Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru kwa kunipa fursa niweze kuchangia katika sekta hii muhimu sana kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi, lakini pia kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wetu mmoja mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa tunaongea juu ya sekta inayoajiri zaidi ya asilimia 65.5 ya wananchi wetu. Suala la ajira nchi hii limekuwa ni jambo ambalo halijawahi kupata suluhu; lakini hapa tunayo sekta ambayo inaajiri asilimia 65 ya watu wetu, lakini ni sekta ambayo pia tunaipa fedha kidogo kiasi hicho. Takwimu zimetuambia Sekta ya Kilimo mwaka 2015 na mwaka 2016 imechangia asilimia 29 ya pato la Taifa. Nadhani tuna kila sababu ya kuitizama sekta hii ili iweze kuchangia pato la Taifa kwa kiasi kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaongea asilimia 65 ya Watanzania, Watanzania waadilifu, watiifu ambao wamebaki vijijini wanazalisha, siyo wale waliokimbilia mijini, lakini Watanzania hawa ni wale ambao wanakumbana na changamoto mbalimbali za kimaendeleo. Ukija ukame ni wao; wadudu waharibifu ni wao, kwelea kwelea ni wao, tatizo la maji linaandama kundi hili, lakini bado ni kundi ambalo mimi kwa mtazamo wangu naona hatujalitendea haki kikweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu tumeanza kujadili bajeti za Wizara ni kama tumefika nusu ya safari. Sasa mimi sijui hizi fedha pengine hizo Wizara zinazokuja ndiyo zitapewa asilimia hizo nyingi 70%, 80% na 90%, lakini tangu tumeanza ni 3%; sana sana tumekwenda mbele asilimia 50 na kitu. Hizi fedha zinasubiri kupangiwa Wizara ipi, kama Wizara nyeti kama hii inapewa fedha kidogo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye kilimo cha zao la mahindi. Zao la mahindi ni zao la biashara lakini pia ni zao kuu la chakula kwa maeneo mengi ya nchi yetu. Zao hili kwa takwimu za kitabu cha Waziri linachangia karibu tani milioni sita kwa mwaka. Tukiwa serious tunaweza kuzalisha zaidi ya mara tatu au nne ya kiasi hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa kwenye kilimo cha zao la mahindi ni suala la mbegu. Utafiti unaonesha kabisa ukilima mahindi ukatumia zile mbegu zetu za asili, zile za kuchukua tu, utavuna kidogo, lakini ukipanda mbegu zile zilizoboreshwa, utapata angalau kiasi cha kutosha kwa heka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wenzangu wamesema, mbegu za mahindi ambazo zimeboreshwa ni ghali sana na sehemu kubwa inatoka nje ya nchi. Sasa Mheshimiwa Waziri na Naibu wake, mimi sijui wataacha legacy gani mtakapoondoka katika eneo hili la kilimo cha mahindi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tunaomba ili tuwakumbuke mtuambie Kampuni ya TANSEED iliyokuwa inazalisha mbegu nchini miaka ya nyuma, imekwenda wapi? Mtuoneshe hilo kaburi mahali lilipo tukafufue ili tuzalishe mbegu ndani ya nchi yetu ili bei ya mbegu iwe rahisi.

Wakulima wengi wanajitahidi sana, wanalima kwa muda, lakini linapokuja suala la kupanda, kwa kweli mbegu inawakwaza. Mwisho wa siku wanaishia kwenye kupanda kile chochote ambacho ama amenunua dukani au amepewa chakula cha msaada na matokeo yake kwa heka anaishia kupata gunia mbili au tatu. Tunao uwezo wa kuongeza uzalishaji wa zao la mahindi kama tutazingatia suala la mbegu bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye zao la mbaazi. Kwa miaka ya karibuni, zao la mbaazi limekuwa ni mkombozi kwa wakulima wengi kwenye zile kanda ambazo zao hili linalimwa. Msimu wa mwaka 2015 zao hili lilikwenda kwa kilo karibu shilingi 3,000, msimu wa mwaka 2016 zao hili likashuka hadi shilingi 900; wakulima wamechanganyikiwa, wamekosa hamu ya kulima zao hili kwa sababu bei hailipi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawaomba ndugu zangu mliopo kwenye dawati la Wizara
hebu mtusaidie kutuunganisha na masoko ya zao hili yalioko ndani au nje ya nchi ili wakulima wetu waweze kupata bei nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kwenye eneo hili ni suala la wanunuzi wa zao hili. Wapo wanunuzi ambao hadi leo tunapoongea, bado hawajawalipa wakulima fedha zao baada ya kuchukua mbaazi zao. Tunaomba Mawaziri mtakapokuwa mnahitimisha mtuambie, wanunuzi wa mazao kama hawa, ambao wanawakopa wakulima mwaka mzima, wachukuliwe hatua gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye eneo la pembejeo. Wenzangu pia wamelisema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara imejaa wataalamu wa kila aina na wa kila rangi, hivi inawezekanaje pembejeo zinachelewa kwenda kwenye maeneo yanayohusika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnajua watu hawa wanahitaji mbegu kwa ajili ya kupanda; msimu wa kupanda ni Januari, lakini mbegu zinaenda mwezi wa tatu za kazi gani? Kwa hiyo, nadhani kuna vitu vingine tunapopiga kelele, sijui tatizo lipo wapi? Kwa nini hayo marekebisho yasifanyike? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi hata kabla sijaingia Bungeni, suala la ucheleweshaji wa pembejeo limekuwa ni jambo ambalo halijapata ufumbuzi. Nadhani ni vitu vidogo sana. Suala la kalenda ya kilimo kwenye maeneo mbalimbali ya nchi yetu inafahamika; na pembejeo hizi kwa bahati nzuri au mbaya inawalenga watu wachache. Hivi inashindikana nini kupeleka tani tano au kumi kwenye Wilaya X kwa muda ili wananchi wale waliolengwa walime pia na kupanda kwa muda?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani hili jambo linawezekana. Hebu mzizi huu sasa ukateni, fitina kwenye eneo la ucheleweshaji iishe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Maafisa Ugani ni watu muhimu sana kuwasaidia wakulima wetu, lakini tunao wachache sana.

