Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Amani na Usalama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Amani na Usalama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Nami kwanza niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kumwombea mwenzetu uponyaji wa haraka kwa haya yaliyompata.

Mheshimiwa Naibu Spika, Azimio hili la leo ni muhimu sana kwa nchi yetu, hata kwa nchi zinazotuzunguka. Labda ningeanzia pale kwenye Azimio, nafikiri kunahitaji masahihisho kidogo ya jina la Wilaya. Kuna Wilaya pale imetajwa, Mbeya Vijijini. Hatuna Wilaya ya Mbeya Vijijini, ila tuna Wilaya ya Mbeya. Kwa hiyo, labda kwa ajili ya kumbukumbu sahihi za Bunge, ingebadilishwa na kusahihishwa kuwa Wilaya ya Mbeya.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hivyo, niende zaidi kwenye maoni. Niungane kwanza na maoni ya Kamati, walivyosisitiza kuwa katika mkataba huu labda ndiyo wakati muafaka wa Serikali kuangalia ni namna gani huu mkataba vile vile unaweza kutusaidia katika kutatua tatizo la mgogoro wa mpaka ulioko katika Ziwa Nyasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri hiki kinaweza kuwa ni chanzo kizuri sana na Ziwa Nyasa linatokana na Mto songwe na Mto Songwe kwa kiasi kikubwa unatoka kwetu, kwa hiyo, nafikiri hiyo inaweza kuwa ni chanzo kizuri ni namna gani tukaondoa hili tatizo la mgogoro wa Ziwa Nyasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili katika maoni ya Kamati, vile vile waligusia elimu kwa wananchi. Nafikiri hili ni jambo muhimu sana kuangalia ni namna gani wananchi wakashirikishwa kikamilifu na kuwapa elimu ya namna ya kuhifadhi haya mabonde yetu na hivi vyanzo vya mito.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia tunapozungumzia bonde la Mto Songwe, kuna Mto Songwe ambao unakwenda Ziwa Nyasa na kwa kweli kilichonifurahisha hapa ni namna gani yatajengwa yale mabwawa matatu na faida za yale mabwawa matatu ambayo yatazalisha umeme takriban Megawatt 182.2. Pamoja na hilo, hayo maji yatatumika kwa ajili ya umwagiliaji na vile vile kwa ajili ya matumizi ya majumbani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia yale maeneo ya kwetu hasa katika Wilaya yangu, pamoja na kuwa na mito mingi ambayo ndiyo vyanzo vya mito hii inayokwenda Songwe na ile Songwe inayokwenda Rukwa, vile vile ndiyo chanzo cha Mto Ruaha, lakini yale maji kwa kiasi kukubwa wananchi hawayafaidi. Kwa hiyo, kwa mtazamo huu uliopo kwenye mkataba huu nina imani ya kwamba Serikali itaangalia ni namna gani wananchi nao wafaidike na haya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapoliangalia bonde la Mto Songwe ambao unaelekeza maji yake kwenye Ziwa Nyasa, napendekeza kuwa Serikali vile vile iangalie bonde la Rukwa ambalo nalo lina Mto Songwe ambao unapeleka maji Ziwa Rukwa. Hili ni bonde muhimu sana na kwa kiasi kikubwa Ziwa Rukwa karibu linaanza kupotea kwa ajili ya udongo na mmomonyoko ambao unasongwa na mto Songwe kupelekwa Ziwa Rukwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa katika huu mtazamo ambao tunauona hapa leo, nafikiri itakuwa ni jambo jema sana, tuanze sasa hivi kuangalia kuchukua hatua za haraka, ili haya yanayofanyika kwenye Bonde la Mto Songwe unaopeleka maji Ziwa Nyasa, vile vile iende na kwenye Mto Songwe unaopeleka maji Ziwa Rukwa. Tufanye hivyo hivyo, kwa vyanzo vingine vya mito vilivyoko kwenye milima ya Uporoto na Kitulo ambao maji yake ndiyo chanzo cha Mto Kiwira ambao unapeleka maji vile vile Ziwa Nyasa na vile vile ndiyo chanzo cha Mto Ruaha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hivi vyanzo vyote ni muhimu sana. Kwa hiyo, elimu itakuwa muhimu sana kwa wananchi, lakini tufanye mikakati ya makusudi, ni namna gani tuwasaidie hawa wananchi ili waone manufaa vile vile, nao wahusike katika kuhifadhi hivi vyanzo vya hii mito.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)