Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia. Kwanza kabisa naomba nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu Subhanah Wataala ambaye ameendelea kunijalia afya njema na leo hii niweze kuzungumza machache niliyokuwa nayo, pili nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi asubuhi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema kwamba wakati nachangia bajeti ya Wizara ya Maji, nilizungumza hapa kwamba Mtume Mohammed alisema Karne ya Sita kwamba Man laa yashkur nnasa,laa yashkur Allah, kwamba mtu yeyote ambaye hashukuru binadamu wenzake kwa wema wanaofanya basi hata Mwenyezi Mungu kwa neema alizompa hawezi kumshukuru pia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya kipekee kabisa naomba nikiwa kama mzalendo wa Taifa hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kitendo kikubwa alichokifanya jana, kwa maamuzi magumu aliyoyafanya jana, kuhakikisha kwamba wale wanaotorosha madini yetu kwenda nje ya nchi wanachukuliwa hatua kwa kunyang’anywa yale madini. Tunampongeza kweli na ni kitendo cha kishujaa kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nieleze tu kwamba nchi hii kama hatuchukui maamuzi magumu tutaendelea kuwa maskini mpaka kiama. Wenzetu walioendelea duniani kupitia sekta hii ya madini, nchi ndogo kama Botswana ni kwa sababu wanachukua maamuzi magumu. Nimwombee Mwenyezi Mungu aendelee kumpa afya njema Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania achukue maamuzi magumu zaidi, Tanzania tuondokane na umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata mimi ninayezungumza hapa kama siyo kufanya maamuzi magumu nisingekuwa Mbunge leo hii, mimi nilikuwa Mwalimu, nikaandika barua kuomba likizo isiyokuwa na malipo ili niweze kugombea Jimbo la Mtwara Mjini, lakini kulikuwa na ujanja ujanja ulifanyika wakaninyima ruhusa nikamua kuacha kazi masaa 24 ili niweze kugombea Ubunge na leo hii nazungumza ni Mbunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Jimbo la Mtwara Mjini ni kwa sababu ya maamuzi magumu. Kwa hiyo, hii nchi kama tunahitaji maendeleo lazima tuwe na Viongozi wanaochukua maamuzi magumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kwa namna ya kipekee kabisa, niishukuru Wizara hii ya Ardhi, siku kadhaa zilizopita nilikuwa Mtwara nikiwa na Mheshimiwa Waziri hapa tulienda kuzindua mpango kabambe ambao unaitwa master plan kwa mara ya kwanza tangia Serikali hii ya Awamu ya Tano mpango wa kwanza kuzindua ni mpango wa master plan wa Mtwara Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kufanya kazi kubwa sana na wananchi wa Mtwara sasa kwa sababu hii master plan ambayo tumeizindua juzi ndiyo mwarobaini ya migogoro yote ya ardhi pale Manispaa ya Mtwara Mikindani. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri na namshukuru sana, Mungu ambariki aendelee kutatua migogoro mingine ambayo ipo katika maeneo mbalimbali ya nchi hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, wakati nafanya kampeni 2015 niliweza kuzungumza mambo mengi sana yanayohusu ardhi, kwa sababu Mtwara Mjini kulikuwa na changamoto nyingi sana za ardhi. Miongoni mwa mambo mengi ambayo nilikuwa nayahutubia na wananchi wangu wakanituma nije kueleza katika Bunge hili, ilikuwa ni suala la urasimishaji wa ardhi. Mheshimiwa Waziri hapa wakati anazungumza kwamba maeneo kadhaa ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hivi sasa urasimishaji unaendelea ikiwemo Jimbo la Mtwara Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Wizara hii na namshukuru Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kwa kubariki Mtwara Mjini, lakini pia kutuletea Wataalam ambao tunashirikiana nao katika suala hili la urasimishaji wa ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wito wangu kwa Madiwani wa Jimbo la Mtwara Mjini, wahamasishe wananchi wa Jimbo la Mtwara Mjini ili zoezi hili liweze kukamilika kwa wakati. Kwa namna ya kipekee kabisa nawashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Mtwara