Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii iliyopo mbele yetu. Awali ya yote, napenda kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunifikisha hapa nilipo nikiwa na afya njema. Niwahi mapema kabisa kusema kwamba naunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kujibu na kutoa maelezo ya hoja mbalimbali za Waheshimiwa Wabunge, naomba kwanza kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Mbunge wa Ruangwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuongoza nchi yetu kwa busara na hekima ambayo imeendelea kuleta amani, utulivu na maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda vilevile kumshukuru sana Waziri wangu Mheshimiwa Dkt. Eng. Charles John Tizeba, Mbunge wa Buchosa kwa kunishirikisha kwa karibu sana katika majukumu ya kuongoza Wizara hii nyeti ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Vilevile napenda kuwashukuru sana Makatibu Wakuu wa Wizara yetu, Eng. Mathew Mtigumwe, Dkt. Yohana Budeba na Dkt. Mary Mashingo, Wakuu wa Idara na Taasisi zilizo chini ya Wizara na wafanyakazi wote wa Wizara kwa ushirikiano wa hali ya juu wanaonipa katika kazi yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba vilevile niwashukuru sana wapiga kura wangu wa Jimbo la Ngorongoro kwa ushirikiano wanaoendelea kunipa Jimboni na mara nyingine wamekuwa wavumilivu pale ambapo shughuli za kitaifa zinanifanya nisiwepo Jimboni mara kwa mara. Mwisho lakini sio kwa umuhimu, namshukuru sana kwa dhati kabisa mke wangu mpendwa Asha Mlekwa na watoto wangu wapendwa. Wao wamekuwa sehemu kubwa sana ya mafanikio yangu kwa kunipa nguvu na faraja katika shughuli zangu za kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi, sasa nianze kuchangia moja kwa moja hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge. Mapema kabisa niseme kwamba zimetolewa hoja nyingi sana na sitaweza kujibu kila hoja lakini vilevile itaniwia vigumu kuwataja Wabunge mmoja mmoja kwa majina. Niseme tu kwamba tunathamini sana michango yao na tutaendelea kuifanyia kazi, hatutaweza kuyajibu yote hapa, lakini niwaahidi Waheshimiwa Wabunge kwamba tutaleta majibu ya hoja zote ambazo wametoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nianze kwa hoja ambayo imezungumziwa sana na Waheshimiwa Wabunge wengi na hii inahusu umuhimu wa sekta ya mifugo hapa nchini. Michango ya Waheshimiwa Wabunge ilielekea katika sehemu kubwa kuonyesha kwamba Serikali haitoi kipaumbele katika sekta ya mifugo na wala haitambui kwamba ni sekta muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilifahamishe Bunge lako Tukufu kwamba Serikali ya Awamu ya Tano haiwezi kamwe kuitenga na kuiweka nyuma sekta ya mifugo. Sekta ya mifugo ina umuhimu sana katika usalama wa chakula, uchumi na ajira ya watu wetu. Sekta ya mifugo inatoa ajira kwa kaya zipatazo milioni 4.4 ambayo ni karibu asilimia 50 ya kaya milioni tisa zilizopo hapa nchini na vilevile sekta ya mifugo inachangia asilimia 7.7 ya pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inajulikana kuwa zipo baadhi ya nchi zinazoagiza mazao ya mifugo kwa asilimia 100 endapo nchi yetu ikiingia kwenye kundi hilo, ingetumia jumla ya shilingi trilioni 17.8 kwa mwaka ambayo ni sawasawa na asilimia 60 ya bajeti ya mwaka 2016/2017 kwa ajili ya kuagiza mazao ya mifugo. Hii ni kwa mujibu wa takwimu za ulaji yaani consumption data ya mwaka 2016/2017. Kwa maana hiyo, hata pale kunapokuwepo na watu wanaosema sekta ya mifugo haichangii katika pato la Taifa, ni vizuri kuangalia kwamba tungeweza kupata hasara gani kama tusingekuwa na mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile bei ya mazao ya mifugo ingekuwa kubwa sana na wananchi wa kawaida wasingemudu kutumia mazao hayo kama tusingekuwa na mifugo. Kwa hiyo, sekta ya mifugo ni muhimu sana na Serikali ya Awamu ya Tano inatambua umuhimu wa sekta