Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi nichagie kidogo angalau kwa muda huu mchache. Kwanza nampongeza Rais wangu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, kazi anayoifanya inaonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nizungumzie huduma ya maji katika Jimbo langu la Manyoni Mashariki. Katika ukurasa wa saba Mheshimiwa Waziri mmesema kwamba hadi kufikia Machi, 2017 mmeweza kuwafikishia wananchi wale wanaoishi vijijini asilimia 72. Inawezekana ni sawa lakini si sawa katika Jimbo langu la Manyoni Mashariki. Hali halisi ya Manyoni Mashariki ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninavyo vijiji 58, kati ya hivyo ni 19 tu vimepata maji. Vilevile nina vitongoji 248, kati ya hivyo 37 tu ndivyo vimepata maji, ambavyo ni sawasawa na asilimia 14.9. Ukijumlisha kwa maana ya Rural Manyoni ni asilimia 18.3 tu ya wananchi ndiyo wameweza kupata maji, hii 72 na 18 pengo ni kubwa mno na inasikitisha sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali halisi hii inaridhishwa na kilichopo ndani ya kitabu hiki cha bajeti. Ukiangalia jedwali namba 5(c) ukurasa wa 156 mpaka 157 item namba 10, orodha ya ile mikoa ambayo inatakiwa kujengewa miundombinu ya kusambaza maji ile mikoa kame ile, Manyoni Mashariki haipo, nimejaribu kuangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kama vile haitoshi, jedwali namba 8 ukurasa wa 174 mpaka 184, zile scheme za umwagiliaji, Manyoni Mashariki, pamoja na kwamba tuna Bwawa la Mbwasa, bwawa la kimakakati lile ambalo linatakiwa lichimbwe na upembuzi yakinifu ulishafanyika, inasikitisha halipo kwenye orodha hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama vile haitoshi, jedwali namba 9(a) ukurasa wa 185 fedha za mfuko wa maji zilizopelekwa katika Halmashauri hadi Machi mwaka huu Manyoni Mashariki haipo inasikitisha. Kama vile haitoshi, jedwali namba 13 ukurasa wa 196, orodha ya visima vilivyochimbwa 272 katika nchi hii Manyoni Mashariki haipo; jambo hili linasikitisha sana ni lazima tulalamike. Kuna msemaji amesema huwezi kulalamika, lakini ni lazima mimi niseme kwa nini Manyoni Mashariki tu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilidhani Wizara kwa kuzingatia haya fedha ambayo imetolewa mwaka huu katika bajeti hii tumepewa shilingi milioni 611 tu. Tulidhani angalau tungepewa angalau shilingi bilioni nne Manyoni Mashariki lakini hii haitoshi pia nilidhani kwamba Wizara wangepanga mji wa Manyoni katika awamu ile ya kwanza, katika zile fedha za Mfuko wa India; zipo awamu tatu, Manyoni imepewa awamu ya tatu, kwa nini tusingepengiwa angalau awamu ya kwanza kwa sababu tuna kiu ya maji kwanini mnatuweka kwenye awamu ya tatu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuokoa muda nitoe ombi kwamba Kamati ya Bajeti mtakapokaa na Serikali hebu itazameni Manyoni Mashariki kwa jicho la peke yake, kwanini mnatubagua? Lazima nilalamike, hivi mimi ninakuja kuwapigia tu wenzangu makofi hapa, halafu narudi mikono mitupu kweli kabisa? Hapana, hebu itazameni Manyoni Mashariki tumekosa nini sisi? Sisi ni Watanzania wenzenu.

T A A R I F A . . .

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba ulinde muda wangu, naikataa taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema hapa, sijui kwanini kuna Waheshimiwa wengine hawasikilizi, hizi ni za mwaka wa jana, lakini pia nimeomba hizi pesa za India, nimesema nilidhani kwamba hizi fedha za India, Manyoni ingepewa awamu ya kwanza zipo awamu tatu hapo Mheshimiwa aliyenipa taarifa hebu apitie vizuri pale ziko awamu tatu wamegawanya Manyoni iko awamu ya tatu, tuna kiu, nimesema hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe na mimi nikubaliane na ile tozo ya shilingi 50 kwenye mafuta iongezwe ifike shilingi 100 mtusaidie na hii fedha ianzie Manyoni Mashariki jamani. Pia nakubaliana ya kwamba iundwe Wakala sasa wa Maji Vijijini kama ambavyo ilivyo REA, tusiiweke Seriakli kuu, Serikali Kuu tunaona pesa inapotea na usimamizi siyo mzuri naomba wakubaliane na hilo iundwe wakala kamili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru kwa nafasi.