Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii kuchangia katika Wizara hii muhimu ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kupeleka fedha za maendeleo katika miradi mbalimbali na taasisi zake kwa asilimia 34, ni hatua nzuri ukizingatia zaidi ya miaka miwili kabla ya Serikali ya Awamu ya Tano kuingia fedha za maendeleo hazikuwa zikipelekwa, lakini sasa zimeanza kupelekwa, ni hatua ya kupongezwa badala ya kubeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo, sasa nianze kutoa mchango wangu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Fedha za Usimamizi na Ufuatiliaji wa Miradi ya Maendeleo. Serikali imetoa Mwongozo wa kusitisha miradi yote ya maji kutosimamiwa na Wakandarasi Washauri kwa kupunguza matumizi na badala yake kazi hiyo ya usimamizi wa utekelezaji wa miradi ifanywe na wataalam wa mkoa na halmashauri husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na nia hiyo nzuri ya kubana matumizi, lakini Serikali imesahau kupeleka fedha katika halmashauri husika za usimamizi na ufuatiliaji wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya maji na mingine na kusababisha miradi mingi kutekelezwa chini ya kiwango na kuchukua muda mrefu kukamilika kwa kukosa usimamizi wa karibu wa kitaalam kwa watumishi wenye weledi wa kazi hii. Naomba kushauri Serikali yangu kupeleka fedha za usimamizi na ufuatiliaji kuwezesha halmashauri na mikoa kusimamia miradi hii ili kupata thamani halisi ya fedha ya miradi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Chalinze III. Mradi wa Chalinze III ni wa muda mrefu sana na mpaka sasa haujakamilika. Katika mradi huu na sisi watu wa Morogoro Kusini Mashariki ni wanufaika wa mradi wa Chalinze III katika Vijiji vya Kidugalo, Chiwata, Maseye, Kinonko, Ngerengere, Sinyaulime na Lubungo, pamoja na Kambi zetu za Jeshi za Kinonko, Kizuka na Sangasanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu ya usambazaji maji na matanki ya kuhifadhia maji imejengwa zaidi ya miaka tisa iliyopita kiasi kwamba mingine imeanza kuchakaa, lakini maji hayajawahi kutoka hata siku moja. Nataka kupata kauli ya Serikali kuwa ni lini watu wa jimbo langu katika vijiji hivi watapata maji?

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, Mkandarasi yupo site kufuatilia na kukagua miundombinu ya maji na kutaka kujenga kidaka maji (intake) ya kupokea maji kutoka Ruvu Chalinze kwenye chanzo cha maji. Nataka kujua, ili mkandarasi aweze kujenga kidaka maji hicho, ni eneo gani litajengwa tanki ili aweze kujenga? Kwani mpaka sasa mkandarasi anashindwa kujua wapi ajenge kidaka maji kwa sababu hajui mwelekeo wa bomba kuu litatoka wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kulipwa wakandarasi wa maji. Katika Halmashauri yangu ya Morogoro tulikuwa na bajeti ya shilingi bilioni 5.19 mwaka 20/06/2017, lakini mpaka sasa tumepata shilingi bilioni 1.09 tu sawa na asilimia 19.84 ya bajeti ya mwaka na sasa tumebakiza miezi miwili muda wa mwaka wa fedha kibajeti kwisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshapeleka madai ya Certificate zaidi ya mara tatu, lakini mpaka sasa hatujapata majibu yenye thamani ya shilingi milioni mia nane ya kumlipa mkandarasi wa Mradi wa Fulwe, Mikese na wengine, ili waweze kumaliza miradi hii kwa wakati. Ombi langu kwa Serikali ni kutuletea fedha hizi, ili kuwalipa wakandarasi kabla ya mwaka wa bajeti kwisha kwani, bajeti ya mwaka huu imekuwa ndogo kuliko ya mwaka jana, yaani ni shilingi bilioni
1.7 toka shilingi bilioni 5.1.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ujenzi wa Bwawa la Kidunda. Bwawa la Kidunda mwaka wa jana ndani ya Bunge lako Tukufu, Serikali kupitia Wizara hii ya Maji iliomba bajeti ya shilingi milioni kumi na saba kwa sababu ya kulipa fidia kwa watu wangu waliopisha mradi wa Bwawa hili la Kidunda; Matuli, Kwaba, Mkulazi, Diguzi, Chanyumbu na watu wa Kitongoji cha Manyunyu na pia kutengeneza barabara ya kutoka Ngerengere mpaka Kidunda.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hakuna fidia iliyolipwa ya shilingi bilioni nne wala barabara iliyotengenezwa katika eneo hilo, ingawa barabara hii ilitengenezwa sehemu korofi na mwekezaji wa Shamba Number 217, Mkulazi Holding Company Limited. Kwa sasa barabara hiyo imejaa maji na kuharibika kabisa kutokana na kwamba haikutengenezwa yote na kwa kiwango kilichotarajiwa na DAWASA. Kwa kuwa, bajeti tulitenga ya shilingi bilioni 17 na Hazina wametoa shilingi bilioni 10 kati ya fedha hizo, lakini sasa Wizara wanasema wametenga shilingi bilioni 1.5 tu ya mwaka 2016/2017 na shilingi bilioni mbili katika bajeti ya mwaka 2017/2018 ambayo haitoshi kwa fidia wala ujenzi wa barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kupata Kauli ya Serikali; kwanza, ni lini wananchi watalipwa pamoja na fidia kwa kuwa muda mrefu umepita? Pili, ni lini Serikali itajenga barabara hii ya kwenda Kidunda, ukizingatia bajeti tulishapitisha na fedha kutolewa na Hazina? Tatu, kwa kuwa, watu waliopisha mradi ni wakulima waliopoteza nyumba zao na mashamba yao yaliyokuwa katika sehemu walizopisha mradi, lakini walikopelekwa wamepewa viwanja tu kama vile wao ni watumishi wa Serikali au wafanyabiashara wakati ajira zao ni kilimo; na kwa kuwa bila mashamba maisha ya wananchi hawa yatakuwa magumu sana na kwamba haiwezekani kuishi, je, Serikali sasa haioni umuhimu wa kumega Msitu wa Mkulazi ulio karibu na makazi mapya ili wananchi hawa wapate sehemu za kulima na kuendesha maisha yao?

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.