hii, lakini jitihada mbalimbali lazima ziendelee kufanyika ili kuendelea kuboresha sekta hiyo na iweze kutoa mchango mkubwa zaidi katika maendeleo ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Tano inachukua hatua kadhaa kwa kutambua umuhimu wa sekta ya mifugo ili kuongeza mchango wake kwa Taifa. Wizara kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imeandaa mipango mbalimbali ya kuendeleza sekta hiyo ikiwa ni pamoja na Mpango Kabambe wa Sekta ya Mifugo (Livestock Master Plan) ambao unatekelezwa kupitia ASDP II. Vilevile mradi wa uendelezaji wa uhamilishaji; mradi wa kuendeleza tasnia ya maziwa wa Afrika Mashariki; mradi wa kuendeleza nyanda za malisho; mradi wa kuboresha ambali za kuku; mradi wa kuboresha ambali za ng’ombe na maziwa na mradi wa kuimarisha lishe wa kaya kupitia ufugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kupitia mkopo wa riba nafuu wa dola za Kimarekani milioni 50 kutoka Mfuko wa Maendeleo ya Ushirikiano wa Kiuchumi wa Serikali ya Korea umepanga kukamilisha ujenzi wa machinjio ya Ruvu na hii itaendana na ujenzi wa viwanda vingine vya kusindika ngozi, kutengeneza bidhaa za ngozi na viatu. Vilevile itaboresha Ranchi ya Ruvu kuwa ya mfano; kukarabati na kuweka mizani katika minada 164 nchini kote; kuweka mfumo wa kidigitali wa kuunganisha wafugaji, wasindikaji na wafanyabiashara wa ndani na nje na vilevile mradi huu utajenga mtandao wa wasambazaji wa nyama Jijini Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo Waheshimiwa Wabunge walitumia muda sana kuijadili, ni suala la migogoro ya matumizi ya ardhi baina ya watumiaji mbalimbali. Migogoro ya matumizi ya ardhi inayohusisha wafugaji, wakulima na watumiaji wengine wa ardhi imeendelea kuwepo hapa nchini kwa muda mrefu. Juhudi mbalimbali zilizofanywa na Serikali inawezekana hazijaweza kumaliza tatizo hili na hii ni kutokana na ukweli kwamba migogoro hii huhusisha sekta zaidi ya moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na hilo, Serikali ya Awamu ya Tano iliamua kuunda timu ya wataalam kutoka sekta zinazohusika na ardhi ili kuhakikisha kwamba masuala ya kila sekta yanaangaliwa kwa pamoja. Tayari kama tulivyoweza kuonesha wakati wa hotuba ya bajeti yetu, ripoti ile tumeshaipata na inafanyiwa kazi ili iweze sasa kwenda kwenye Baraza la Mawaziri na hatimaye utekelezaji wa mapendekezo uweze kufanyika. Kwa hiyo, tunaomba Waheshimiwa Wabunge wavute subira kazi iliyofanyika ni kubwa na tunaamini mapendekezo yale yatatusaidia sana kuondokana na tatizo la migogoro ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ni vizuri kueleza kwamba changamoto tuliyonayo katika sekta ya mifugo ni zaidi tu ya migogoro ya ardhi, mifugo mingi tuliyonayo nchini iko kwenye maeneo yanayopata mvua kidogo kwa mwaka ambayo kwa kiwango kikubwa yameathiriwa na madhara yatokanayo na mabadiliko tabia ya nchi hususani ukame ambao umeacha maeneo haya yakiwa hayana nyasi zinazofaa kwa malisho ikiwemo kuongezeka kwa majani yenye sumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri Waheshimiwa Wabunge wakaendelea kufahamu kwamba hata maeneo ambayo ardhi ya wafugaji bado inapatikana kwa kiwango kile kile, lakini ubora wa ile ardhi kwa malisho umepungua sana na ndiyo maana lazima tufikirie tu zaidi ya migogoro. Hali hii imesababisha wafugaji kuhitaji maeneo makubwa zaidi ya kawaida na wakati mwingine hulazimika kuhamia maeneo yenye unafuu na upatikanaji wa malisho na maji na hivyo imekuwa chanzo cha migogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro pia imesababishwa na ongezeko la watu, mifugo na shughuli za kijamii na kiuchumi ambazo zinafanyika kwenye ardhi hivyo kusababisha mgongano wa matumizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuondokana na hali ya nyanda za malisho kuendelea kupungua na malisho nayo kuwa duni Wizara imeanza mpango wa