Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata fursa ya kuchangia hoja hii muhimu katika Taifa letu. Naungana na wananchi wa Mkoa wa Arusha na Taifa zima kwa maafa ya vifo vya wanafunzi na Walimu wa shule ya Lucky Vincent. Mungu awafanyie wepesi wafiwa wote na Mungu awalaze marehemu wote mahali pema peponi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza Waziri wa Maji, Mheshimiwa Injinia Gerson Lwenge, Naibu Waziri Mheshimiwa Injinia Isaack Kamwelwe, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri sana wanayoifanya pamoja na ufinyu wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuanza kuchangia kwa kuonesha masikitiko kuwa Wizara muhimu kama hii ambayo inagusa moja kwa moja maisha na ustawi wa jamii nzima ya Watanzania imepewa bajeti ndogo. Nina imani kabisa kuwa Watanzania wakipatiwa maji safi na salama watakuwa na ustawi mkubwa wa kiafya, kiuchumi na kimazingira. Maji yataboresha afya za wananchi na kupunguza maradhi na vifo. Kwa kuzingatia umuhimu wa sekta hii tunahitaji kuona bajeti kubwa zaidi ikitengwa kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliwahi kupendekeza kuwa Serikali izingatie changamoto za maji vijijini zaidi na wazingatie kwa njia mbili. Kwanza, yale maeneo yenye maji ya kutosha lakini wanahitaji miundombinu tu lakini pili ni yale maeneo yenye ukosefu kabisa ya maji kutokanana ukame au mvua isiyotosha. Mikakati ifanywe kutokana na changamoto zilizopo kuliko kutoa suluhisho aina moja kila sehemu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ileje na Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini ni maeneo yenye maji mengi sana mwaka mzima kwa sababu ya mito, vijito na chemichemi nyingi kwa hivyo tusingetegemea kuwa wilaya na mikoa hii iendelee kuwa na tatizo la maji la miaka mingi namna hiyo. Je, ni lini sasa Wilaya ya Ileje na mikoa tajwa itapatiwa miundombinu tosha ya kueneza maji katika kata zote lakini zaidi kwa maeneo ya Tarafa ya Bulambya (Humba, Isongole, Chitete, Izubo, Mbebe, Mlale, Dubigu na Malangali).

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo haya wanategemea maji ya Mto Songwe ambayo ni machafu sana. Hata kule kwenye mabomba maji ni machafu sana. Tunaiomba Wizara itukamilishie hii miradi ili tuondokane na adha hii kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ileje ina skimu nyingi za umwagiliaji na zote hazifanyi kazi kikamilifu kwa sababu ya upungufu mdogo mdogo ambao kwa kweli haustahili kukwamisha mradi wa kipindi kirefu namna hiyo. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri atuwezeshe kumalizia skimu zote za umwagiliaji Ileje ili kilimo cha uwagiliaji kifanyike kwa tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ileje na Kyela ni sehemu ya mradi wa Bonde la Mto Songwe unaoendeshwa kati ya Serikali ya Tanzania na Malawi zinazopitiwa na Mto Songwe. Mradi huu upo Mkoa mpya wa Songwe na Ileje na Kyela Mbeya na kwa upande wa Malawi ni wilaya mbili zipo pembezoni mwa Mto Songwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo kuu la mradi huu wa Mto Songwe ni kutunza maji yanayosababisha mafuriko kipindi cha mvua na kuathiri wakazi wa nchi hizi mbili wanaoishi karibu na Ziwa Nyasa. Utekelezaji wa mradi huu ulilenga kujenga mabwawa matatu kandokando mwa Mto
Songwe mpakani mwa nchi hizo, karibu na Ziwa Nyasa. Mabwawa haya yangetumika kuzalisha umeme na pia kufanya kazi za umwagiliaji karibu hekari 3,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri ameainisha kuwa mradi huu uko kwenye awamu ya tatu. Je, hizo awamu mbili zilizopita zilihusu masuala gani? Vilevile Mto Songwe umekuwa ukihamahama kwa sababu ya mabadiliko ya tabia nchi huku ukiharibu rasilimali za wakazi wa bonde na kingo zake kutokana na mafuriko. Je, Serikali ina mkakati gani wa kudumu wa kudhibiti uharibifu huu?

Mheshimiwa Naibu Spika, wakazi wa Kata ya Bupigu Ileje walizuiliwa kutumia Bonde la Mto Songwe kwenye kata yao kwenye eneo ambalo lilikuwa lichimbwe bwawa kubwa mojawapo tangu wakati mradi ulipoanza hadi sasa. Je, Serikali ina mpango gani wa kuanza kushughulikia bwawa hilo sasa au kuwaruhusu wananchi waendelee na shughuli zao?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mto Songwe una urefu wa kilomita 200 ndani ya Ziwa Nyasa, eneo la Bonde ni square kilometer 4,243, square kilometer 2,318 ziko Tanzania na square kilometer 1,025 ziko Malawi. Bonde lina wakazi 341,104 kati yao 210,005 ni wa Tanzania na 131,099 ni wa Malawi. Bonde la mto lina eneo la hekta 6,200 zinazofaa kwa shughuli za uzalishaji na hii ni sababu nyingine kubwa ya kuwa na mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, je, Serikali inaweza kutupatia mkakati wa maendeleo ya bonde hili na ratiba nzima ya utekelezaji na fedha ya kuendeleza mradi huu? Je, Serikali itakaa lini na Halmashauri ya Ileje na Kyela kwa maana ya kutoa taarifa ya kina ya mipango ya utekelezaji wa mradi huu na nini utakuwa ushiriki wa Halmashauri hizi moja kwa moja lakini hata indirectly kwenye mradi huu? Je, kuna mpango gani wa kukutanisha Halmashauri za upande wa Tanzania na wa upande wa Malawi? Kutokana na mpango mkakati wa mradi huu nini kinategemewa kuwa matokeo makubwa ya mradi huu kwa nchi kwa ujumla lakini kwa Ileje na Kyela kiuhalisia?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuhitimisha, naunga mkono hoja ya kuangalia uwezekano wa kuiongezea bajeti Wizara hii na kuziweka fedha hizi kwenye Mfuko Maalum wa Maji Vijijini ili zisitumike vinginevyo. Tunapendekeza asilimia 70 ya fedha ya mfuko huu iende vijijini na asilimia 30 iende mijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja.