Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ujumla naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, mimi nikiwa Mbunge wa Jimbo la Mbogwe Mkoani Geita naomba kuelezea kuvunjwa moyo kwa hatua ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kuliweka kando ombi letu la maji ya Ziwa Victoria kufikishwa Wilayani Mbogwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimetumia muda wangu mwingi nikiwa Mbunge wa Jimbo la Mbogwe kuiomba Wizara na kuielezea kwa undani kuhusu tatizo la muda mrefu la ukosefu wa maji hasa nyakati za kiangazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kihistoria Wilaya ya Mbogwe ilikuwa ni sehemu ya Mkoa wa Shinyanga na Wilaya ya Kahama na kwamba Wilaya zote za uliokuwa Mkoa wa Shinyanga zimepatiwa maji ya Ziwa Victoria, mfano, Kahama, Shinyanga, Kishapu, Maswa, Bariadi na Meatu, ziko vizuri na sasa maji hayo yanapelekwa Mkoani Tabora. Sisi tunatengwa hasa baada ya Wilaya yetu ya Mbogwe kuhamishiwa Mkoani Geita.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mahitaji ya maji na suluhisho lake la kudumu hasa katika nyakati hizi mbaya za mabadiliko ya tabianchi. Licha ya kwamba kwa sasa maeneo yetu bado yana misitu na miti kiasi, lakini suala la uharibifu wa mazingira litasababisha ukame utakaosababisha uhaba wa maji na suluhisho la kudumu ni kupata maji kutoka Ziwa Victoria ambayo yako jirani kabisa katika Mji wa Kahama.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwamini Mheshimiwa Waziri Lwenge na Naibu wake Mheshimiwa Kamwelwe kutokana na ahadi ambazo wamekuwa wakiwapatia wananchi wa Wilaya ya Mbogwe kuwa ipo siku maji ya Ziwa Victoria yatafika Wilayani kwao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ujumla, nimevunjika moyo baada ya kuipitia na kuisoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri kuona ndoto ya maji ya Ziwa Victoria imeyeyuka na kupotelea mbali. Hata hivyo, bado nikiwa Mbunge, nitaiishi ndoto hiyo na kumwomba Mungu siku moja maji ya Ziwa Victoria yafikishwe Mbogwe tokea Kahama.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mbogwe tunaomba maji ya Ziwa Vivtoria. Mungu ibariki Serikali ya Tanzania na Mungu ibariki Mbogwe na ombi letu la maji ya Ziwa Victoria lifike kwa Mwenyezi Mungu na limfikie Mheshimiwa Rais na Mawaziri wetu wa Maji, waiishi ndoto yetu ya kupata maji ya Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.