kuboresha nyanda za malisho kwa kupanda mbegu za nyasi zinazoweza kukabiliana na hali ya ukame hasa katika maeneo yaliyoathirika. Kwa hiyo, Wizara inazihamasisha Mamlaka za Serikali za Mitaa ambapo Waheshimiwa Wabunge nyie wote ni Madiwani, kuandaa mipango itakayowashirikisha wafugaji katika kuunga mkono juhudi za Wizara kwa kutenga maeneo ya wafugaji pamoja na kuboresha malisho na kuweka miundombinu ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Waheshimiwa Wabunge tuendelee kuwasisitiza wafugaji wetu kubadilisha aina ya ufugaji ili waendane na mabadiliko ya tabia ya nchi. Katika enzi hizi ambapo mvua na nyasi zimepungua ni lazima nazo tabia zetu za ufugaji zibadilike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo Waheshimiwa Wabunge wameizungumzia sana ni kuhusiana na suala la upigaji wa chapa. Zoezi la upigaji wa chapa linatekelezwa kwa mujibu wa Sheria ya Utambuzi, Usajili na Ufuatiliaji wa Mifugo Na.12 ya mwaka 2010. Utekelezaji wa sheria hii unaendelea nchi nzima na tunafahamu kwamba kuna changamoto ambazo zinaendelea kutokea. Wizara ilibidi isitishe kwanza zoezi hilo ili kutoa fursa kwa Wizara na wadau wengine kujipanga upya na hususani kutoa hamasa na elimu ili wadau waweze kushiriki kikamilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto moja ambayo imetokea karibuni ni kuhusu bei na gharama ya kufanya zoezi hilo. Wafugaji wanalalamika nchi nzima kwamba bei imekuwa kubwa lakini niwaeleze Waheshimiwa Wabunge kwamba utaratibu ambao unatakiwa ufuatwe ni kwamba Halmashauri inayotaka kupiga chapa mifugo ni lazima ijadiliane na wafugaji na wadau wengine kuhusu gharama. Kwa hiyo, ni marufuku Halmashauri au Mkurugenzi mwenyewe kujiamulia bei ya kupiga chapa bila kuwashirikisha wafugaji na wadau wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tatizo la elimu limekuwa kubwa na ndiyo maana Wizara ilielekeza kwamba kabla Halmashauri haijafanya zoezi la chapa ya mifugo ni muhimu kutoa elimu kwa wafugaji na wadau wengine. Nalo hili ni sharti ambalo tumeliweka na tunaomba Halmashauri zote zizingatie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunatambua kwamba suala la upigaji wa chapa linahusiana vilevile na ubora ngozi, tumetoa maelekezo ya namna ya kupiga chapa ambapo haitaathiri ubora wa ngozi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nalo limevuta hisia ya Waheshimiwa wengi ni suala la maendeleo ya ushirika nchini. Serikali inapenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kuwa itaendelea kusimamia maelekezo ya kisera na Sheria ya Vyama vya Ushirika, Na. 6 ya mwaka 2013 ili kupata maendeleo endelevu ya ushirika nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara kupitia Tume ya Maendeleo ya Ushirika inaendelea kushirikiana na Wizara ya kisekta kuwahamasisha wananchi kote nchini kujiunga na kuanzisha vyama vya ushirika wa aina mbalimbali kulingana na mahitaji yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wameonesha wasiwasi mkubwa sana wa baadhi ya tozo ambazo tunapendekeza kufutwa kwamba zitaua ushirika nchini na hususani vyama vya msingi. Tunafahamu kwamba ni kweli kabisa ushuru ni chanzo kikuu cha mapato ya vyama vya ushirika katika kusaidia uendeshaji wake lakini nataka nitumie fursa hii niwatoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge kwamba Wizara imebadilisha mfumo wa upatikanaji wa fedha hizo ambazo awali zilikuwa zikichukuliwa moja kwa moja kulingana na mjengeko wa bei wa mazao husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu tunaopendekeza sasa ni kwamba bodi za vyama zinatakiwa kuomba fedha hizo za uendeshaji kupitia mikutano mikuu ya wanachama ambao wataidhinisha kutokana na hali halisi ya uzalishaji katika makisio yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kimsingi ushuru ule wa kuendesha vyama vya ushirika utakuwepo lakini siyo kwa