Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuijalia amani nchi yetu na kutuwezesha Wabunge wote kuwepo hapa kushiriki katika Mkutano huu muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Rais, Champion wa Maji kwa kuendelea kuniamini na kuamini wafanyakazi wa Wizara ya Maji ili tuweze kutatua tatizo la maji kwa wananchi wa Tanzania. Namshukuru Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu, Mheshimiwa Rais alimteua Mama na suala la maji ni la mama, kwa hiyo anatusimamia vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuendelea kusimamia vizuri shughuli za Bunge na tunaendelea vizuri kwa amani kabisa bila fujo ya aina yoyote. Namshukuru Mheshimiwa Spika, nawe Mheshimiwa Naibu Spika na leo ndio umekalia kiti hicho kwa jinsi mnavyoliongoza Bunge kwa weledi mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa ushirikiano wenu, kwa miongozo yenu na kwa jinsi mnavyotuombea, lakini jinsi ambavyo mnaendelea kushirikiana nasi ili azma hii ya kuondoa tatizo la maji katika nchi yetu liweze kufikiwa bila tatizo lolote.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nami niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kutoa pole za dhati kwa wananchi wote nchini hususan wananchi wa Arusha, kwa msiba mkubwa wa ajali ya gari uliogharimu maisha ya wanafunzi, Walimu, dereva na shule, msiba uliotutokea mwezi huu, msiba mgumu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesikitika sana kwa sababu barabara ile nimeisimamia mwenyewe kutoka Makuyuni mpaka Ngorongoro. Tunaomba roho za vijana hawa na hawa watu wazima wote Mungu aziweke mahali pema peponi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Lwenge, amenipa ushirikiano mkubwa sana, ameniongoza ndiyo maana hata nimeweza kufahamu mambo mengi kwa muda mfupi. Namshukuru sana Mheshimiwa Lwenge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Katavi kwa ushirikiano wao mkubwa wanaonipa mimi Mbunge wao, unaosaidia kufanikisha shughuli mbalimbali za maendeleo katika Jimbo letu, naendelea kuwaahidi kwamba nitawatumikia kwa kadiri Mwenyezi Mungu atakavyonijalia na kwa nguvu zangu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile naishukuru familia yangu sana kwa jinsi inavyonishauri na jinsi inavyonipa ushirikiano ikiongozwa na mke wangu ambaye ni Mwalimu Bora Jeremiah Ulaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda kuwa ni mdogo, nianze kuunga mkono hoja au shughuli yetu hii ya leo na niombe Waheshimiwa Wabunge mpitishe ili tukafanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepokea michango mingi sana kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge, michango ambayo kwa kweli inatutetea ili tuweze kuhakikisha kwamba tunatimiza kuwapatia wananchi wa Tanzania majisafi na salama lakini pia tuweze kuboresha kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaanza mchango wangu kwa kilimo cha umwagiliaji. Nchi yetu mwaka 1990 ilifanyika study ambayo ilibaini kwamba tuna hekta milioni 29.4 zinazofaa kwa kilimo cha umwagiliaji, lakini ambazo zimeendelezwa ni hekta 461,000. Baada ya kuteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji, nashukuru maeneo niliyofanya ziara; nimekwenda kuona jinsi gani hili eneo dogo ambalo limeendelezwa jinsi linavyofanya kazi na nimebaini upungufu uliopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimetembelea eneo la Mang’ola, nimekwenda kuona kilimo pale Wilaya ya Karatu, wanalima mara tatu. Hekta moja inatoa kuanzia tani tano mpaka tani kumi lakini hekta moja hiyo hiyo inalimwa mara tatu. Ni maeneo machache sana ambayo yameshafikia hatua hiyo ya kilimo kwamba hekta moja inaweza ikalimwa mara tatu. Maeneo mengi yanalimwa mara moja na ni kipindi cha mvua tu; kipindi cha kiangazi hatuwezi kulima kwa sababu hakuna maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana Serikali kwa sasa imeweka Mhandisi Mshauri ambaye anapitia maeneo yote ili kubaini upungufu uliopo ni kwa nini hatuwezi kulima mara tatu ili tuweze kuondokana na tatizo la njaa katika nchi yetu. Upungufu huo ukishapatikana utaainishwa na malengo yetu ya kuhakikisha kwamba tunaandaa hekta nyingine millioni moja katika huu muda wa miaka mitano, nina hakika kwamba yatafikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo letu ni kuhakikisha tunalima mara mbili hadi mara tatu, kwa sababu hata hizo hekta chache ambazo nazo hazitumiwi kwa efficiency inayotakiwa, lakini bado zina uwezo wa kuchangia chakula kwa zaidi ya asilimia 25.

Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo cha umwagiliaji ndiyo uti wa mgongo wetu na Ilani ya Chama cha Mapinduzi imeelekeza kwamba nchi yetu inakuwa ya viwanda na viwanda hivyo vitatumia rasilimali ya kutoka mashambani ili tuweze kunyanyua uchumi wa wananchi wetu twende kwenye uchumi wa kati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tutahakikisha kawamba kilimo hiki cha umwagiliaji tunakisimamia ipasavyo. Kwa sababu Waheshimiwa Wabunge mlipitisha tume, katika huu muda mfupi ambao nimekaa nao, nimebaini upungufu uliopo. Upungufu uliopo, ni kweli kama mnavyolalamika Waheshimiwa Wabunge miradi mingi ambayo tulipata hela za wafadhili haijajengwa katika ile hali ambayo tulikuwa tunaitarajia. Kila ukiuliza, ukienda kwenye Halmashauri, Halmashauri wanakwambia ni matatizo ya Tume; ukiongea na watu wa Tume, wanakwambia ni matatizo ya Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeongea na Waziri wangu kwamba hiyo miradi iliyokuwa inaendelea iendelee, lakini miradi mipya yote itakayokuja, tunataka tuone mtu mmoja anaitekeleza na sio mwingine, itakuwa ni Tume ya Umwagiliaji, ili kama kuna upungufu katika ile tume, Waheshimiwa Wabunge tuweze kuurekebisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepata michango mingi, Mheshimiwa Mwalongo, Mbunge wa Njombe Mjini ameongea kitu cha msingi sana, kwamba Halmashauri yake ina matatizo ya Wahandisi, ina matatizo ya wataalam wa manunuzi. Ni kweli, lakini nashukuru bajeti ya mwaka 2016, mliagiza Wizara ya Maji na umwagiliaji kwamba mnataka tuunde Wakala wa Maji Vijijini. Mheshimiwa Waziri atalielezea vizuri, niwahakikishie kwamba tumeshaanza. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, hata mimi mwenyewe baada ya kuteuliwa katika Wizara ya Maji na Umwagiliaji, kwa sababu nimetoka kwenye Wakala wa TANROAD niliona ili tuweze kwenda hakuna namna nyingine, ni lazima tuunde wakala ujitegemee, ufanye kazi kama ambavyo TANROAD imekuwa inafanya, ufanye kazi kama ambavyo REA inafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mwalongo tatizo hilo alilonalo la wataalam wa manunuzi litakwisha baada ya sisi kuwa na Wakala wa Maji Vijijini. TANROAD imefanikiwa kwa sababu wataalam wa manunuzi ndani ya TANROAD ni Wahandisi hao hao wanaojenga barabara, ndiyo maana mambo yanakwenda vizuri; tunaelekea huko Waheshimiwa Wabunge. Sasa hivi inaandaliwa na tutakapoileta hapa, tutawaomba Waheshimiwa muipitie, mtushauri na muipitishe ili tuanze utekelezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Musukuma katika mchango wake, nilikuwa nafikiri nami ataniuliza what is your weakness? Alisema kwamba miradi hii, bajeti hii hatuwezi kuitekeleza kwa mwaka mmoja.

