Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Susanne Peter Maselle

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. SUSANNE P. MASELLE: nakushukuru Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabla sijaanza kuchangia napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kuilinda familia yangu, hasa baba yangu ambaye alikuwa anaumwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda nipongeze hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani ambayo imesheheni vitu vingi sana na vya muhimu ambapo Serikali kama itavichukua na kuvifanyia kazi, basi sekta hii itafanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia kuhusu uvuvi. Kanda ya Ziwa katika sekta hii ina umuhimu sana hususan Mkoa wa Mwanza, maeneo ya Buchosa, Magu, Kwimba na Ilemela wanategemea sana uvuvi, lakini Serikali naona kama haitilii umuhimu sana hii sekta. Kwa sababu gani nasema hivi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wavuvi wamekuwa wakinyanyaswa sana kwa kunyang’anywa nyavu zao. Siyo kwamba nabariki watumie nyavu ambazo hazifai, la hasha! Mwaka 2016 nilizungumza nilivyokuwa nachangia kwamba Serikali inatakiwa itoe elimu jinsi ya kutumia hizi nyavu, ni nyavu gani wavuvi wanatakiwa watumie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilizungumza na Waheshimiwa Wabunge wengi sana walizungumza kwamba ni kwa nini maduka bado yapo ambayo yanauza; na viwanda vinatengeneza nyavu hizo? Wavuvi hawa wamekuwa wakinunua kwa kutumia pesa, matokeo yake, wananyang’anywa, zinachomwa na wanajikuta wanaingia katika umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi Februari kulikuwa na mgomo wa wavuvi na Serikali ikasema kabisa kwamba inaunga mkono mgomo huo. Sasa mimi nikashangaa ni kwa nini Serikali iunge mkono badala ya kutatua tatizo? Maana yake ni kwamba inaunga mkono tuwe na watu ambao hawana kipato na mtu asipokuwa na kipato matokeo yake anakuwa anafikiria mawazo mabaya ambayo yanapelekea hata kujiingiza katika vitendo vibaya ambavyo siyo vizuri kwa jamii. Kwa mfano, tunaweza tukatengeneza watu ambao ni vibaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningetaka tu Serikali na Mheshimiwa Waziri anapokuja atuambie ni mkakati gani walionao wa kuweza kutatua hili tatizo ili wananchi wetu waweze kufanya hii shughuli wakiwa na amani na kusiwe na ile tabia ya Serikali na wavuvi kuviziana. N kama vile wanaviziana kwamba wakitumia hizo nyavu na wenyewe wanakuja kuwanyang’anya ni kama kuviziana. Sasa tukitoa elimu, tutakuwa tumewasaidia sana watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu kilimo, Mkoa wa Mwanza una eneo kubwa, takribani asilimia 53 ambalo limzungukwa na Ziwa Victoria. Hii inatoa nafasi kubwa kwa kilimo cha umwagiliaji, lakini mpaka sasa sijaona hatua yoyote ambayo imechukuliwa ili tuwe na kilimo cha umwagiliaji katika Mkoa Mwanza. Wakulima wengi wamekuwa wakitegemea kilimo ambacho ni cha majira, lakini majira yakibadilika, wanashindwa kulima. Kama kwa sasa, kumekuwa na ukame, tungekuwa na kilimo cha umwagiliaji wananchi wetu wangeweza kulima bila kutegemea majira ambayo yanakuwa yanawaangusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona chakula kimekosekana na wananchi wanapolalamika, kwa mfano Mheshimiwa Rais alikuja, nafikiri ilikuwa ni Shinyanga, watu wakamwabia kwamba wana njaa na akawaambia hawezi kuwapikia. Wanaposema kwamba wana njaa, siyo...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa kwa mchango wako.