachukua muda mrefu, lakini nitatambua kwenye majibu rasmi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Walimu kutopandishwa vyeo mwarobaini wake sasa umefika. Nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wa Bunge lililopita kwa kupitisha Sheria ya Tume ya Utumishi wa Walimu. Hivi katika bajeti yangu hii, nimeleta bajeti ya kiasi zaidi ya Shilingi bilioni 10 kwa ajili ya Tume hii kuanza na tunaendelea kuzungumza. Tunaamini Tume hii Makao Makuu yake itakuwa Dodoma ili waweze kuwahudumia Walimu kwa urahisi. Tume hii ikianza, ndiyo itakayomaliza matatizo yote haya ya Ualimu ikiwa ni pamoja na hili la kupandisha madaraja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Walimu wetu wameumia sana. Mtu anafanya kazi, maana kupanda madaraja ni kila baada ya miaka mitatu, mitatu. Mtu anafika miaka tisa hata kumi na mbili hajapandishwa daraja, halafu aliyeanza kazi, ame-lobby lobby amefanya ujanja, sijui ametoa rushwa, amepandishwa daraja mpaka anamzidi aliyefanya kazi miaka kumi. Hii haiwezi kukubalika na tutaliangalia. Tume hii siku nitakapokuwa naizindua, nitahakikisha first task ni hiyo na hata ikibidi tuweze kutengeneza upandaji wa madaraja wa mserereko ili waweze kukutana na wale waliopanda wakipitiliza, basi na wenyewe tutawashusha kwa sababu wapo pia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo limechangiwa na wengi lakini pia na Kamati ya Bunge ya Kudumu ya TAMISEMI, ni mabasi yaendayo haraka Dar es Salaam, yaani DART. Ni kweli mradi huu ulikuwa na makando kando mengi sana. Kweli kabisa! Hakuna asiyejua, ni ukweli kabisa! Makando kando mengi ya DART kama DART, yamesababishwa na DART kumchukua mwendeshaji wa muda. Maana kulikuwa na mwendeshaji wa kudumu anayekuja kuendesha mradi wa mabasi yaendayo kasi Dar es Salaam, ambapo kulingana na miundombinu ilivyokuwa imekamilika, mchakato wa kumpata mwendeshaji wa kudumu unaweza ukachukua miaka miwili hadi mitatu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, yakatokea mawazo mema na mazuri tu kwamba jamani hivi hapa nchini kwetu hatuwezi kupata mwendeshaji wa muda kwa kipindi cha miaka miwili hadi hapo tutakapompata mwendeshaji wa kudumu? Jambo hili likaonekana ni jema kwa sababu shida tunayoipata Dar es Salaam tunaiona, miundombinu imekamilika, tunasubiri nini? Kwa nini tusianze? Ukiangalia kwa watu wenye uzoefu wa ku-operate mabasi mengi na wenye facilities, ikiwa ni pamoja na garage kubwa, maeneo makubwa ya kuweza kutunza magari na mass operation, a big flit ya mabasi kama 100 hadi 200, wenye uwezo huo ni UDA.
Kwa hiyo, UDA na wao wakaomba kama walivyoomba waombaji wengine. Katika ku-evaluate hao waliokuwepo huko wakati huo, wakaona kwamba UDA wanaweza wakatusaidia katika ku-operate mabasi haya kwa muda. Kilichotokea ni kwamba kumbe UDA nyuma yake ana makandokando mengi. UDA inamilikiwa sasa na kampuni inaitwa SGL. Kampuni ya SGL ikawa ime-assume kwamba imechukua the full control ya Shirika la UDA na ikaanzisha kampuni ya UDART iliyokuja kuomba kazi DART.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kilichotokea pale ni kwamba, sisi tulipoingia mwezi Desemba, tukaanza kazi, tukaangalia, tukawaambia hapana, uhalali wa UDA huku tunauona una mashaka. Kwa hiyo, hatuwezi kuendelea na huyu.
