Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Deo Kasenyenda Sanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Makambako

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. Kwanza naunga mkono ushauri wa Kamati ya Kilimo na Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuishukuru Serikali ya CCM inayoongozwa na Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli, pamoja na Mawaziri, Waziri wa Maji, Naibu Waziri pamoja na wataalam wa Wizara hii ya Maji pamoja na Mawaziri wote wa Wizara zote kwa kazi nzuri wanazozifanya za kutekeleza Ilani ya CCM. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze kama mchumi. Imezungumziwa hapa kwamba fedha zilizotengwa kutoka mwaka jana, shilingi bilioni 900 ya 2016/2017 na sasa zimetengwa fedha pungufu utofauti na nani!

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naipongeza sana Wizara kupitia wataalam, wametenga kitu ambacho ndio uhalisia ambao fedha zitakwenda kwenye miradi. Kwa sababu fedha zilizotengwa mwaka jana hatukuzifikia na ndiyo maana wameonesha hapa tumefikia asilimia 19. Kwa hiyo, nawapongeza sana wataalam wa Wizara hii kwa maana wametenga sasa fedha ambazo zinakwenda kutekeleza uhalisia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na wenzangu ambao wamesema iongezwe tozo ya shilingi 50. Naungana nao kabisa kwamba angalau itaongeza fedha katika huu Mfuko wa Maji. Kamati ya Bajeti watakwenda kukaa kuona namna ambavyo hii tozo yashilingi 50; nadhani tutakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nipate maelezo mazuri Mheshimiwa Waziri atakaposimama, katika miradi ile iliyopata fedha kutoka Serikali ya India ambapo kuna miradi 17 katika Tanzania Bara na Zanzibar ikiwemo na Makambako; watueleze kwa sababu tayari hapa baadhi ya Wabunge tumekuwa na wasiwasi kwamba fedha hizi ambazo zimekuwa zikitoka nje tumekuwa hatuzipati. Sasa naomba Mheshimiwa Waziri atakaposimama atueleze kwa kina uhakika wa kupata fedha hizi ili wananchi wangu wa Makambako wajue fedha hizi zitakwenda kutekeleza mradi ambao Mheshimiwa Rais aliahidi kwamba shughuli ya maji Makambako itatekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kuna Mradi wa Bwawani wa Bwawa la Makambako ambao ni tofauti na mradi huu mkubwa. Mradi huu ulishatangazwa na Mamlaka ya Maji Iringa (IRUWASA) wanaosimamia. Na ilivyotangazwa suala hili liko Wizarani. Nataka nipate majibu nini sasa kinaendelea ili wananchi wa Makambako wajue mradi huu sasa umefikia hatua gani kwa sababu umetangazwa na una muda mrefu tangu watangaze, zaidi ya miezi miwili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo, niwaombe Wizara, fedha kwa mfano zilizotengwa mwaka jana mpaka sasa mtusaidie wenzetu ma-engineer walioko huko, wataalam wa maji, mpaka sasa kuna baadhi ya miradi haijatangazwa. Sijajua kuna kigugumizi gani? Mtusaidie Wizara wanaohusiana na mambo ya Mkoa kule na kadhalika ambapo fedha hizi zilizotengwa katika eneo langu zingeweza kusaidia kupata maji katika vijiji vifuatavyo; vijiji vya Mbugani, Mawande, Mtulingala, Mahongole, Usetule na Ibatu wangepata maji. Lakini vilevile Mheshimiwa Waziri nisaidie kuna mradi mkubwa ule wa Tove ambao unahudumia vijiji kadhaa, vimeishia pale Ilunda. Ilunda pale kuja kwenye kijiji cha Ikelu ni kilometa mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mradi unasimamiwa na nani? Nani ambaye anazuwia wananchi pale Ikelu wasipate maji? Naomba utakaposimama hapa Waziri uniambie kwa sababu maji pale yako mengi na kadhalika, hawapati maji paleā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.