Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia hii Wizara muhimu ya Kilimo. Kwanza nianze kwa kumpongeza Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Wizara nzima kwa bajeti nzuri. Pia napongeza na uchambuzi wa Kamati, kwa kweli wamekuwa makini sana Kamati, wamekuja na report nzuri sana ambayo imetusaidia hata katika huu mchango nitakaoutoa mimi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze kwa kipekee kabisa Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa juhudi ambazo wanazifanya kuondoa zile changamoto zilizopo kwenye mazao yetu na hasa zao la pareto kule Mbeya, naona sasa hivi kuna kiwanda kimeanzishwa pale Inyala ambacho kimeongeza ushindani lakini nina imani kuwa zile changamoto ndogo ndogo ambazo zimebaki wanaendelea kuzishughulikia ili tuondokane na zao la pareto kutoka leo chini ya tani 3,000 twende mpaka tani 8,000 ambazo ndiyo potentials, tunaweza kuzalisha Tanzania. Vile vile waendelee kuboresha bei ya pareto kutoka hii iliyopo sasa hivi ya Sh.2,500/= ifike angalau Sh.4,000/= kwa kilo, ambayo nafikiri itamsaidia hata wale wauzaji wa nje wanaweza nao kupata faida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nampongeza Waziri kwa report yake hii ambayo ameonyesha ni namna gani inalenga kuwasaidia wakulima kupata pambejeo kwa bei nafuu. Ni kweli kabisa pembejeo au mazao ya kilimo hata mashirika ya nje yanaangalia kwa karibu sana ni namna gani wamsaidie mkulima. Wenzetu ambao ni wanunuzi wakubwa kule nje na wazalishaji wakubwa wanaangalia ni namna gani mkulima wasimnyonye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo nampongeza Waziri kwa vile umelisema mwenyewe katika ukurasa wa 51, ambapo ameelezea kuwa mwenendo wa bei za mbolea katika soko la dunia zipo kwenye viwanda vichache na zinauzwa kwa bei ya chini katika muda muafaka, hilo ni zuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na hii bulk procurement ya fertilizer. Hata hivyo, inabidi tuangalie, je, ni peke yake Wizara ya Kilimo atafanikisha mkulima apate hii faida? Bila kuungana na wenzako hii haitafanikiwa kwa sababu (value chain) ya mbolea ni ndefu mno na hapa kwetu bei ya mbolea haitokani peke yake na bei ya kununulia (CIF), inatokana na gharama kubwa za usambazaji kuanzia Bandarini. Bei ya kununulia ni asilimia 53 tu lakini bei ya ukiritimba wa usambazaji kutoka Bandarini, tunatumia magari, barabara zetu mbovu inachangia hiyo asilimia nyingine 47. Sasa ukija kuchanganya na kwa vile mbolea tunanunua nje, kama hatutaweza kudhibiti mfumuko wa exchange rate ina maana vile vile hatutawasaidia wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sisi ambacho kinaweza kutusaidia ambacho naiomba Seriakli ijaribu kutusaidia, ni namna gani tupunguze gharama hii ya asilimia 47 ambayo ni mzigo mkubwa sana kwa mkulima. Kwa sababu ukilinganisha na wenzetu wa Ufilipino, ni asilimia chini ya 10, ukienda kanchi kadogo kama Myanmar ni asilimia chini ya 20, sasa sisi kwanini mkulima achangie asilimia 47 ya bei ya CIF? Inamuumiza sana mkulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshauri Mheshimiwa Waziri na timu yake wakae chini na Wizara ya Miundombinu, mahali kama Mbeya huhitaji kusafirisha mbolea kwa magari, ni gharama kubwa. Tani moja inakwenda zaidi ya 100,000 na ikifika pale inabidi iende kijijini. Kwa nini hiyo mbolea ikija kwa bulk itoke kwenye meli iingie kwenye mabehewa ya TAZARA, tuwe na bandari kavu Mbeya ili tuweze kusambaza Ukanda mzima wa Nyanda za Juu na packing ifanyikie pale Mbeya na si Dar es Salaam?