Kwa hiyo, mambo makubwa matatu tuliyo-achieve ni yafuatayo:-
Moja, tukawaambia sikiliza, wewe unasema una full control ya Shirika la UDA, umetoa wapi hiyo full control? Anasema nimenunua hisa kutoka Jiji. Lete vielelezo; akaleta. Tukamwambia lakini unadaiwa wewe! Huko Jiji la Dar es Salaam kwenyewe hujamaliza kulipa deni lote. Akasema ninachodaiwa nadaiwa tu, lakini hizi hisa nilikwishazinunua. Kwa hiyo, ushahidi wa hayo na kesi ya Jiji na UDA na SGL ilikuwepo Mahakamani.
Mheshimiwa Naibu Spika, bahati mbaya sana tulipofikiria kushughulikia jambo hilo, tukajikuta tunafungwa, maana yake waliingia mpaka Deed of Settlement kati ya Jiji na Simon Group. Deed of Settlement na wakasajili Mahakamani ya kwamba kweli amenunua, lakini tunamdai fedha hizi na kwamba akitulipa fedha hizi tunampa the full control ya shares zetu asilimia 51.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo tulimkuta SGL amemfungia sandukuni TR ambaye ana asilimia 49 shares. Tukaenda pale tukamwambia kama humfungulii huyu, sisi hatuzungumzi na wewe. Akaenda Mahakamani akasema nafuta hii kesi ya kumfungia huyu Mahakamani, akamfungulia. Tukamwambia TR wewe asilimia zako 49 zipo? Akasema asilimia zangu 49 mpaka nikazi-verify. Akaenda aka-verify, tukazikuta asilimia 49 zile, tukazikomboa, zipo. TR anazo asilimia 49 za hisa. Kwa hiyo, Serikali mle kwenye UDA ina asilimia 49, lakini tukamkuta UDA amechukua unissued shares au unallotted shares, amezichukua zote zilizokuwa zimebakia za wabia, wanahisa wawili kati ya Jiji la Dar es Salaam na Treasury Registrar, anasema zote zile za kwake.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hizi 49 tumeshazikomboa lakini anasema hizi unallotted shares, hisa zisizogawiwa, anasema na hizi ni zangu, Bodi iliniuzia. Tukaenda tukamshinda, akasema nakubali bwana, sitaki kupoteza huu mradi, narudisha. Kwa hiyo, amekubali, amezirudisha zile hisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tumekomboa unallotted shares, tumemrudisha TR kwenye nafasi yake ya share zile 49, tumebakia na kampuni ya SGL ambayo ni kampuni ya Mtanzania ambayo ina hisa 51 alizozinunua Jiji. Sasa kila kitu Jiji as an authority wamekifanya, Jiji as an authority wamepokea hizo pesa; Jiji as an authority wamekubali kuuza. Leo mkisema turudi tuka-nullify ile sera, kwa maslahi ya nani? Maana sasa mradi unasimama. Kutafuta mtu mwingine it will take us three or four years. Serikali hii kazi yake pia ni kuwezesha, lakini tunawezesha watu ambao wanafanya mambo kisheria. We have tried to prune him in every wrongs that he did; tumemtoa huko!
Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, tutakubaliana, naomba nisiendelee na hili maana ni refu mno. Tunakuja kutoa taarifa rasmi ya Serikali ndani ya Bunge na Wabunge tutaliangalia on merits tutakubaliana. Mkisema tusifanye, Serikali hatulazimishi. Mkisema tufanye, kwa sababu Dar es Salaam kuna foleni watu wa Dar es Salaam na sisi tunaumia, tutaangalia the option.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi hatulazimishi kufanya, tumeyakuta madudu tumeya-clear. Sasa kwa nini tubebe sisi msalaba? Msije mkaniua, mkanishikia vifungu vyangu hapa! Nipeni bajeti yangu mimi niendelee, nina mambo mengi ya kufanya ya afya na kila kitu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Property Tax kwamba sasa ikusanywe na TRA; hivi nani hapa haiamini TRA? Mkusanyaji mkubwa wa kodi katika nchi hii, whatever kodi, popote pale, ni Waziri wa Fedha. Waziri wa Fedha ndiyo mwenye TRA! Sasa kama anasema ana njia na ana muscles za kukusanya zaidi kuliko sisi, kwani hivi bajeti za Halmashauri za Mamlaka ya Serikali za Mitaa zinatoka wapi? Over 95 percent Halmashauri zetu hazina uwezo wa kujitegemea hata kwa asilimia tano. Hela zote zinatoka Serikali Kuu Hazina, anayekusanya ni TRA. Sasa akisema anataka kukusanya, sana sana unamwambia baba nakushukuru, ukikusanya niletee. Basi! Mimi sioni kama kuna tatizo hapa! (Makofi)
Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, sisi tutadai haya mafungu tunayopendekeza, Waziri wa Fedha atuletee. Akisema anataka kukusanya, hewala; akisema kusanyeni nyie hewala, lakini tumekubaliana kwamba sisi Mamlaka ya Serikali za Mitaa hasa kwa mfano kwa Dar es Salaam, tulikuwa tumejiandaa vizuri sana katika kukusanya kodi hii, naye akasema mimi sifanyi chochote, nitapokuja tutashirikiana kwa pamoja, lakini fedha hii itakusanywa. Ninyi kinachotakiwa kufanya, si tumepitisha bajeti, tumwombe Waziri wa Fedha atupe fedha zile tulizopitisha, that is it.
Mheshimiwa Naibu Spika, hilo naomba tuliangalie, lakini kimsingi sioni tatizo lake na wala sitaki kuingia kwenye matatizo na sioni tatizo kwa Waziri wa Fedha na wala sioni kwamba ana nia ya kutokuisaidia Wizara yangu kufanya kazi, mimi naiona dhamira yake ni njema. Kazi yangu mimi na nyie Wabunge ni kusimamia, mimi kuhakikisha kwamba napata fedha kutoka kwa Waziri wa Fedha ili tuweze kupeleka malengo na bajeti iweze kutekelezwa mbele zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, posho za Wenyeviti wa Mitaa, Vijiji na Vitongoji. Sheria namba saba (7) na nane (8), ukizisoma kwa pamoja na program mbalimbali tulizonazo tulikubaliana kwamba asilimia 20 ya mapato ya ndani yapelekwe kwenye vijiji na asilimia 20 ya mapato ya ndani haya ni vyanzo vya ndani, actual own source na ile ambayo huwa inapelekwa kutoka Hazina ya fidia ya vyanzo vya mapato vilivyofutwa, vilivyokuwa kero. Kwa hiyo, ukichukua ile, ndiyo inayoitwa own source kwenye Halmashauri, yaani vyanzo vile vinavyopatikana na vile ambavyo vilifutwa na Serikali Kuu inavifidia kwenye Halmashauri. Ukivijumlisha ndiyo unatakiwa uchukue 20 percent uipeleke kwenye vijiji.
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha hii kwa baadhi ya maeneo ya vijiji na kwenye Halmashauri zetu inawasaidia sana Wenyeviti wa Vijiji kwa mgawanyo ufuatao:-
13% ya fedha hiyo inakwenda kwenye vijiji; 4% inakwenda kwenye Ward C; na 3% inakwenda kwenye Vitongoji. Kwa hiyo, at least hata kama ni kadogo, kanaweza kufika.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii fedha siyo ndogo kwa kila eneo; own source ya Dar es Salaam ni Shilingi bilioni 85. Hebu piga 20 percent halafu uipeleke kwenye Mitaa kwa own source ya Manispaa ya Ilala peke yake ni bilioni 85. Piga 20 percent of it, peleka kwenye Mitaa, it’s a big sum, inaweza kusaidia. Own source ya Mpwapwa inaweza ikawa ndogo, ukichanganya na ile ya ruzuku, inaweza ikasaidia kitu.
Waheshimiwa Wabunge, tuna mambo mengi ya kufanya, tuna shida nyingi kwa wananchi wetu. Hili ni jambo jema! Nami nasema naona kabisa umuhimu wa Wenyeviti wa Vijiji na Wenyeviti wa Vitongoji, ikiwa ni pamoja na Madiwani. Wanafanya kazi nzuri, lakini iko nature ya aina fulani za kazi if we exaggerate tutajikuta nchi hii kila mtu anastahili kulipwa hela inayotoka Hazina na hela hiyo haitoshi. Ziko kazi nyingine kwa nature yake ni kutaka heshima tu. Mashehe na Wachungaji, hawalipwi mishahara. Wanachongojea ni sadaka ikipelekwa, hewala; isipokuwepo, hewala.
Vile vile zipo nature za kazi nyingine ni za kujitolea, kwa mfano, Wenyeviti wa Vijiji. Kwanza unaheshimika, watu wanakuja pale kwako, lakini vijiji vyenyewe mle mle ndani vina makusanyo. Ndiyo maana vijiji huwa vinatakiwa kusoma mapato na matumizi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kila kikao baada ya miezi mitatu, kijiji kinatakiwa kusoma mapato na matumizi. Hivi huwa wanasoma mapato na matumizi yapi? Kuna incomes mle ndani za minada, soko na nini. Naamini, Waheshimiwa Wabunge wote wa pande zote twendeni tukatafakari vizuri tukaangalie uhalisia, tukikutana hapa kwenye bajeti nyingine, tunaweza tukawa tumeboresha wazo hili, tukaona namna bora ya kulifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais amehimiza usafi, lakini tunazo sheria mbalimbali. Usafi ni lazima uende pamoja na upangaji wa miji yetu. Lazima kila Halmashauri nchini iweke utaratibu wa kuwekeza katika upangaji wa miji.
Mheshimiwa Naibu Spika, problem ya nchi yetu, shida yetu sisi Watanzania, kila mmoja anategemea program. Kila mmoja anategemea mpango utakaokuja na fedha, tena zisiwe za ndani tu, ziwe mpaka za nje, huyo mtu utakuta amechangamka kweli! Yako mambo wakati mwingine hayahitaji hata pengine program! Hata wakati mwingine hayahitaji fedha!
Mheshimiwa Naibu Spika, tuchukulie wewe una Maafisa Ardhi watatu, wanne kwenye Halmashauri yako, hebu niambie kama kila siku wanapima square meter labda ya 5,000, yaani kila siku wanachukua na vibarua wale wanaenda site wanapima; si wamefundishwa kupima na kupanga! Hivi kweli kama wangekuwa wanafanya hiyo kazi kila siku, baada ya miaka mitano, miji yetu itakuwa vile? Wamekaa pale wanangojea waletewe program na pesa wakati wameajiriwa kwa ajili ya kazi ya kupima na kupanga!
Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba Waheshimiwa Wabunge, nyie ni Wajumbe, kwenye Vikao vya Baraza la Madiwani, twendeni tukawahimize watu wetu, pamoja na program zinazoandaliwa na Wizara ya Ardhi, pamoja na program zinazoandaliwa na Wizara yangu ya TAMISEMI, bado tuna haja ya kutumia ile human resource tuliyonayo kule hata kama ndogo kuhakikisha kwamba inafanya kazi ile kila siku ili kupunguza migongano na matatizo yanayotokana na miji yetu kutokupangwa vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika usafi wenyewe wa kawaida huu, tumetoa wito na Mheshimiwa Rais ametoa mfano. Nachukua nafasi hii kumpongeza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, ameanzisha utaratibu mzuri wa kuwafanya vijana wachangamkie usafi na anasema usijifanye mstaarabu, kuwa mstaarabu na ili uwe mstaarabu ni lazima uonyeshe usafi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, usafi wa mazingira ya makazi yetu, usafi wa sehemu zetu za biashara ni muhimu sana. Tujitokeze Watanzania kutengeneza Taifa lenye usafi na kila mmoja awajibike, tusitupe uchafu hovyo. Pengine unakuta gari ya Mbunge au Waziri au Kiongozi anaenda Dar es Salaam, mnafuatana njiani, anatupa chupa ya maji barabarani. Sisi tuonyeshe mifano mizuri ya kufuata taratibu na kanuni za usafi.