Waheshimiwa Wabunge tumejipa miaka mitano, tumeanza na bajeti hii tumeitendea haki, tumeingia mikataba, tutatekeleza. Hebu tupimeni baada ya miaka mitano mtaona tutafanya nini? Huu mwaka mmoja tumejitahidi, tumeelewa tunatakiwa kufanya nini. Kwa hiyo, tupeni muda tuifanyie kazi. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wako Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia uchimbaji wa visima vya Kimbiji na Mpera. Waheshimiwa Wabunge tayari visima 17 vimeshakamilika na niwaambie tu kwamba visima vitatu bado, lakini vinakamilika mwezi Juni, 2017 maana yake ni mwezi ujao. Visima hivi vikikamilika, visima vya maeneo ya Mpera vitahudumia wakazi wa maeneo ya Gongolamboto, Chanika, Luzando, Pugu, Mpera, Chamazi, Kidunda, Ukonga, Kinyerezi na Uwanja wa Ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, visima vya maeneo ya Kimbiji vitahudumia wakazi wa maeneo ya Temeke, Kisarawe, kibada, Kimbiji, Kigamboni, Tuangoma, Mkuranga, Kongowe, Mbagala, Kurasini, Mtoni, Tandika, Keko na Chang’ombe. Serikali inaendelea kutafuta fedha ili tuweze kuweka miundombinu ya usambazaji.

Waheshimiwa Wabunge, naomba mtuamini, tunaifanya hii kazi ili tuhakikishe wananchi wote wa Dar es Salaam na Pwani wanakuwa na majisafi na salama kwa ajili ya matumizi ya binadamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Ignas Malocha, Mbunge wa Kwela. Amesema kwamba tumekuwa tukiomba pesa mfululizo kwa miaka mitano, hatujawahi kupewa. Tatizo ni nini? Anaelekeza kwenye miradi ya Maleza, Izia na Mfia. Mheshimiwa tutaweka fedha, tumeanza. Kama nilivyosema, utekelezaji wetu unakwenda miaka mitano, nimhakikishie wananchi wake watayaona sasa matokeo kwamba tunatekeleza maeneo yote haya aliyoyahitaji yakiwemo pamoja na maeneo ya umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Pudenciana Kikwembe amesema mradi wa umwagiliaji wa Mwamapuri kwamba haujatengewa fedha katika bajeti ya mwaka huu; anaomba mradi huo utafutiwe fedha. Skimu ya umwagiliaji ya Mwamapuri ipo Halmashauri ya Mpimbwe, Wilaya ya Mlele Mkoa wa Katavi. Skimu hii ina zaidi ya hekta 13,000 zinazofaa kwa umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwambie Mheshimiwa Pudenciana Kikwembe, tayari upembuzi yakinifu umeshakamilika na tayari tumeshapata gharama, tunahitaji shilingi billioni 15 ili tuweze kuikamilisha hiyo skimu ikiwa ni pamoja na kujenga Bwawa la Ilalangulu ambalo litatunza maji ili tuhakikishe kwamba skimu hiyo inafanya kazi mwaka mzima isifanye kazi wakati wa mvua tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Augustino Manyanda Masele ameuliza, katika nyakati hizi mbaya za mabadiliko ya tabianchi, licha ya kwamba sasa maeneo yetu bado ya misitu na miti kiasi, lakini suala la uharibifu wa mazingira litasababisha ukame utakaosababisha uhaba wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Mpina ameeleza vizuri sana nini kinafanyika, sheria tunazo, lakini kikubwa Mheshimiwa Masele sisi ni Madiwani, lazima tukae na wananchi wetu, tuongee nao, tubadilishe tabia sisi wenyewe. Hatuwezi kuishi kwa sheria tu, lazima tuwe na tabia ya kufahamishana tuelewe kwamba misitu ni uhai na uhai ule siyo wa misitu wala siyo wa wanyama tu, ni pamoja na sisi binadamu. Tukielimishana, basi suala hili la mabadiliko ya tabianchi halitakuwepo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, Wabunge wengi wamelalamika, miradi mingi ya maji tumetekeleza, lakini haifanyi kazi. Ukienda kuangalia, pamoja na matatizo yaliyokuwepo kwamba labda imejengwa vibaya, labda usanifu ulikuwa mbaya, lakini maeneo mengi ni kwamba vile vyanzo vilivyokuwa vimetarajiwa vimekauka. Sasa kama vimekauka, maji ya kuingiza kwenye bomba utayapata wapi? Haiwezekani. Tatizo hili sisi wenyewe, ndugu zangu tuhakikishe kwamba tunasimamia, tunaongea na wananchi wetu kuhakikisha kwamba tunadhibiti uharibifu wa misitu kwa sababu misitu ni uhai.