Mjini kwa kuendelea kuwa na imani na Mbunge wao na nawaambia kwamba naendelea kupambana, nitawatetea kipindi chote cha miaka yote iliyobaki na Mtwara Mjini sasa ni Mtwara kuchele kweli kweli, siyo kama kauli za kubeza za miaka ya nyuma kulivyokuwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani hizo za dhati kabisa naomba nizungumze suala moja ambalo hivi sasa pale Mtwara Mjini, nimwombe Mheshimiwa Waziri atusaidie katika hili. Mtwara Mjini kuna eneo linaitwa Mangowela, sasa hivi wamebatiza jina panaitwa Libya, hili eneo lilikuwa linamilikiwa na Wazee Nane wa Mji wa Mtwara, na hapa nina majina yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niyasome haya mbele ya Bunge lako hili Tukufu, wamiliki wa eneo hili ni Mzee Mohammed Saidi Mussa, Mussa Ismail Selemani, Ndugu Karama Akidi Ismail, Ndugu Abdallah Mfaume Mkulima, Ndugu Fatu Mchimwamba, Ndugu Abubakari Zarali Mohammed, Ndugu Musa Saidi na Ndugu Ashiraf Makuti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wazee hawa ni wazee ambao wamezaliwa miaka 1920 huko nyuma, walikuwa wanamiliki eneo hili la Mangowela, lakini hivi sasa linaitwa eneo la Libya, lakini jambo la ajabu sana ambalo lilifanyika miaka ya 2000 wameamka asubuhi wakakuta beacon zimewekwa, walivyoulizwa hizi beacon zilizowekwa katika eno hili la Libya ni za nini, wanaambiwa kuwa hili eneo limeuzwa na wamiliki wa eneo hili. Wakashangaa sana, kwamba wamiliki wa eneo hili ni watu wa aina gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, huu mgogoro ni mgogoro ambao ni mkubwa sana hivi sasa Mtwara, naipongeza Wizara hii kwamba jana niliuliza swali hapa juu ya mgogoro wa Mji Mwema na kwamba tayari wameshamaliza na fidia ile inaenda kulipwa mwisho wa mwezi huu, tunashukuru sana kwa hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri mgogoro huu wa Mji wa Libya, naomba sana wananchi hawa wamekuja Ofisini kwangu zaidi ya mara nne, wametembea maeneo yote kudai haki yao, lakini mpaka leo wanaambiwa lile eneo limeuzwa na wao wameuzwa bila wao kuelezwa. Hata hao waliouza wanasema kwamba walipewa na watu fulani, lakini hakuna documents zozote kwamba lile eneo lilikuwa ni la kwao, wamiliki wa eneo hili la Libya ni hawa wazee ambao nimewasoma hapa, kwa hiyo tunaomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja atusaidie katika hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuzungumza Mbunge mmoja kaongea hapa kuhusu shirika la NHC (Shirika la Nyumba Tanzania), kwa kweli linafanya kazi kubwa sana ya kuhakikisha wanaboresha makazi ya Watanzania, wanajenga majumba maeneo mengi, lakini nyumba hizi ambazo zinajengwa kwamba eti ni nyumba za maskini, kimsingi siyo nyumba za maskini. Mfano tu hata nikiwa Mwalimu pale Lindi, mwaka 2007, kuna nyumba zilijengwa pale Lindi, lakini zile nyumba mimi nilienda kuomba kama Mwalimu, Mwalimu ambaye nilikuwa nachukua mshahara 940,000 wakati ule, nikaambiwa kwamba zile nyumba wewe kama Mwalimu huwezi kuzinunua ni nyumba ambazo zinaanzia Sh.50,000,000/= na Sh.60,000,000/= huko na kuendelea. Sasa hizi kweli ni nyumba za bei nafuu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba Waziri ahakikishe kwamba hii NHC kweli ijenge nyumba za bei nafuu ili Watanzania wengi maskini waweze kupata hizi nyumba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze pia suala hili la kucheleweshwa hati, Mheshimiwa Waziri ana mpango mzuri sana hapa, kazungumza vizuri sana, kwamba ametoa maagizo kwa Taasisi zote, kwa Halamshauri zote, wahakikishe kwamba tunaenda kama Wabunge kukagua Masjala za Halmashari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe atoe agizo lingine kwamba ucheleweshaji wa hizi Hati unafanywa na Watendaji wa Halmashauri na watu wa ardhi wa Halmashauri na wale ambao wataendelea kukiuka agizo lako Mheshimiwa Waziri, basi hawa watu aweke hatua za kuchukuliwa mara moja ili sasa tatizo hili la kuchelewesha Hati Tanzania liweze kwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.