Mengi niliyoyasema haya yalisemwa na upande wa Kamati ya TAMISEMI lakini na Waheshimiwa Wabunge wengi walichangia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo hili ambalo limesemwa kwenye hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani kwamba Serikali Kuu inaingilia madaraka ya Serikali za Mitaa kwa kufanya uteuzi wa Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala, Wakuu wa Wilaya na akadiriki kusema mpaka Wakurugenzi. Pia likazungumzwa hili jambo lingine kwamba Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wanaingilia mamlaka na majukumu ya Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, ngojeni niwakumbushe na sitaki kuchukua maneno mengi, ngoja niwasomee sheria. Mwingiliano huu tunaousema unaweza ukawa na tafsiri zinazolingana na mazingira yetu, lakini naomba niwakumbushe; na bahati mbaya hii citation iko kwa Kiingereza, sasa naomba niisome:
“In relation to the exercise of powers and performance of functions of the Local Government Authorities conferred by this Act.” Hii ni sheria ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa, urban authority lakini this provision reads the same as the one in the District Authority.” Anasema: “in relation to the exercise of powers and performance of the function of the Local Government Authorities conferred by this Act.” Kifungu cha 78(a), lakini kwenye JUTA, ile sheria rasmi ni kifungu cha 87.
Mheshimiwa Naibu Spika, inasema: “The role of the Regional Commissioner and of the District Commissioner shall be to investigate the legality when questioned of actions and decisions of the Local Government Authorities within their areas of Jurisdiction and to inform the Minister (The Minister in respect of this law is the Minister responsible na TAMISEMI) or take other appropriate action as may be required. The legality of the actions, decision and the way of doing things kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa, inaweza ikahojiwa, ikatazamwa na kuangaliwa na kuchukuliwa hatua na Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya. Sio mimi, ni sheria. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, shida moja inayokuja siyo kwamba wanaingilia. Wao, why tunasema wanaingilia? Kama vitu vinaenda sawasawa, assume everything goes vizuri, vitu vinaenda sawasawa! Tukimkuta Mkuu wa Mkoa au Mkuu wa Wilaya anaingilia, tunamshangaa. Why unaingilia mamlaka halisi ya watu hawa ambao wanaweza kufanya mambo yao? Hao wamefanya kosa na watachukuliwa hatua, pindi tukiwakuta wanaingilia wakati mambo yanakwenda sawa. Pia hatuwezi kusema wasiingilie kama mambo hayaendi sawa. When things are not moving okay, hatuwezi tukasema sisi ni mamlaka ya Serikali, tumepanga, tumeamua! Mmepanga, mmezingatia sheria?
Mmezingatia kanuni? Mmezingatia taratibu? Kama mmezingatia hivyo, then there is no need of interference. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama hakuzingatia, wanasema…
MHE. PAULINE P. GEKUL: (Aliongea nje ya microphone).
