Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, nampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri na timu yake yote kwa ujumla kwa kazi nzuri na hotuba nzuri yenye mtazamo wa kukidhi na kufikia matarajio ya Watanzania wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami naomba kuchangia katika suala zima la maji hasa vijijini. Hakuna asiyefahamu kuwa Lushoto ni Wilaya ya milima na mabonde na yenye vyanzo vingi vya maji; lakini tunu ile tuliyopewa na Mwenyezi Mungu hatuitumii ipasavyo, tena ndio sehemu kubwa ya wananchi wanaokosa maji. Kuna tatizo kubwa sana la maji katika Kata za Makanya, Mbwei, Kilole, Ngwelo, Malibwi, Kwekanga, Kwai, Migambo, Ubiri, Gare, Ngulwi, Kwemashai.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo yote haya yana uhaba mkubwa wa maji na ukizingatia maeneo yote haya yana vyanzo vikubwa vya maji, lakini Serikali haijapeleka hata nguvu za kusaidia wananchi hao, kwani kilio chao ni cha muda mrefu sana. Pamoja na kuleta suala hili katika Ofisi za Wizara ya Maji lakini mpaka sasa hatujatengewa pesa yoyote ya maji vijijini na katika Jimbo langu sijawahi kupewa hata mradi mmoja mkubwa, zaidi ya kurukwa kila mwaka. Kwa hiyo, naomba Serikali yangu Tukufu itufikirie watu wa Jimbo la Lushoto na sisi tuweze kupata maji kama wenzetu wa maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, naishukuru Serikali yangu Tukufu kwa kunitengea shilingi bilioni 1.6 kwa ajili ya maji katika Mji wa Lushoto, nawashukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naungana na wenzangu kwa hoja ya kuongeza tozo ya mafuta ya sh.50/= ili iwe sh.100/= kwa kila lita ya mafuta, kwani hii itapelekea upatikanaji wa maji kwa haraka kwa wananchi wetu. Pamoja na hayo, Serikali iweke msisitizo katika Halmashauri zetu na ufuatiliaji madhubuti kuhakikisha wanatenga pesa hizi za vyanzo vya ndani ili pesa hizo nazo ziweze kusaidia maji vijijini kuliko ilivyo sasa, kwani Halmashauri nyingi zinadharau mpango huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naishauri Serikali yangu Tukufu kujenga mabwawa kwa ajili ya kusaidia wakulima pamoja na wafugaji. Kama nilivyosema, mvua nyingi sana zinanyesha katika Wilaya ya Lushoto, lakini maji yale yanaharibika na kuleta maafa pamoja na kuharibu miundombinu ya barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naishauri Serikali yangu Tukufu baada ya kuyaachilia maji haya ya mvua kwenda kuharibu miundombinu, tujenge mabwawa ili maji haya yaweze kusaidia wananchi. Sambamba na hayo, katika Vijiji vya Wilaya ya Lushoto kuna maeneo ambayo mpaka sasa wananunua ndoo ya maji sh.500/= hadi sh.1,000/=. Vijiji hivyo ni vya Kwemakame, Kweulasi, Mbwei, Kilole, Mshangai, Malibwi, Handei, Miegeo, Kizara, Masange, Kongei na Gare.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali yangu, katika bajeti ya mwaka huu nitengewe pesa kwa ajili ya vijiji hivi. Kama unavyojua, tuliwaahidi wananchi tena kwa kujigamba kwa kujiamini kwamba mkinichagua mimi pamoja na Rais wa Chama cha Mapinduzi tatizo la maji tutalimaliza, lakini mpaka sasa naulizwa na wananchi kuhusu maji, nakosa majibu ya kuwapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niihakikishie Serikali yangu Tukufu, wananchi wanayo imani kubwa sana na Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Ninachokiomba kwa heshima na unyenyekevu mkubwa katika Wizara hii initengee pesa ili nikamalizane na wananchi wangu hawa, pamoja na kuendelea kujenga imani kwa wananchi na viongozi wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naishauri Serikali yangu kuhusu hawa Wahandisi walio wengi, hawafanyi kazi kwa weledi, kwani hawa ndio wanachangia kurudisha nyuma miradi hii kwa kutosimamia vizuri. Kwa hiyo, wataalam hawa ambao hawana uwezo wasimamiwe na Mainjinia wa Mikoa ili kusukuma miradi hii ya maji kwa haraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia 100 nami ndiyo nitakuwa miongoni mwa Wabunge watakaoipitisha bajeti hii kwa kusema ndiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.