Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. ANGELLAH J. KAIRUKI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kipekee kuchukua fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitoe pongezi kwa Serikali kwa kuendelea kutekeleza Mradi wa Same – Mwanga – Korogwe. Mradi huu ni vema ukakamilishwa mapema kwa mujibu wa mpango kazi ili wananchi waweze kunufaika. Aidha, ni vema Serikali ikaona umuhimu wa kuhakikisha dola milioni 97.6 zinapatikana ili Vijiji vya Hedaru, Mabilioni, Gavao, Makanya, Mgwasi, Bangalala, Mwembe, Njoro, Ishinde, Ruvu, Bendera na vinginevyo vipate uhakika wa maji kwa wananchi 264,793 wa Wilaya ya Same.

Mheshimiwa Naibu Spika, pongezi kwa uboreshaji unaoendelea katika Jiji la Dar es Salaam katika sekta ya maji. Wizara ione haja ya kuharakisha utafutaji wa fedha ili kuanza ujenzi wa Mradi wa Bwawa la Kidunda na Kisima cha Kimbiji na Mpera. Aidha, natoa rai Serikali ikamilishe ujenzi wa Tanki jipya la Changanyikeni na Kituo cha Kusukuma Maji Makongo katika mwaka wa fedha wa 2017/2018.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa pongezi kwa Serikali kuona umuhimu wa kuweka mfumo mpya wa kusambaza maji katika maeneo yasiyokuwa na mtandao wa mabomba. Ni vema basi mkandarasi apatikane na fedha za ujenzi wa mifumo hii mipya zitafutwe mapema ili wananchi wa Jiji la Dar es Salaam na Miji ya Kibaha na Bagamoyo waweze kusambaziwa maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na haya, ili kuweza kuongeza kiwango cha upatikanaji wa maji, ni muhimu visima vingi zaidi vikachimbwa ili wananchi ambao hawapati maji waweze kupata. Aidha, maeneo kama ya Kigamboni na mengineyo yaangaliwe ili nayo yaweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, ni muhimu pia Kijiji cha Suji – Malindi -Kitunda (Same, Kilimanjaro) waweze kusambaziwa mfumo wa mabomba ili waweze kupata maji ya kutosha na waweze pia kujihusisha na kilimo cha umwagiliaji maana mfumo uliopo sasa ni wa zamani sana na uliwekwa wakati eneo hili lilikuwa na wananchi wachache. Aidha, maji kupitia Msitu wa Shengena yapo, ni suala tu la kutandaza mabomba yenye uwezo mkubwa ili nao wapate maji ya kutosha. Eneo hili ni la mlimani, hawajanufaika na Mradi wa Same – Mwanga – Korogwe, hivyo, ni vema na maeneo ya milimani nayo yaangaliwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.