Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa na mimi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa pumzi na uhai na kwamba naendelea kuwatumikia wananchi wa Mkinga, lakini vilevile kutoa mchango kwa Taifa langu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze sana Kamati inayohusika na Wizara hii. Kamati imefanya kazi kubwa, Kamati imetufumbua macho juu ya hali mbaya iliyopo katika sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapoambiwa ukuaji wa sekta hii ni 1.7%, lakini unapoambiwa kwamba 65% ya Watanzania nguvu kazi hiyo inafanya kazi kwenye sekta hii halafu unapoambiwa kwamba mikopo inayokwenda kwenye sekta hii is only 2% na unapoambiwa kwamba fedha za maendeleo zilizotoka ni 3% tu, unachanganyikiwa. Kama nchi lazima tujitazame upya, lazima tujitafakari, tukishindwa kufanya hivyo tutaendelea kuwa soko la nchi nyingine.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii usindikaji wa maziwa yetu is only 3% ya tunachozalisha. Tunaagiza 62% ya maziwa kutoka Kenya, tunaagiza twenty something percent kutoka South Africa, tunaagiza 4% ya maziwa kutoka Uganda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa hapa ni mashahidi leo hii Tanzania imekuwa jalala la matunda kutoka South Africa. Tunaagiza apples, machungwa na kadhalika. Hatuwezi kwenda namna hii lazima tubadilike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri anapoambiwa kwamba usindikaji wa maziwa katika nchi yake ni 3% tu, hili lazima limuumize kichwa. Nawasihi sana tuongeze nguvu katika kurekebsha mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye korosho halikadhalika. Korosho yetu yote tunaipeleka ikiwa ghafi kwa kiasi kikubwa. Nilisema juzi hapa na wapo baadhi ya Wabunge wenzangu waliniunga mkono kwamba tutumie fedha zile za export levy, twendeni tukajipange tuseme walau tuanze kwa kuhakikisha 50% ya korosho yetu inabanguliwa hapa ndani, tutumie fedha zile kujenga viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza Wizara wamekuja na initiative ile ya kugawa bure dawa zile za kunyunyiza. Vilevile mnaangalia uwezekano wa kutoa hata magunia, ni hatua nzuri. Hata hivyo, ili twende haraka zaidi hebu twende kule kwenye kujenga viwanda vya kubangua korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine, tuliwahi kuambiwa hapa ndani ya Bunge, wakati watu wa Tanga tunapiga kelele kuhusu viwanda vya matunda, tukaambiwa Tanga machungwa yenu hayafai kwa kutengeneza juice. Sasa Serikali mkishasema hivyo halafu mnaishia hapo, kwa nini hamji na utaratibu wa kuhakikisha mnabadilisha mbegu ile ili tuwe na mbegu zinazofaa kwa wakulima wetu? Kwa nini hatuipi nguvu Mlingano iweze kufanya utafiti au tukaingiza mbegu kutoka nje ili kubadilisha machungwa katika nchi yetu tuwe na machungwa hayo yanayofaa kwa kutengeneza juice? Nawasihi sana liangalieni hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Tanga tunalima mazao ya viungo, Muheza, Korogwe na Mkinga, lakini tuna tatizo kubwa la utafiti wa mbegu bora katika maeneo hayo. Mbegu inayotumika ni ya tangu Adam na Hawa. Tunaomba mfanye kazi katika eneo hilo. Najua huko mbele ya safari mtasema tumieni ASDP na kadhalika lakini toeni maelekezo ili kutumia ASDP II mambo haya yaweze kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine. Hivi Serikali mmeshindwa kutusaidia watu tunaolima zao la minazi kuweza kuondokana na tatizo lile kwa zaidi ya miaka 20 sasa? Kweli mmeshindwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu Philipines walipopata tatizo la janga lile la mafuriko na minazi yao ikaondolewa walikimbilia kwa watu wa FAO, walipata fedha dola milioni 35. Leo hii Philipines imerudi kwenye chart yake ya kuwa nchi ya pili kwa uzalishaji wa zao la nazi duniani. Tunaomba mtusaidie tuondokane na umasikini kwa watu wetu. Zao la minazi ndani yake unapata bidhaa karibu 11 lakini zao la minazi ukilienzi maana yake hata mazingira unayatunza. Hebu tujielekeze kwenye eneo hili tuondoe tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nisipolisema nitakuwa sijatenda haki ni kuhusu uvuvi. Nimekuwa nikisema hapa sekta ya ufugaji wa samaki ndiyo sekta inayokua katika ulimwengu kwa kasi kuliko sekta yoyote ndani ya sekta za kilimo. Hapa nimeona taarifa kwamba kwa mwaka jana mazao ya samaki kutokana na ufugaji wa samaki yameongezeka kutoka tani 3,000 mpaka tani 11,000. Nina uhakika hizi ni jitihada binafsi za watu kwa sababu jedwali hili linatuonesha kwamba hatukuwa na fedha za maendeleo kwa mwaka uliopita lakini hii ni sekta ambayo tukiwekeza tunaweza kuvuna zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu Kenya miaka sita iliyopita waliwekeza takribani bilioni 35. Mwaka huu wa fedha wametenga bilioni saba kwa sekta ya ufugaji wa samaki peke yake. Jirani zetu Zambia wameanzisha mradi mkubwa, wamewekeza bilioni 112 kwa ajili ya sekta ya ufugaji wa samaki peke yake, halikadhalika Uganda. Hii maana yake nini? Maana yake wenzetu wameiona hii opportunity wanawekeza, sisi hatuwekezi maana yake tutakuwa soko la samaki watakaowazalisha. Nawasihi sana twendeni tukawezeke kwenye eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni bandari ya uvuvi. Hivi tunapata kigugumizi gani kwenye jambo hili? Mimi niliwahi kusema hapa hebu tujiongeze…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.