Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue fursa hii kukushukuru sana kwa kunipa fursa hii ndogo ili na mimi nichangie hoja hii. Kama walivyofanya wenzangu, nampongeza Waziri, Naibu wake, Katibu Mkuu na watendaji wote kwa kazi ambayo wamefanya katika Wizara, ni nzuri ndiyo maana wanapongezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Hotuba ya Waziri ukurasa wa 34 kuna hoja hii inayohusu mipaka ya kimataifa, hili ndilo jambo lililonifanya nisimame. Kwanza nimshukuru sana Waziri kwa kuliongelea jambo hili kwa sababu jambo hili limeleta sintofahamu kubwa sana kwa wananchi wangu wa Rombo eneo la Kikelelwa mpaka Nayeme. Wananchi wamewekewa nyumba zao X kwa hoja kwamba wanahamishwa kutoka mpakani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa sababu nimefuatilia jambo hili na Waziri ameniweka wazi, kwamba Serikali ya mkoa ina mipango yake ya ulinzi na usalama. Sikatai kuhusu hiyo mipango lakini linapokuja suala linalohusu ardhi ningeomba sana Serikali za Mikoa zihusishe Wizara, kwa sababu sasa hivi wananchi wa Kikelelwa, Tarakea na Nayeme wengine sasa hivi wanaanguka kwa presha, wengine wanawaza kwenda mahakamani kwa sababu ya tishio la kubomolewa nyumba zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti na Mheshimiwa Waziri wananchi hawa wameishi katika haya maeneo kabla ya uhuru na kwa sababu hiyo kuwawekea X sasa hivi ni sawa sawa na kuwapa hukumu ya kifo. Naomba ieleweke Rombo hatuna ardhi, hivi sasa hivi tunawaza namna ya kujenga hata taasisi za umma hatuna ardhi, hatuna hata maeneo ya viwanja vya michezo. Kwa hiyo jambo linalohusu ardhi katika Wilaya ya Rombo lisichukuliwe tu kwa mihemko kwa sababu ni jambo hatari na linaweza likasababisha maumivu makubwa sana kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, Mheshimiwa Waziri nashukuru na nimwombe atakapohitimisha hoja yake aseme kitu ambacho kitawapa comfort wananchi wa Nayeme, Tarakea na Kikelelwa ili waweze kupata utulivu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze jambo lingine linalohusu ardhi. Mheshimiwa Waziri pale Rombo kuna eneo la Chala. Lile eneo ni ardhi ambayo wazee wanaotoka Kata za Holili, Mahida, Chala, Mengwe, Mamsera na Kata ya Manda walipewa na Land Board zamani, wanazo risiti walikuwa wanalipia hiyo ardhi, lakini sasa hivi kuna watu wamepewa ile ardhi kinyemela. Kinachotokea wananchi hata wakiingia katika lile eneo wengine wanapigwa, wengine wanakamatwa na kadhalika. Namwomba Mheshimiwa Waziri aje Rombo tukatembelee lile eneo, aseme kitu cha kuwapa comfort wananchi wa maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwamba pamoja na uhaba wetu wa ardhi tuna Miji ya Tarakea, Mkuu pamoja na Mji wa Holili, ni miji ambayo inapanuka lakini inapanuka hovyo kwa sababu hatuna fedha kwa ajili ya kulipa fidia. Mnajua matatizo ya ardhi kwetu tunazika katika mashamba yetu humo humo, kwa hiyo ukiamua kumwondoa mtu fidia yake ni kubwa kwa sababu unafidia mpaka makaburi, sasa ile miji inadumaa. Naomba sana Mheshimiwa Waziri, Halmashauri hawana uwezo lakini wameomba awasaidie bilioni moja kwenye ile taasisi yake wapime, wananchi wapo tayari kununua hivyo viwanja na kurejesha fedha yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalize kwa kusema kuhusu migogoro hii ya ardhi. Sisi ambao hatuna ardhi tunaomba hii migogoro iishe kwa sababu tuna hakika ardhi hii ikipimwa kwa sababu na sisi ni Watanzania, vijana wetu wa Rombo nao wanaweza wakapata ardhi katika maeneo mengine. Nilikuwa katika Kamati ya Bunge iliyochunguza migogoro ya ardhi. Wako watu waliopewa mashamba makubwa kwa maana ya uwekezaji, wengine wameyakodisha. Tulienda Kilosa hapa tukakuta Mchina ana shamba anakodisha watu; tumemkuta Mwenyekiti wa Halmashauri hapo ana shamba, anakodisha watu

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.