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Gekul, mwache Mheshimiwa Waziri amalize kujibu hoja.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, wanasema the legality; kwa hiyo, the legality maana yake ni kwamba tuna-assume kwamba kuna kitu kimevunjwa na ndiyo maana lazima wafanye interference. Hiyo ndiyo tafsiri ya sheria na niwaombe sana, hakuna mwingiliano wowote unaofanyika na wale watakaokuwa wanaingilia, leteni taarifa tujue wameingiliaje, tutafsiri kwa mujibu wa majukumu yao tuone kama wameingilia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumesema eneo lingine ni kwamba Wakurugenzi wapatikane kwa kufanya usaili. Ni mawazo, tunayachukua kama kweli tutaweza kupata watu bora, lakini kuna shida huko kubwa! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine lililosemwa na watu wengi ni uanzishaji wa maeneo mengi ya utawala. Waheshimiwa Wabunge nchi yetu bado ni kubwa. Ukiangalia namna tunavyokwenda na kuigawagawa pengine the rationale kwenye hii hoja ni kwamba, mgawanyo ambao hauzingatii matatizo genuine kama alivyosema Mheshimiwa Keissy, kwamba unalikuta eneo lingine ni kubwa sana na hapa Kambi ya Upinzani mlisema pengine tuzuie mgawanyo tena wa nchi hii, imetosha; ili tuhakikishe tumefanya. Yako maeneo mengine bado wenzetu hawajaridhika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano. Mkoa wa Kilimanjaro, una square kilomita 14,000 plus or something; Wilaya ya Mpanda Vijijini ina square kilomita 19,000, unasemaje unazuia mgawanyo? Ukiichukua Kilimanjaro ukaijumlisha pamoja na Zanzibar, haiifikii Mpanda Vijijini. Watu wanaongezeka. Ndiyo maana sasa hivi wala hatukai kwa makabila, tunahitaji kufanya movement. Twendeni, ni lazima tutaendelea na hili, hatuwezi kufanya hivyo, lakini tutajaribu kuzingatia alichosema Mheshimiwa Keissy, tuangalie uwiano upya na vigezo vinavyotumika isije ikawa ni upendeleo unaofanyika na ambao utatuletea nchi yetu kuingia kwenye imbalance of peace. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine lililosemwa na Wabunge wengi pia kwamba barabara za Halmashauri zichukuliwe na TANROAD. Waheshimiwa Wabunge wa pande zote mbili, jambo hili haliwezi kutupeleka kwenye jibu. Ni vizuri nichukue maoni yaliyotolewa na mtu mmoja nilimsikia alisema tuanzishe Wakala wa Barabara za Vijijini, Barabara za Halmashauri. Hili amelichukua kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Naomba niisome. Katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi kifungu cha 39(a)(3) kimesema:
“Kuanzisha Wakala au Taasisi itakayosimamia kazi za ujenzi na matengenezo ya barabara za Miji na Majiji na Halmashauri ambazo ziko chini ya TAMISEMI.” Kwa hiyo, Ilani ya Uchaguzi ya CCM ililiona hili na sasa hivi wataalam wanafanyia kazi jambo hilo kutuletea namna bora ya kuweza kuanzisha huu Wakala. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni changamoto za elimu ya msingi bila malipo. Tumejitahidi sana. Serikali ilipoingia madarakani kuanzia mwezi Desemba hadi Juni kabla hatujapitisha hii bajeti, tulisema lazima tuanzishe elimu bila malipo. Msingi wa hili Waheshimiwa Wabunge, kusema ukweli ni hali ngumu waliyokuwanayo baadhi ya wazazi kutoka familia maskini katika kuwapeleka watoto wao shule. Ilikuwa siyo rahisi kwenda kumwandikisha mtoto darasa la kwanza. Mambo yaliyokuwa ni magumu! Mzazi alitakiwa kutoa hadi Sh. 20,000. (Makofi)
