Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya na nguvu kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa na ninachowaahidi sitawaangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuchangia Wizara hii kwanza kipekee nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya. Kwa kweli ameonesha huyu ni mtetezi wa wanyonge. Ninachowaomba Waheshimiwa Wabunge na Watanzania, Mheshimiwa Rais anafanya kazi ambayo anahitaji msaada wa Mungu pekee ili ampe ulinzi. Hili jambo si la kawaida na halikuwahi kusikika kwenye masikio ya Watanzania, naomba tumwombee sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara ya Ardhi kwa kazi nzuri wanayoifanya. Ingawa kwa upande wangu kwenye Jimbo la Kyerwa bado hajafika lakini nasikia kwingine anafanya vizuri, kwa hiyo nampongeza; na naamini huko Kyerwa atafika, kwa sababu yanayojiri huko Kyerwa anayajua na anayafahamu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee Jimbo langu la Kyerwa. Kwa kweli, tunayo matatizo ambayo ni makubwa kutokana na kwamba ile Wilaya bado ni mpya. Mheshimiwa Waziri bado hatujapata watendaji wa kutosha wa kuweza kupima maeneo ya wananchi, hasa yale maeneo ambayo ni ya Mji ule wa Rubwela na miji mingine midogo ambayo tumeitenga. Naamini wananchi wangu hawa watakapopimiwa ardhi yao tutaweza kuinua uchumi wao, wataweza kwenda kukopa. Pia maeneo haya yakipimwa naamini hata uchumi wa Taifa utainuka kwa sababu watakapopata pesa watafanya shughuli ambazo zitawapatia kipato na Serikali itapata sehemu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tuna watumishi wachache pale kwenye halmashauri yetu, kwa hiyo niombe Mheshimiwa Waziri aliangalie. Hata hivyo, si watumishi wachache tu, Idara ya Ardhi hawana hata gari, hawana hata pikipiki na jiografia ya wilaya yangu kwa kweli si nzuri. Kwa hiyo, hili tuliangalie, tusiwapeleke tu kule watumishi halafu tukawa-dump kule, hawana vitendea kazi halafu tutegemee hatimaye wanaweza wakawapimia wananchi ardhi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo Mheshimiwa Waziri naomba alisikilize ni kwamba, bado maeneo ya vijijini wananchi wanalalamika wanasema gharama za upimaji ni kubwa. Tuliangalie hili, tusije tukalinganisha na maeneo ambayo ni ya mijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo ambalo mimi nimekuwa nikishangaa sana na nimekuwa nikijiuliza maswali mengi. Mara nyingi hapa Waheshimiwa Wabunge tumekuwa tukiongelea migogoro ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji, lakini nimejiuliza jambo moja, hivi vipindi vyote ambavyo vimepita Serikali haikutenga maeneo kwa ajili ya wafugaji na wakulima? Nimejiuliza sana, lakini hatimaye katika kufuatilia kwangu nimegundua Serikali ilitenga maeneo kwa ajili ya wafugaji lakini maeneo haya kwa sababu ya viongozi ambao wamejaa tamaa, viongozi ambao hawawezi kusimamia majukumu yao maeneo haya wameyagawa, watu wengine wameingia na hatimaye tunasababisha migogoro mikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kule kwangu Kyerwa. Kuna eneo ambalo lilitengwa kwa ajili ya wafugaji mwaka 87. Eneo hili lilitangazwa kwenye Gazeti la Serikali likapewa GN Number 620, lakini eneo hilo leo watu wameingia kiholela bila kufuata utaratibu, wamegawana hovyo hovyo. Sasa unajiuliza hili eneo ambalo lilitangazwa na Serikali bila kutolewa tangazo lingine la kubadilisha matumizi, leo unaweza kuingizaje watu wengine waweze kujimilikisha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri; hili najua ugumu wake na mimi kama Mbunge nimetumwa na wananchi kwa ajili ya kuwatetea, hivyo sitanyamaza wala sitatulia katika hili, lazima tuondoe hii migogoro ambayo hatimaye inaleta uadui kati ya wakulima na wafugaji. Mheshimiwa Waziri nakuomba sana, jambo hili siwezi kulinyamazia wakati linaendelea kuleta mgogoro mkubwa kati ya wakulima na wafugaji, lazima litolewe ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo mengine kule kwangu, kwa mfano Kata ya Nkwenda, kuna Kijiji kimoja cha Nyarutuntu; maeneo ya vijiji yanachukuliwa hovyo na wanakijiji hawana msaada, wanapofuatilia hawapati msaada. Naomba Mheshimiwa Waziri aandike, kwenye Kata ya Mgwenda, Kijiji cha Nyarutuntu kuna mgogoro. Huyu bwana amekuwa akiwatumia viongozi wakubwa kwa ajili ya kuteka ile ardhi ambayo ni ya wananchi; hivi vitu ndivyo vinaleta shida kubwa kwa wananchi wetu, naomba tuyafuatilie hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kwenye Mabaraza ya Ardhi. Haya Mabaraza ya Ardhi ni mazuri lakini maeneo mengine yamekuwa kero, hawatendi haki. Kwa mfano maeneo ya vijijini hawana elimu ya kutosha ili waweze kutimiza majukumu yao. Nimwombe Mheshimiwa Waziri tusiishie mijini hebu twende na huko vijijini tuweze kuwapa elimu ili wawatendee haki Wanakyerwa na Watanzania ambao hawajatendewa haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sina mengi ya kusema lakini naomba nirudie, namwomba sana Mheshimiwa sana afike Kyerwa kama anavyofika katika maeneo mengine ili aweze kutatua migogoro ya ardhi ili yule anayestahili haki akapewe haki yake na hatimaye tuweze kukaa vizuri na wakulima na wafugaji wetu kama ndugu na kama marafiki kama ilivyo siku zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru sana na naunga mkono hoja.