Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo kama uti wa mgongo wa uchumi wa Taifa letu bado hakipewi uzito unaostahiki. Pesa zilizotengwa katika bajeti hazitoshi kukabili mahitaji yaliyopo, hata hivyo nashauri yafuatayo:-

(a) Utafiti ufanyike ili kujua matatizo katika ardhi na kwa maana hiyo ushauri ufanyike ni mbegu gani itumike kwenye eneo husika kulingana na utafiti uliofanyika. Mfano, ardhi ya Visiwa vya Ukerewe inahitaji kufanyiwa utafiti na hatimaye lipatikane suluhisho la aina ya mbegu, mazao na kilimo kinachopaswa kufanyika.

(b) Ufanyike uwekezaji wa kutosha katika kilimo cha umwagiliaji hasa kutokana na mabadiliko ya tabianchi hali inayoathiri kilimo chetu kinachotegemea zaidi mvua. Mfano, eneo linalozungukwa na maji kama Ukerewe ingepaswa kuwa wazalishaji wakubwa wa chakula iwapo tu Serikali itawekeza katika kilimo cha umwagiliaji katika visiwa hivyo. Kuna mabonde makubwa ya Bugorola na Miyogwezi ambapo Serikali imewekeza zaidi ya shilingi millioni 700, lakini mradi huo umetelekezwa. Naomba kujua Serikali ina mpango gani na miradi ya umwagiliaji wa Miyogwezi?

(c) Zitolewe ajira kwa Maafisa Ugani wengi na wasambazwe kwenye maeneo mbalimbali ili kutoa ushauri kwa wakulima wetu na hivyo kuongeza tija katika kilimo chetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shughuli za uvuvi zinatoa ajira kubwa kwa wananchi wengi katika nchi hii lakini kuna changamoto nyingi sana na hivyo naomba kushauri yafuatayo:-

(a) Sheria Na. 22 ya mwaka 2003 ipitiwe upya na ufanyike utafiti wa kina kwa kushirikisha wadau hasa wavuvi wenyewe ili tuwe na sheria nzuri na rafiki kulingana na mazingira. Mfano, kuzuia nyavu ‘piece 3’ kunahamasisha wavuvi wa sangara kuvua kina kifupi cha maji na hivyo kuharibu mazalia ya samaki. Pia nyavu za mm10 kwa nyavu za dagaa ni kuwanyima fursa wavuvi hasa katika Ziwa Victoria ambapo ni vigumu kupata dagaa size hiyo.

(b) Wavuvi wamekuwa wanavamiwa na kujeruhiwa au kuuawa wanapokuwa wanafanya shughuli zao za uvuvi katika ziwa. Nashauri Serikali iweke mfumo thabiti wa kiulinzi ili wavuvi hawa wafanye shughuli zao kwa usalama.

(c) Bado tozo ni nyingi sana katika sekta hii zinazowakabili wavuvi na hivyo Serikali ipunguze tozo hizi ili wavuvi wetu wafanye shughuli zao kwa ufanisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza hatua ya kuondoa ada ya usafiri kwa mitumbwi midogo.