Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia hotuba ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya fedha za Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa mwaka wa fedha 2017/2018.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu miradi ya maji ya Benki ya Dunia katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru miradi iliyokamilika ni minne, miradi mitatu inasuasua kwa kuchelewa fedha na mitatu mingine haijaanza kabisa kutokana na matatizo mbalimbali. Hivyo, tunaomba miradi ile mitatu inayoendelea ya Mbesa, Mtina na Matemanga ipelekewe fedha ili ikamilike kwa sababu ni muda mrefu wakandarasi wanasuasua kukamilisha miradi hiyo. Vilevile miradi mitatu ya Mchoteka, Matemanga na Namasakata ianze kwa vile wananchi walishachangia sehemu ya fedha kama masharti ya miradi ile iliyohitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri ya Tunduru vyanzo vya maji ni vingi sana lakini miundombinu ni michache sana. Maji yanapatikana ndani ya mita 100 za urefu ardhini, hivyo tunahitaji gari la kuchimbia visima vifupi na virefu ili kupunguza gharama za upatikanaji wa maji. Nadhani kama Halmashauri yetu ingekuwa na gari la kuchimbia visima tungeweza kusaidia kupata maji kwa wepesi zaidi kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi mingi ya maji inayotumia generator wananchi wameshindwa kuendesha hivyo Serikali iangalie upya katika miradi ya jamii kuweka solar badala ya kutumia generator ambazo wananchi wameshindwa kununua diesel kuendesha mashine za maji. Hivyo, ninaomba miradi iliyobaki ni vema mashine na pump zinunuliwe zote zinazotumia solar badala ya generator ya diesel.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu miradi ya umwagiliaji Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru imebahatika kuwa na maeneo yanayofaa kwa kilimo cha umwagiliaji na maeneo kadhaa tayari yana miradi ya umwagiliaji, lakini tatizo wataalamu wetu wanatuangusha sana, miradi ile inatumika wakati wa kifuku tu, kiangazi miradi hii haifanyi kazi kutokana na upungufu mkubwa wa maji katika mito na mabwawa yanayotumika, ubovu wa miundombinu ya mifereji kutokana na mapungufu makubwa ya kitaalamu. Miradi hii inatumia fedha nyingi sana lakini haifanyi kazi
iliyokusudiwa. Ninaomba wataalam wetu kutumia utalaam wao kwa uangalifu sana ili kufanya miradi hiyo iwe endelevu, miradi ya umwagiliaji hailingani na kiasi cha pesa kinachotumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Tunduru bado tuna maeneo mengi yanayofaa kwa kilimo cha umwagiliaji ni vema basi tukafikiria kutumia maji ya kuchimba visima virefu na vifupi na kutumia mabomba ya kawaida badala ya kutumia mabanio ya kujenga mifereji inayotegemea maji ya mito au mabwawa ambayo kwa sasa yanakosa maji kipindi cha kiangazi, hivyo kutokuwa na uzalishaji kwa sababu maji yanapungua sana hayawezi kupanda kwenye mifereji na mitaro iliyojengwa na mifereji mingi inabomolewa wakati wa kipupwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa maji ndiyo kila kitu katika maisha ya binadamu, basi ni vema tozo ya maji kwenye mafuta ingeweza kuongezwa kutoka 100 ili kuongeza fedha za miradi ya maji vijijini na ni vema ukaanzishwa Mfuko wa Maji Vijijini ili kuharakisha maendeleo ya miradi ya maji vijijini.