Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kukushukuru, kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake na watendaji wao wote kwa kazi nzuri waliyoifanya. Naomba niende moja kwa moja kwenye kuchangia Wizara hii ambayo ni muhimu kwa watu wote; siyo hata kwa asilimia kiasi gani, ni kwa watu wote. Asilimia 75 inatoa ajira, asilimia 100 yote inatoa chakula, inatoa malighafi kwenye viwanda na inachangia pato la Taifa kwa 28%.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba wote kwa pamoja kama tulivyoonesha toka juzi kwamba sekta hii ni sekta muhimu na tuombe Serikali ione umuhimu wake kwa kujali kuiongezea bajeti, hata kama siyo mwaka huu, basi miaka inayokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia utaona kilimo kinashuka, hakipandi. Ndiyo maana umaskini wa watu unaongezeka ndugu zangu. Mwaka 2011 kilimo kilikua kwa 3.5%, mwaka 2016 kilimo kilikua kwa 1.7%. Angalieni kutoka 3.5% mpaka 1.7% na bado tunategemea kuondoa umaskini wa Tanzania itakuwa ni kazi ngumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo kilimo kimechangia 28% katika pato la Taifa. Bajeti ya kilimo kwa mwaka 2011 ilikuwa 7.8% ya bajeti ya Serikali. Mwaka 2016 bajeti ya kilimo imepangiwa 4.9%. Kwa hiyo, muone uhusiano kati ya ukuaji wa kilimo na jinsi bajeti inavyotolewa. Kwa hiyo, naomba Waziri aone na Serikali nzima ione kwamba namna pekee ya kukuza sekta hii ni kuiongezea bajeti yake na kujielekeza kwenye changamoto ambazo zinakabili sekta hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri na Serikali kwa ujumla kuona kwamba, namna moja ya kukabiliana na changamoto ni kuwa na ununuzi wa pamoja wa pembejeo na hususan mbolea. Tukifanya hivyo, tutakuwa tumeisaidia sana, lakini naomba sana mbolea hii ifike kwa wakulima na wapate manufaa ya ununuzi wa pamoja, isiishie hapa katikati kwa sababu kuna hatari ya manufaa haya kwenda kwa wafanyabiashara badala ya wakulima na hivyo isiwe na impact kwenye kilimo chenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niongelee kwa muda uliobaki juu ya mifugo. Mimi ni mtoto wa wafugaji, lakini vilevile wafugaji ambao wanalima. Kwa hiyo, sina sababu ya kupendelea upande mmoja, ila ninaomba Waheshimiwa Wabunge na Serikali tuone kwamba mifugo ni mali ya watu mmoja mmoja, lakini ni rasilimali ya Taifa. Mifugo kweli ni mali ya mtu mmoja mmoja lakini ni rasilimali ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hifadhi zimepangiwa maeneo na yanajulikana. Kilimo kinajulikana kwa sababu mazao yako shambani, lakini mpaka leo maeneo ya wafugaji hayajulikani, wao wanahangaika nchi nzima. Ninaomba sana, mipango na matumizi ya ardhi ndiyo namna pekee ya kuondoa migogoro na hifadhi na wakulima na watumiaji wengine na wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba kwa maisha yao wafugaji wanategemea mifugo hiyo, kunapokuwa hakuna majani wanatafuta. Mipaka ya hifadhi wakati mwingine haijulikani, kwa hiyo, ng’ombe wanaingizwa kwenye hifadhi labda kwa bahati mbaya, siyo kwa sababu watu wanataka kuvunja sheria. Kwa hiyo, wanapokutwa ng’ombe kule, wanapokamatwa na wanapoadhibiwa wafugaji, wakiamua kwamba ng’ombe warudi, ni lazima warudi wamepungua. Hii ni sawa na ni haki jamani? Naomba tuwasaidie wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kwamba, kunapokuwa na ukame, kwanza bei ya mifugo