Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze tu kwamba, Mtume Muhammad Karne ya sita alishawahi kusema kwamba “Manla-yashkurunnasa la-yashkurullah” yaani yule ambae hawezi kumshukuru binadamu mwenzake basi hata Mwenyezi Mungu kwa neema alizompa hawezi kumshukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti naomba nichukue fursa hii kukushukuru wewe na kiti chako, lakini kwa namna ya kipekee kabisa kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuja Mtwara kuzindua mradi mkubwa wa utanuzi wa Bandari ya Mtwara Mjini, ninamshukuru sana na nimuombee tu Mwenyezi Mungu aendelee kutusainia mikataba mingine magati yale matatu yaliyobaki yaendelee kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikichangia moja kwa moja kwenye Wizara hii ya maji, mwaka jana niliuliza swali hapa namba 197 ambalo niliulizia suala zima la ujenzo wa maji kutoka Mto Ruvuma kuja Manispaa ya Mtwara. Majibu ya Mheshimiwa Waziri, alieleza Bunge lako hili Tukufu kwamba kwa sasa Serikali inaendelea na majadiliano na Serikali ya China kwa ajili ya kupata mkopo nafuu wa utekelezaji wa mradi huo. Ujenzi wa mradi huo unatarajiwa kuanza katika mwaka wa fedha 2016/2017 na kazi zitakazofanyika ni pamoja ujenzi wa chanzo, mtambo wa kutibu maji, bomba kuu la kupeleka maji Mtwara Mikindani pamoja na kujenga matenki lakini pia na usambazaji wa maji hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikiangalia katika kitabu hiki, Mheshimiwa Waziri amepanga vizuri sana, ameweka na ameeleza kwamba mradi huu bado mpaka leo haujapata pesa wakati mwaka jana walitueleza kwamba mradi huu wa kutoa maji Mto Ruvuma na kusambaza maji Mtwara Mjini ungeweza kuanza katika bajeti iliyopita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba atueleze Mheshimiwa waziri kwamba tunavyoelezwa hapa ndani ya Bunge hili na kwenye Hansard inaeleza kwamba pesa zimetengwa, lakini huu mradi mpaka leo naambiwa majibu yale yale ya mwaka jana mabyo alitueleza, aje na majibu ambayo kimsingi yatawaridhisha wananchi wa Mtwara Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nieleze tu kwamba baadhi ya maeneo ya Mtwara Mjini na hasa kata ya Ufukoni na kata ya Mitengo maji hatuna kabisa na mimi kama Mbunge niliweza kutenga pesa zangu baada ya kuona kwamba huu mradi ni mradi wa muda mrefu na utachukua muda mrefu kuweza kuanza, lakini pia kumalizika, nikapeleka pesa zangu milioni 10 kwa ajili ya kichimba kisima pale. Hata hivyo niliweza kuomba Idara ya Maji, kuna gari pale wanalo la Wizara ambalo linafanya utafiti na kuchimba maji lakini pesa alizonieleza ni pesa nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwambiwa kwamba tutashirikiana na Mbunge tuweze kuchimba kisima maeneo ya Comoro ambako utafiti tayari nilishatoa pesa yangu ya mfukoni tukafanya utafiti, lakini mpaka leo wananinyima gari la kwenda kuchimba kisima pale ili wananchi waweze kupata maji ni jambo la ajabu sana. Nilikuwa namuomba Mheshimiwa Waziri aliangalie hili, atusaidie gari kwa sababu huu mradi bado haueleweki kwa sababu kila siku tunapewa dana dana kwamba watu wa Benki ya China hawajatoa pesa; kila nikiuliza naambiwa watu wa Benki ya China hawajatoa pesa na wananchi kule wanapiga simu sana na wanadai sana maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, mle ambamo tathmini imeweza kufanyika kutoka Kitaya, Jimbo la Nanyamba mpaka Mtwara Vijijini, vijiji vile 26 wote wanahitaji fidia lakini mpaka leo, miaka zaidi ya mitatu hivi sasa wale wananchi wamechukuliwa maeneo yao na fidia hawajalipwa, wanasumbua kweli kweli Wabunge wote wa Mtwata Mjini na Mtwara Vijijini wanatusmbua sana. Kwa hiyo, nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri anisaidie hilo, atupatie gari tuweze kuchimba kata hizi ambazo Mtwara mjini hatuna maji, nitasaidia na mimi Mbunge ili tuweze kuondoa tatizo hli la maji. Pia nizungumzie…………..

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru, muda wenyewe ndiyo hivyo tena, ahsante sana.