mpango wa sasa ambapo tunaweka kiwango kimoja katika nchi nzima, ni lazima mahitaji ya chama kimoja kimoja yajadiliwe na kuombewa ruhusa ili hizo fedha ziweze kupatikana. Kwa hiyo, kimsingi Waheshimiwa Wabunge ninachosema tunajali suala hili kwa sababu vyama vya ushirika ndiyo hasa vinaendesha maendeleo ya mazao kwa hiyo siyo kwamba vyama vya ushirika vitakufa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya Waheshimiwa Wabunge walitoa hoja kuhusu kupatiwa ruhusa ya baadhi ya vyama vikuu ambavyo vimeonekana vikubwa viweze kugawanywa. Mfano uliotolewa ulikuwa ni chama cha TANEKU. Tunachosema kulingana na sheria lakini vilevile kulingana na Katiba, uhuru wa kujumuika ni pamoja na uhuru wa kutotaka kujumuika kwa mtu au taasisi ambayo inapenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Chama chochote cha ushirika ambacho kinataka kuchukua hatua za kujigawanya ni sharti wazo hilo na maamuzi yafanyike katika mikutano ya kisheria hasa mikutano mikuu lakini baadaye wakishafanya kwa sababu Wizara na hasa Tume ndiyo inayosimamia Sheria ya Ushirika, ni lazima vitu vingine viangaliwe ikiwa ni pamoja na kuangalia kwamba ushirika unaendelea kuwa imara lakini vilevile kuangalia economic viability.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama wananchi na wanachama wa TANEKU wanakusudia kugawa chama cha TANEKU wao wakae kwenye mikutano yao halafu baada ya hapo walete mapendekezo Wizarani na sisi tutaangalia kama kweli masharti mengine wameweza kukidhi ikiwa ni pamoja na kuangalia isije ikasababisha migogoro zaidi kwa sababu kuna maeneo ambayo tumegawanya vyama lakini migogoro ikatokea hususani wakati wa kugawanya mali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachosisitiza tu ni kwamba tunachoangalia sana siyo utitiri wa vyama, sio uwingi, lakini ni ubora na uwezo wa kujiendesha kama taasisi ambazo zina demokrasia lakini ambazo zinaweza kujimudu kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa ningependa kuzungumzia suala la uwekezaji katika maeneo tengefu ya Shungimbili, Mbarakuni na Nyororo kwa sababu ya muda nitazungumzia kuhusu kisiwa cha Shungimbili. Hoja ilitolewa kwamba kisiwa cha Shungimbili kimeuzwa, naomba kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba hakuna ukiukwaji wowote wa utaratibu uliofanyika katika uwekezaji katika kisiwa cha Shungimbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi hifadhi ya bahari na maeneo tengefu haijawahi kupora maeneo na kuyauza, shughuli zinazofanyika katika maeneo tengefu ni zile zinazokubalika kwa mujibu wa sheria ambazo ni mafunzo, utafiti na utalii ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya utalii ambayo ni rafiki kwa mazingira, hicho ndio kilichotokea Shungimbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo wasiwasi wa wananchi wa Mafia kwamba kisiwa kimeuzwa ni kwa sababu mwenye hoteli amegeuza jina akaita Thanda Island na hivyo akaona kwamba imeuzwa mpaka imebatizwa jina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba tayari kuna maelekezo kutoka Wizara ni kwamba mwekezaji abadilishe jina kutoka Thanda Island lirudi kuwa Shungimbili. Haiwezekana kisiwa ambacho cha watu wa Pemba kwa miaka yote wanafahamu kwa jina la Shungimbili halafu leo hii Mwekezaji anakuja anabadilisha jina analotaka yeye, tumetoa amri kwamba ni lazima jina lirudi kama ilivyokuwa mwanzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ningependa tu kumhakikishia Mbunge wa Mafia kwamba taratibu zinaendelea, lakini vilevile Halmashauri ya Mafia imekuwa ikinufaika na uwekezaji uliofanyika hapo, changamoto zingine ambazo zipo tutaendelea kujadiliana na Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi na Halmashauri ya Mafia ili kuendelea kuzitatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, machache, nashukuru sana na niombe kuunga mkono hoja.