Kwa hiyo, dhana ya elimu ya msingi bila malipo, inazingatia uendeshaji wa shule bila ada, wala michango ya aina yoyote ya lazima kutoka kwa wazazi au walezi wa wanafunzi. Vile vile hatukusema wadau hawawajibiki! Huku mbele tukazungumzia; na jana nilimsikia rafiki yangu, shemeji yangu Mheshimiwa Cecilia Paresso, shukuru Mungu mimi nimeoa kule kwenu, najua hili jambo limewasaidia wangapi kwenda shule! Watoto wa maskini walikuwa hawaendi! Katika uandikishaji wa darasa la kwanza mwaka huu, malengo yetu tumepita kwa karibu watoto 400,000.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, ina maana hawa 400,000 wasingekwenda shule! Rwanda watoto waliokwenda darasa la kwanza mwaka huu ni 150,000; Burundi ni 120,000. Sisi 400,000, hawa walikuwa ni sawasawa na watoto wa darasa la kwanza wa nchi mbili, wasingekuwa wanakwenda shule. Tungetengeneza bomu la namna gani? Leo wanakwenda shule kwa sababu Serikali imeamua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumepanga mpango kwamba tulianza kuanzia Desemba mpaka Juni, 30 tupeleke Shilingi bilioni 18.77 kwenye shule zetu na zinaenda straight kwenye shule na hizi ni kwa ajili ya kuhakikisha kwamba watoto hawa wanasoma, hakuna michango ya uendeshaji wa shule; hakuna michango ya ada; na tumefuta ada kwa ajili ya Sekondari na tumefuta gharama za kulipia mitihani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwezi wa Kwanza mpaka mwezi wa Sita mwaka huu tutapeleka Shilingi bilioni 131. Fedha hizi ni nyingi! Unasema hatukujipanga, hata takwimu zako ulizokuwa unazisoma jana zime-tally na hizi ninazozisema mimi. Kwa hiyo, information uliyotupa ni sahihi tumeitekeleza, lakini bado tuna changamoto, lazima tuzishughulikie. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto zenyewe tuliposema shule za bweni, tulimaanisha shule za bweni zile ambazo zinajulikana Kitaifa, lakini Shule za Kata na zenyewe zilijenga mabweni na kuna watoto wanaishi pale. Je, watakula wapi chakula? Haya ni mambo tushirikiane, tunajenga Taifa letu! Hatukuwa hivi tulipo leo. Tumefika hapa kwa sababu ya kazi nzuri iliyofanywa na waliopita. Tusilaumiane, tushauriane. Tusikatishane tamaa, tusaidiane ili tuweze kutimiza matarajio ya Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kubadili kanuni za Halmashauri ili kuruhusu uwepo wa Kamati za Uwekezaji, tumeanza. Halmashauri sita tunafanya pilot study kwenye Halmashauri sita na hili limesemwa na watu wengi. Zikifanikiwa hizi, tutaanzisha Kamati za Uwekezaji kwenye kila Halmashauri, kwa sababu wengi wanapenda kukopa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili la maslahi ya Madiwani nimelisema. Ufinyu wa bajeti kwa ajili ya miradi ya maendeleo ikiwemo miradi ya barabara, maji, afya, ni kweli hatuwezi kumaliza kila kitu kwa bajeti hii. Waliopata this time, next time watapata wengine. Kwa hiyo, sisi tunatunza record na tutajitahidi kugawa rasilimali hizi kwa uwiano na vigezo sahihi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili nisiache kuzungumzia masuala ya mgawanyo wa bajeti ya ruzuku. Ile ruzuku ugawanyaji wake na vigezo vilivyoweka ilikuwa ni only population; lakini katika data analysis za kisasa, ni lazima uangalie poverty margin, uangalie ukubwa wa eneo, uangalie population. It is not only population!
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa
muda wa Mzungumzaji)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mengi kama nilivyosema yamesemwa, lakini kusema ukweli siyo rahisi kuyajibu yote. Nakushukuru sana na nawaomba sana Wabunge wote wa pande zote muunge mkono bajeti hii. Hii bajeti ndiyo maisha ya Watanzania! Nawaomba sana.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Yule atakayepinga, ananikatisha tamaa. Tuache twende tukatekeleze yale ambayo tumewaahidi wananchi na niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge wote wa pande zote mbili, muunge mkono bajeti ya TAMISEMI.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.