Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nichukue nafasi hii kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu pamoja na timu yao kwa kazi nzuri inayofanyika katika kuboresha huduma za maji hasa katika Halmashauri nyingine kasoro Halmashauri ya Nyasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa uchungu nina masikitiko makubwa juu ya mwenendo wa miradi ya maji katika Wilaya yangu. Nakumbushia barua yangu kwako Mheshimiwa Waziri juu ya tatizo la maji, katika hotuba yako Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 133, Ziwa Nyasa linaongoza kwa kuwa na ujazo mkubwa wa maji. Mwaka 2015/2016 milimita 1,359.78 na mwaka 2014/2015 milimita 1208.92. Ukurasa 135 Ruhuhu ni wa pili kwa wingi wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Wizara inatoa maji toka Mwanza kupeleka Shinyanga/Tabora zaidi ya kilometa 150, lakini wananchi wa Nyasa wana umbali chini ya kilometa 1- 3 kutoka Ziwa Nyasa na hawapati maji salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la Kingirikiti kulikuwa na mradi mkubwa wa maji uliotekelezwa toka tukiwa Wilaya ya Mbinga, zaidi ya shilingi milioni 600 lakini mpaka leo hakuna maji. Nilitoa fedha zangu shilingi milioni 1.5 kusaidia upimaji wa maeneo ya kuboresha upatikanaji wa maji katika Kata ya Tingi, mpaka leo hakuna chochote kinachoendelea. Kituo cha Afya cha Lupalaba kina hali mbaya, niliomba hata ifanyike kazi ya kunusuru kata hiyo mpaka leo hakuna kitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kata ya Mbaha hasa kijiji cha Ndumbi hamna maji, hali ni mbaya. Mji wa MbambaBay Makao Makuu ya Wilaya hakuna maji, lakini maji ya Ziwa Nyasa yapo umbali wa mita 30 tu kutoka makazi na shughuli za watu, lakini bado watu hao wanakosa maji salama. Mheshimiwa Waziri, nadhani kuna tatizo Mhandisi waMaji wa Wilaya yangu nadhani anahitaji kusaidiwa, uwezo ni mdogo, yupo kwenye comfort sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kabrasha sijaona mradi specific kuhusu Wilaya ya Nyasa. Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Naibu Katibu Mkuu, wote hawa ni wanangu kule Rukwa, Katibu Mkuu pia ni mwanangu kule Wizara ya Elimu, mbona hamnihurumii? Leo nimejipanga, kesho kusipoeleweka nitashika shilingi kiaina.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitengewe fedha kisha nipewe wataalam wa kunisaidia, suala la maji halijapata majibu kabisa kwenye Jimbo langu, Mbinga tupewe fedha mpaka waseme fedha za mradi wa Kingirikiti wamepeleka wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitashika kifungu.