Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi

Hon. Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuungana na wenzangu kwa masikitiko makubwa sana kwa tukio ambalo limetokea mchana wa leo. Mimi nakaa Area ā€˜Dā€™, nimesikia bunduki, lakini baadaye nakuja kupata taarifa kwamba ni Mbunge mwenzangu ambaye amejeruhiwa. Kwa kweli inasikitisha sana, kwa siku ya leo inaleta uwoga kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kutoa shukrani kwa Kamati ya Bunge ambayo inashughulikia miundombinu ya maji kwa michango yao mizuri ambayo wametushauri kuanzia tulipoanzia michango hii kwenye Kamati. Pia nashukuru sana Maoni ya Kambi ya Upinzani ambao wameunga mkono moja kwa moja kwenye jambo hili. Nashukuru kusema kwamba kwenye masuala kama haya, kwa sababu tunajenga nchi kwa pamoja, sisi wote ni Watanzania, kwa hiyo, inabidi tuungane tuache suala la tofauti za itikadi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi tunavyoongea, tayari tuna Interim Secretariat na imeshafanya kazi kubwa sana. Hii Interim Secretariat Ofisi yake iko Kyela, nami nimeshatembelea pale. Ndani ya Watumishi; tuna Watumishi wa kutoka Malawi na Watumishi wa kutoka upande wa Tanzania. Makubaliano yaliyopo ni kwamba hata tutakapokuwa tumekamilisha hii Kamisheni, ikisharidhiwa ni kwamba Ofisi zitakuwa Kyela.

Mheshimiwa Naibu Spika, tayari tangu Sekretarieti ilipoanza, Serikali ya Malawi na Serikali ya Tanzania wanachangia hela kuendesha ile Sekretarieti ya mpito; na imefanya kazi kubwa sana. Imeshakamilisha feasibility study, imeshakamilisha detailed design na imefanya semina mbalimbali na mikutano mbalimbali na Wafadhili na kutangaza kuhusu huu Mradi wa Bonde la Songwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, tayari kuna indication kubwa kwamba Wafadhili wanasubiri tupitishe hili ili sasa mazungumzo ya mwisho yaweze kufanyika, tufanikiwe kutekeleza ule mradi. Kwa hiyo, suala kama hili Waheshimiwa Wabunge kwa kuliunga mkono, sisi kwa kweli kama Watanzania na kama Wabunge na Wizara ya Maji tunafarijika zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia juzi kulikuwa na Mkutano wa SADC, nami Mheshimiwa Waziri alinituma niende kule. Katika miradi miwili ambayo imepita; imepitishwa na SADC, ni pamoja na huu Mradi wa Songwe. Umepitishwa kwa sababu una components tatu ndani yake kama alivyokuwa amezungumza Mheshimiwa Mwakyembe. Tutazalisha umeme pale, tutatengeneza skimu za umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna hekta za mwanzo 6,200; na kati ya hekta hizo, hekta 3,150 ziko upande wa Tanzania na hekta 3,050 ziko upande wa Malawi. Kwa hiyo, wananchi wa maeneo ya Tanzania na huku watafaidika na umeme na bado watafaidika na kilimo cha umwagiliaji, kilimo chenye uhakika.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia maji yatachakatwa majisafi na salama. Kwa hiyo, sehemu ya maji yatakwenda upande wa Tanzania na sehemu ya maji watatumia watu wa Malawi. Kwa hiyo, sioni katika mpangilio kama huo ambao tuna-share umeme, tuna-share huduma ya maji safi na salama na tuna-share kilimo cha umwagiliaji, jamani undugu utazidi hapo. Unatarajia kuwe na ugomvi kweli hapo? Hata matatizo mengine yaliyopo kwenye lile Ziwa Nyasa, tuna imani kabisa kwamba utatuzi wake sasa utakuwa rahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge katika michango yao wamezungumzia suala la ushirikishaji wa jamii. Tangu mwanzo hii Interim Secretariat ilivyoanza, imeshirikisha wananchi kutoka ngazi za Vitongoji, imekuja kwenye Vijiji, mpaka Kata, mpaka Wilaya. Wameshirikishwa na minutes zipo na taarifa hizi tumezitoa kwenye Kamati. Kwa hiyo, kila mwananchi yuko aware na suala hili na wanalisubiri kwa hamu kabisa kwamba Kamisheni hii ipitishwe na Bunge letu ili ianze kufanya kazi, wao wanasubiri kupata maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, hebu tujaribu kuiangalia mipaka kwa wale ambao wanaishi kwenye mipaka. Kama maendeleo yakiwa upande mmoja kwingine kukawa hakuna maendeleo, maisha yanakuwaje katika hilo eneo? Kwa maana ya hii Kamisheni kwamba maendeleo yatakayopatikana yatakuwa shared upande wa Tanzania na upande wa Malawi. Kwa hiyo, tutazidi kuimarisha undugu wetu na ushirikiano utakuwa mkubwa. Migogoro mingine midogo midogo wakati mwingine unaitatua automatically kwa kuweka huo ushirikiano.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, tunawashukuru sana na tunawaomba kwa kupitia kwenye michango ambayo wengi mlipata nafasi ya kuchangia, wengi mnaridhia na hili. Kwa hiyo, mwisho kabisa tunawaomba mridhie ili hatua nyingine ziweze kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo, namalizia kwa kushukuru tena, ahsanteni sana.