Kwa hiyo, nilikuwa nadhani katika Wizara hii kama kuna eneo ambalo mnaweza kuwatendea haki wananchi wetu ni kuwapeleka Maafisa Ugani wa kutosha. Wale wachache walioko vijijini, sasa hivi ndiyo wamekuwa Acting WEOs na Acting VEOs hawafanyi zile kazi zao ambazo zimewapeleka kule. Kwa hiyo, naomba Maafisa Ugani pia wapewe uwezeshwaji wa vifaa vya usafiri ili waweze kuwafikia wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri amechelewa kupiga marufuku uchinjwaji wa punda. Amechelewa kabisa! Nilitegemea angesema kesho. Wanyama hawa wanaisha na wanyama hawa wanazaliana kidogo kidogo sana. Kule vijijini wanyama hawa ambao walikuwa wanatusaidia kusafirisha vitu, kuchota maji na kupeleka vitu sokoni, sasa hivi wanaibiwa hovyo.

Kwa hiyo, naomba suala la kupiga marufuku ikiwezekana punguza huo muda. Siku 45 zinatosha kumaliza punda katika nchi hii. Hao wanaofanya biashara ya punda, sasa hivi wamebadilisha mbinu nyingine, wanawachinja huko huko na ngozi wanazichukua na wanapeleka huko wanakopeleka. Wanyama hawa ili wasiishe, hiyo marufuku naomba ipunguze muda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme juu ya suala la kilimo cha umwagiliaji. Kilimo chetu kwa muda mrefu kimekuwa ni kilimo kinachotegemea mvua. Hebu tuchukue jitihada za makusudi za kuelekea kwenye kilimo cha umwagiliaji. Nchi hii, leo mvua inanyesha, baada ya wiki mbili, tuna shida ya maji. Tuwekeze kwenye miradi mikubwa mikubwa ambayo itachochea kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Olenasha jirani yangu, anafahamu kwamba sisi Mang’ola ni wakulima wazuri sana wa vitunguu na tunazo chemchemi zenye uwezo mkubwa wa kumwagilia mwaka mzima, lakini tatizo letu mifereji ile ya kumwagilia haijajengewa. Hebu wekeni mpango tusaidieni wananchi wa Mang’ola waweze kumwagilia vizuri baada ya ile mifereji kujengewa ili maji yafike kwa wakulima walioko upande wa pili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongee juu ya migogoro ya wakulima na wafugaji. Migogoro hii imekuwa ni ya muda mrefu. Jitihada mbalimbali zimefanyika, lakini jambo hili naishauri Serikali, hebu lifike mwisho. Hawa watu wawili wote ni Watanzania; hebu tuwekeni pamoja kwenye meza moja tuongee, tusiwe tunagomba kila siku. Nchi hii imetawaliwa na migogoro ambayo haiishi. Kila mmoja hapa anachangia kwenye pato la Taifa. Huyu mfugaji kwa sehemu ni kama alikuwa ameachwa achwa, ni kama hakulindwa. Ifike mahali tutambue kwamba hata ndugu zetu wafugaji wana mchango kwenye pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya kuchungia hayapo. Serikali sasa hivi inasema tutenge maeneo, hivi tutatenga kutoka wapi? Hivi ukisema Wilaya ya Karatu tutenge maeneo ya kufugia, yako wapi? Hebu mje mtembee mwone, hakuna eneo la kufugia! Pia mje na mpango ambao utatusaidia hata yule ng’ombe moja au wawili tuwafuge kwa ubora ili watupe kile ambacho tunataka. Mkisema tuuze ng’ombe, hivi mnadhani wafugaji hawajui mahali minada ilipo? Tunajua mahali minada ilipo, lakini hatuuzi kwa sababu ng’ombe ni benki yetu. Sasa ukiniambia niuze, wewe mbona accounts zako za NBC na CRDB hufungi? Kwa hiyo, suala siyo kuuza mifugo, suala ni kumsaidia mkulima ili afuge kwa kisasa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwenye eneo la hifadhi ya chakula. Tunapoteza chakula kingi kwa sababu ya uharibifu unaofanywa na wadudu. Takwimu zinasema, karibu asilimia 40 ya tunachokivuna, kinapotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naunga mkono hoja ya Kambi ya Upinzani.