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo itasaidia vile vile na mazao mengine ambayo kahawa sasa hatutakuwa na sababu ya kuipeleka bandarini, tutaisafirisha kwenye Ulaya kutoka kwenye Bandari kavu pale Mbeya. Hii itapunguza gharama na mzigo mkubwa kwa mkulima. Kwa hiyo namwomba sana ndugu yangu, anafanya jitihada kubwa, zimeshaonekana na leo hii watu wanasifia hizo tozo ambazo zimepunguzwa, kama kwenye kahawa, ni lini zitaanza na nina imani kuwa zinaanza mara moja, wakulima wamefurahia na kweli hiyo itatupunguzia mzigo mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kilimo chetu tunakuwa maskini wakati mwingine kwa sababu wataalam hawatusaidii vizuri. Ukilima vizuri hekta moja ya mahindi unaweza kutumia mifuko kama mitano ya mbolea na huhitaji hata kulima kilimo cha hifadhi ardhi. Unachohitaji ni kuweka mbolea muafaka ambayo inalingana na udongo, na siyo lazima iwe Urea ama DAP. Hilo nalo Waziri ajaribu kuliangalia kwa vile sasa tumebadilika, hatulimi tena kwa kupandia na DAP, hatulimi tena kwa kukuzia na Urea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo cha sasa hivi tunachotumia, nikitumia mbolea labda ya NPK 17-17-17 or NPK 15-15-15, nina uwezo kwa hekta moja kupata kilo 13,000 ambazo zinaweza kuniletea milioni 12 kwa hekta. Kwa mkulima wa kawaida ambaye amelima, ametumia mifuko mitatu mingine anauwezo wa kupata kilo 6,000 na akapata milioni tano. Vile vile mkulima atakayelima kwa hizi mbolea ambazo nazisema, atapata kilo 1,800 ambayo ni hela kidogo sana, inamwendeleza kuwa masikini. Kwa hiyo hapa suala siyo mbolea tu na mbolea ni tofauti na petrol. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbolea ni product kutokana na udongo. Tunahitaji hii lime inayozalisha hapa Dodoma iletwe Mbeya iboreshe ili wakulima waweze kupata kilo 13,000 kwa hekta. Ni zao zuri sana, limejaribiwa na uzuri wake hata kile Chuo cha Kilimo Uyole, waliwapeleka wakulima kwa mkulima mmoja Iringa, tumekuta yule halimi yeye ardhi ile; anapanda kisasa, anatumia mbolea kisasa na tumeangalia kwa macho yetu kulinganisha na mashamba ya jirani yake na hiyo ni Wizara iliyotupeleka pale. Sasa kwa nini tusielekee hiyo kwa ajili ya kumsadia mkulima? Hiyo ndio itakayotusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii bila kumsaidia mkulima umaskini utaendelea kututesa na kilimo tukifanye cha kijasiriamali mno, cha mahesabu. Tusiseme tu ya kwamba tutaleta DAP na UREA, tuseme ya kwamba kwenye eka moja utazalisha nini? Utaondoka vipi kwenye umaskini huu tulionao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina imani tukilifuatilia hilo kwa sisi tunaotoka kwenye majimbo ya kilimo, tunalima viazi; ukilima kisasa unakuwa tajiri, ukilima mahindi unakuwa tajiri, ukilima kahawa unakuwa tajiri na haya mazao yetu yana bei nzuri huko duniani kuliko kwingine. Ni competitive kwa sababu ukiangalia kahawa ya kwetu ni changamoto tu zinafanya bei inakuwa ndogo kuliko Kenya au Ethiopia. Ukiangalia mahindi ni changamoto tu zinafanya bei inakuwa ni ndogo kuliko ya Zambia. Tunaomba Serikali iwe na mkakati na iangalie ni namna gani itaondoa hilo ili tuweze kumsaidia mkulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu mwingine nitachangia kwa maandishi. Naunga mkono hoja na ahsante sana.