Mheshimiwa Naibu Spika, wapo Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia suala la kwamba mradi kutumia hela nyingi. Ukienda kuuliza, unaambiwa hii design iliharibiwa na Consultant. Mikataba iko wazi! Iko design liability ya Consultant. Kama Consultant ameharibu na ikathibitishwa kwamba ameharibu, lazima anailipia. Hizo fedha za kujenga huo mradi tutazipata kutoka kwenye insurance yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, iko michango mingi sana ya Waheshimiwa Wabunge ambayo hatuwezi kumaliza kuijibu yote, lakini tutahakikisha kwamba kwa muda mfupi michango yote hii tutaiandika na kuhakikisha kwamba tunawapatia Waheshimiwa Wabunge kabla ya kumaliza hili Bunge ili kila mtu awe na nakala na aone mchango wake na majibu ambayo tumeyapata.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Anna Lupembe, Mbunge wa Viti Maalum, maji yasiyotibiwa, malengo yetu na ndiyo Sera yetu kuhakikisha kwamba maji yote ya matumizi ya binadamu yanatibiwa ili mtu aweze kunywa maji yaliyo safi na salama. Concept hii tumeiona, Waheshimiwa Wabunge mmechangia, tukinywa maji yaliyo safi na salama tunapunguza hata kwenda hospitali na gharama za kununua madawa zitapungua. Hilo ndilo lengo letu. Sisi Wizara ya Maji hatupendi tuwe sababu ya kumaliza fedha za nchi hii kwa Serikali kununua madawa mengi kwa ajili ya matumizi ya binadamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Kapufi amezungumzia maji ya Ikorongo. Tayari tumeshasaini mkataba mmoja na wa pili utasainiwa ili tuhakikishe kwamba tunaongeza kiwango cha maji kufikia lita milioni
10.2 zinazohitajika katika Mkoa wa Katavi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Munde, Mbunge wa Tabora, tunakushukuru sana kwa pongezi. Tumesaini mikataba; mkataba ule ni wa zaidi ya shilingi bilioni 600, tunasimamia utekelezaji. Tumejipanga kuhakikisha kwamba unakamilika katika muda uliotarajiwa ili tuhakikishe tunamaliza yale matatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa mama yangu Mheshimiwa Sitta amelalamikia kuhusu mradi tunaotoa maji Malagarasi kuleta Tabora kwamba utachukua muda mrefu. Tutahakikisha kwamba katika huo muda tunaosubiri ili tuweze kupata fedha kujenga huo mradi ambao utachukua miaka mingi, tutahakikisha kwamba tunafanya hatua za dharura ili wananchi wa Kaliua, Urambo waweze kupata maji yaliyo safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri hapa nimeshapigiwa kengele tayari, nimalizie kwa kuunga mkono hoja, lakini nawaomba Waheshimiwa Wabunge, kila bajeti inapokamilika, tunawapatia vitabu. Katika mizunguko yangu ambayo nimekwenda huko kwenye Halmashauri, unakutana na Mkurugenzi anasema yeye haelewi kama ana bajeti ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji. Kabisa, kabisa mama yangu. nimeyaona haya na siyo Halmashauri moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Waheshimiwa Wabunge, baada ya leo, kesho mpigie Mkurugenzi wako, basi msomee hata kama hukumpa kitabu, kwamba Wizara ya Maji na Umwagiliaji una shilingi kadhaa ili waweze kujipanga. Zipo, lakini hawaangalii.