inashuka, lakini na ng’ombe wanahitaji maji na mito itakuwa kwenye hifadhi. Tunafanya nini? Badala ya kungojea kuwaadhibu wafugaji, naomba tujielekeze katika namna ya kuweza kutatua matatizo yao kwa kuwa na mabwawa na miundombinu ambayo itasaidia wakulima na wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni hili kwamba vilevile kunapokuwa na migogoro, wafugaji wanapoenda Mahakamani, pamoja na kwamba watu watalia kwamba kuna rushwa, lakini wanaposhinda basi, ama wale wanaoshindwa, wakate rufaa, lakini wasiamue kuwatesa wafugaji kwa kuwanyima ng’ombe wao au kuwauza. Hata sasa hivi, najua hifadhi zina sheria kali, lakini tuone hali yenyewe ya nchi ilivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba tuone kilio cha wafugaji; wafugaji ni Watanzania, wana rasilimali ya Taifa, wanalinda mali ya Taifa kwa sababu Tanzania ni ya tatu katika ufugaji Afrika. Manufaa ya wafugaji hayaonekani, siyo kwa sababu tu ndugu zangu wanahamahama au wanachunga badala ya kufuga, ni kwa sababu, wanahitaji elimu, wanahitaji miundombinu na kuzijua sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye alama au chapa ya ng’ombe. Naelewa kwamba ufuatiliaji wa mifugo (traceability) ni muhimu sana, lakini naomba tuwaelimishe wafugaji. Vilevile unapoandikisha ng’ombe wako Gairo, kama hakuna maji, hivi watabakije pale? Lazima wahame, kwa hiyo, wafugaji wanaona mkiwachapa ng’ombe, ni kwamba sasa mnawa-condemn wale ng’ombe kufa yatakapotokea matatizo ya ufugaji, kama ukame au magonjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba sana, wakati tunachapa ng’ombe, ili traceability iwe rahisi, tuhakikishe na miundombinu ipo; ili wananchi waone manufaa. Wafugaji nao waelewe kwamba ng’ombe wanavyoweza kufuatiliwa, soko la dunia inakuwa rahisi kulipata. Kama hakuna namna ya kufuatilia, Soko la Dunia linakuwa na wasiwasi. Kwa hali ilivyo sasa hivi, tunakazania kuchapa ng’ombe, lakini hatukazanii kuunda miondombinu kuweza kuwasaidia wafugaji na changamoto ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kidogo juu ya uvuvi na Mheshimiwa Waziri anatoka kule kwenye uvuvi. Jamani ni Tanzania tu ambapo uvuvi haramu umeenea. Ninaomba tuchukue hatua ambazo zinatakiwa ili huu uvuvi haramu uweze kwisha. Wavuvi vilevile waelimishwe waone umuhimu wa kutumia nyenzo zile ambazo zinatakiwa katika uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutaiangalia sekta hii vizuri, Tanzania itaondokana na umaskini na itafika kwenye uchumi wa kati na uchumi wa viwanda. Bila kilimo kutengemaa, viwanda havitawezekana nawaambia. Wafanyakazi wa viwandani watakuwa wanakula nini kama hakuna kilimo nchi hii? Tutakuwa tunaagiza nje. Malighafi zitatoka kule, kama hakuna kilimo, viwanda vitakuwaje imara? Kama viwanda vya Tanzania havitahusishwa na kilimo, maana yake tutakuwa hatuna utengamavu kwa sababu, tunachotaka tuwe na uchumi ambao unapanda kupitia kuongeza thamani ya mazao ambayo Watanzania wengi ndio wanayategemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Nilikuwa nafikiri nitachelewa kutoka Dar es Salaam, nimewahi. Naomba Wabunge wote tuone umuhimu wa kilimo, ufugaji na uvuvi kusudi nchi yetu iendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba wafugaji waangaliwe kwa macho ya huruma badala ya kuwafunga au kuchukua ng’ombe zao na bila kuona kwamba pengine siyo makusudi. Ahsante sana.