Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Amani na Usalama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Amani na Usalama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nami napenda kuchangia hoja hii iliyopo mbele yetu. Kwanza naipongeza Serikali kwa kuleta hili Azimio hapa Bungeni kwa sababu hili suala la mradi wa Bonde la Mto Songwe ni la muda mrefu lakini sasa naona linafikia tamati na inasaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda kupongeza Serikali kuwa sasa hivi pia imeongeza wigo wa zile Wilaya ambazo zitaguswa na mradi huu au programu hii kutoka zile mbili za mwanzo iliyokuwa Ileje na Kyela, sasa mpaka Momba, Mbozi na Mbeya Vijijini, kwa hiyo hii vilevile italeta manufaa zaidi kwa wananchi wa sehemu hizo za Songwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda vilevile kuzungumzia kuwa kwa kweli hii programu imekuja wakati mzuri, kwa sababu kwa muda mrefu sana Mto Songwe umekuwa ukisumbua sana pale ambapo kunakuwa na mafuriko ambayo yanaletea kingo zake kuleta madhara mengi sana ya kimazingira pia kuharibu miundombinu ya eneo husika na kwa kudhibiti sasa hivi itatusaidia sana kuhakikisha kuwa Mto Songwe unadhibitiwa lakini vilevile unatumika vizuri zaidi kiuchumi kulinda mazingira, vilevile kuboresha maisha ya wananchi wa maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na maendeleo hayo inaonekana kuwa programu hii pia itasababisha ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya barabara, vituo vya afya, elimu na masuala ya utalii. Napenda kutoa rai kwa Serikali kuwa wakati wanapofikiria kufanya miradi hii basi wazingatie miradi au mipango ya miradi iliyoko pale kwenye eneo hilo ili tusiwe tuna miradi ambayo inakwenda sambamba wakati kuna haja ya kumalizia ile iliyopo ili tusilete ile duplication au kuzidisha ukiritimba kwenye shughuli za maendeleo za eneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda sana kutoa rai kwa Serikali juu ya kuhusisha wadau muhimu. Kwa sababu hata hapo nyuma ambapo mradi ulikuwa umefikiriwa kufanywa, kuna wananchi mpaka leo walikuwa wameambiwa kuwa maeneo yao wasiyatumie kwa sababu mradi utapita, kama mnavyojua ni miaka mingi tangu wazo liwekwe na wamekuwa kwenye hali ya sintofahamu wakisubiri nini kinaendelea. Kwa hiyo, safari hii tutakapomaliza kuridhia na itakapoanza kufanya hii programu basi wananchi wafahamishwe, Halmashauri husika zihusishwe moja kwa moja ili sasa wananchi watambue ni nini kitakuja kuendelea katika maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia masuala ya kujifunza kutoka kwenye matokeo ya miradi mingine ya haya mabonde, tumesikia hapa kuwa kulikuwa kuna mabonde kama tisa nchini ambayo yamekuwa na miradi lakini yamekuwa na ufanisi ambao wakati mwingine sio mzuri sana. Sasa hii ingekuwa ni fursa nzuri kwa mradi huu na wenyewe kuangalia jinsi gani watajifunza tusiingie tena katika matatizo yale ambayo yaliingiwa katika miradi ya huko nyuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, Ruaha tunajua jinsi ambavyo shughuli za kibinadamu zimeathiri sana mto ule na mpaka sasa hivi unaathirika hata kina chake na kwa hiyo inaleta shida. Sasa na huu mradi nao ukaangaliwe katika mtazamo huo na zile Wizara zote ambazo zinahusika katika mradi huu basi ziwe na ushirikiano wa karibu ili kila mmoja asimame katika nafasi yake kuhakikisha kuwa mradi huu unakuwa wa manufaa kuliko kuwa wa hasara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala amelizungumzia Mheshimiwa Lissu pale ningependa kusema pamoja na kuwa amelizungumza kwa njia ambayo haikufurahisha basi likaangaliwe, ingawa mimi kwa uelewa wangu mdogo ingawa siyo Mwanasheria, huu ni mradi ambao unahusisha rasilimali zinazogusa nchi mbili. Kwa hiyo, naamini kutakuwa na makubaliano mazuri ya jinsi gani ya kusuluhisha usimamizi wake na sikuona kama kulikuwa kuna sababu ya kutoa maneno makali ambayo kwa kweli hayajengi.

Mwisho kabisa nataka kupongeza sana na kuomba Waheshimiwa Wabunge turidhie Azimio hili kwa sababu linakwenda kujenga na kuboresha miundombinu na rasilimali hii nzuri itatumika vizuri zaidi kuliko jinsi ilivyo sasa hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.