Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru Mungu kwa wema na rehema zake nyingi katika maisha yetu. Nakushukuru kwa nafasi hii ya kuchangia hotuba hii ya sekta hii muhimu sana kwa ustawi na mustakabali mzuri wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Dkt. Charles Tizeba, Naibu Waziri Kilimo, Mheshimiwa William Olenasha, Katibu Mkuu na watendaji na wataalam wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri wanayoifanya kusimamia sera, sheria na utendaji wa Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni sekta ambayo ikisimamiwa vizuri itainua uchumi wa Tanzania kwa kiwango kikubwa sana kama takwimu zinavyoonyesha. Naipongeza Serikali kwa kuja na mapendekezo mazuri ya kuboresha sekta zinazosimamiwa na Wizara hii. Hii inalenga moja kwa moja kuongeza mali ghafi muhimu za viwanda mbalimbali nchini kwetu hususan vijijini na wilayani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu kwa Serikali ni kukaa kwa pamoja kuweka mikakati inayojengana (complementary) ili kuhakikisha malengo ya uzalishali, tija na ubora vinafikiwa kwenye mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi. Nnazungumzia Wizara ya Kilimo, Wizara ya Maji, Wizara ya Mazingira, Wizara ya Viwanda, Wizara ya Miundombinu na Wizara ya Nishati na Madini. Hii itawezesha kuhakikisha kuwa lengo letu kuu la kufikia uchumi wa kati na wa viwanda linafikiwa kwa ufanisi, gharama ndogo na matokeo makubwa kwa kuanzia na maeneo ya kimkakati yaliyoainishwa yote yawekewe huduma ya miundombinu muhimu ili yawe na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba inaonesha kuwa sekta ya kilimo inachangia asilimia 29.1 ya pato la Taifa, ajira asilimia 65 na chakula kwa asilimia 100. Basi Serikali ione umuhimu wa kutoa kipaumbele kwenye sekta hii kwa kuwavutia vijana wengi zaidi kuingia katika sekta kwa njia zifuatazo:-

(i) Kuanzisha vikosi vya uzalishaji vya vijana kila kata nchini na kuainisha aina ya uzalishaji unaofaa kila eneo, ufugaji wa mifugo ya kawaida mikubwa kwa midogo, samaki kwa mabwawa, nyuki na kilimo cha aina mbalimbali;

(ii) Kuwapatia mafunzo ya taaluma ya kufanya shughuli hizi na mafunzo ya ujasiriamali;

(iii) Kuwezesha kujisajili kama kampuni au ushirika wa vijana na kuwaunganisha na vyombo vya kifedha kwa kupata mitaji; na

(iv) Vikundi viwe chini ya Halmashauri na Afisa Kilimo, Afisa Maendeleo ya Jamii, Afisa Misitu na Afisa Mifugo. Wote wawasimamie vijana hawa na kuhakikisha wanaendelea na miradi yao hadi kuvuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo maeneo na shughuli za masoko yatengwe na kuwekewa miundombinu mizuri ya kuuza mazao hayo na vijana wawezeshwe kuanzisha viwanda vidogo na biashara ndogo za mazao wanayozalisha. Hii itawafanya vijana wengi kubaki vijjijini kulima, kufuga, kusindika, kufanya biashara na kuacha kwenda kunyanyasika mijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tungependa kuona jinsi Wizara hii inashirikiana moja kwa moja na Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwenye kilimo cha umwagiliaji. Hali kadhalika tuone miundombinu ya barabara na reli na umeme vinaendelezwa kwenye maeneo haya ya uimarishaji wa sekta hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Songwe, hususan Wilaya ya Ileje ambayo iko kwenye Programu ya Bonde la Mto Songwe ina eneo kubwa sana la takriban hekari 6,428 ambalo linafaa sana kwa kilimo cha mazao ya nafaka mbalimbali, ufugaji wa samaki, mifugo na mbogamboga na matunda. Licha ya maji ya Mto Songwe, Wilaya ya Ileje inapata mvua nyingi kila mwaka na ina rutuba ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaitaka Serikali iingize eneo la Bonde la Mto Songwe lililoko Ileje ili lipangiwe mkakati mzuri wa kuliendeleza kwenye mazao ya kilimo cha biashara, kwa mfano, kahawa, ufuta, alizeti, pareto, karanga, mpunga, matunda, mboga mboga pamoja na ufugaji wa samaki wa mabwawa, kuku, ng’ombe wa maziwa na wa nyama, nguruwe, mbuzi, kondoo na nyuki. Hii iendane na wazo la hapa juu la kuwawezesha vijana kwenye vikosi vya uzalishaji itainua ajira sana, mapato ya vijana wenyewe, Halmashauri na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ileje ni wilaya ya mpakani mwa Tanzania na Malawi na kwa kiasi Zambia lakini vilevile ni jirani sana na Wilaya ya Tunduma ambako biashara kubwa inafanywa na watu wa nchi za jirani hadi DRC Kongo. Halmashauri ya Ileje ilijenga soko kwa ajili ya mazao lakini NFRA wamekuwa wakitumia soko la Isangole kama maghala yao. Tunaitaka Wizara kujenga maghala makubwa sana kwa nafaka na mazao mengine ya biashara kama kahawa, pareto, viungo mbalimbali kama iliki, pilipili manga, mdalasini, tangawizi, cocoa na kadhalika. Tunaiomba Wizara itupatie maghala ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu pia kuwa SAGCOT inahusisha Mkoa wa Songwe. Pia tunaitaka Serikali itufahamishe hadi sasa Songwe na hususan Ileje inaguswa vipi na mradi huu na ni katika maeneo yapi na hawa wahusika kwa eneo letu ni akina nani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa ya kilimo chetu ni upatikanaji wa mvua za kutosha, mbegu bora na pembejeo. Tunaipongeza sana Serikali kwa kuja na pendekezo la kuboresha mfumo wa upatikanaji wa pembejeo. Huu ni mfumo wa kimageuzi na utahakikisha wakulima wengi kupata pembejeo na kulima vizuri zaidi. Tutashukuru kuwa sasa pembejeo zitapatikana kwa wakati na kwa bei nafuu na kuondoa malalamiko ya muda mrefu na vilevile kuhakikisha wakulima wanazalisha vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atafute muda wa kutembelea Ileje yeye na maafisa/ wataalam wake waje kujionea wenyewe fursa nyingi zilizopo wilayani humo ili watuweke kipaumbele chini ya programu ya SAGCOT na mradi wa Bonde la Mto Songwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Songwe na Mkoa wa Mbeya na Iringa ni wakulima wakubwa wa arabica coffee, pareto, chai na viungo kwa kutaja machache. Japan wana soko kubwa la gourmet coffee na wanailipa bei nzuri. Wilaya hizi zina uwezo wa kuzalisha aina hii ya kahawa na kuiuza Japan. Tunaitaka Wizara ituunganishe na soko hilo lakini pia watupatie utaalam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba mnada wa kahawa ufanyike Songwe kwenye uzalishaji mkubwa wa kahawa na tunahitaji soko/viwanda vidogo vya kuongeza thamani ya pareto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.