Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, mpaji wa yote, ambaye yeye ndiye ametuwezesha wote tuwepo humu ndani siku hii ya leo, tukifurahia maisha ndani ya nchi yetu yenye amani ya kutosha kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, niwapongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayoifanya chini ya Wizara hii ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Wamekuwa ni Viongozi ambao wamekuwa wakitoa ushirikiano mkubwa sana kwa sisi wawakilishi wa wananchi na hasa sisi tunaotoka maeneo ambayo yanajishughulisha na kilimo. Kwa kweli nawapongeza sana na nawashukuru na kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu waendelee kutoa ushirikiano kwetu, tuendelee kushauriana na kusaidiana ili kuboresha maisha ya wakulima na wafugaji wetu kwa kuhakikisha kwamba nchi yetu inakuwa na chakula cha kutosha na tunaweza kuendesha nchi vizuri kwa ushirikiano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mwakilishi wa wananchi kutoka Jimbo la Njombe Mjini, jina hili mjini ni jina tu lakini Jimbo langu mimi lina Halmashauri moja lakini lina Tarafa mbili. Tarafa moja ni ya mjini lakini Tarafa nyingine ni ya vijijini na ina kata kumi na tunajishughulisha na kilimo barabara. Moja ya mbinu za kilimo ambayo tunatumia ni vinyungu. Wiki iliyopita headlines nyingi sana za habari hapa nchini zilizungumzia vinyungu na leo naomba niongee habari ya vinyungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana kuna Mbunge amesema yeye amekuzwa kwa pamba na samaki na mimi nasema nimekuzwa kwa vinyungu. Kila mwananchi anayetokea Mkoa wa Njombe na yeye amekuzwa kwa vinyungu. Vinyungu sisi kwetu ni kilimo muhimu sana. Hizi sheria zinavyotungwa ni vizuri sana zikafanyiwa utafiti wa kutosha, kwa sababu unapotuambia watu wa Njombe tusilime vinyungu, sisi tunasema na mpunga usilimwe, kwa sababu mpunga ndiyo unaolimwa mabondeni na mpunga ndiyo unatumia maeneo makubwa zaidi kuliko vinyungu. Kwa hiyo kwa kutuambia sisi tusilime vinyungu tu ni kutuonea na kutufanya sisi tuendelee kuwa maskini bila hata sababu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba wataalam, sawa najua kuna Sheria ya Vinyungu inayosema tusilime mita sitini kutoka kwenye mtiririko wa maji, lakini maji hayahifadhiwi bondeni, maji yanahifadhiwa mlimani, ndiyo maana wote tunaokumbuka miaka ya nyuma baada tu ya uhuru na miaka mingine kidogo, kilimo chochote lazima mkulima alime makinga maji ndani ya shamba lake. Makingamaji ndiyo yanayohifadhi maji kwa sababu maji yale yatakuwa hayatiririki yote na kuondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wataalam wetu wa kilimo leo hawaelekezi wakulima juu ya makingamaji, watu wa mazingira na wenyewe wameng’ang’ana tu kuhusu mita sitini. Ninachosema, mita sitini itakuwa ni kuwanyanyasa wananchi na kuwafanya wafe na njaa, lakini kama ni kweli maji yanahifadhiwa bondeni basi na mpunga usilimwe kwa sababu wenyewe ndiyo unaotumia maeneo makubwa zaidi ya mabondeni. Nafikiri ujumbe huo umefika, Mheshimiwa Waziri, naamini hata huko Mwanza nina imani kutakuwa na vinyungu tu, haiwezekani kusiwe na vinyungu, Tanzania nzima tunalima vinyungu wataalam waangalie upya utaratibu wa kuhifadhi maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya suala la vinyungu sasa niongelee suala la mifugo. Nilikuwa najaribu kupitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri, kuna mambo yamenisikitisha sana. Tuna tatizo kubwa sana la ng’ombe wa maziwa, ng’ombe hawa ndio ambao wanaweza wakawa na manufaa makubwa sana kwa wakulima walio wengi, lakini idadi ya ng’ombe wa maziwa ni wachache mno na uzalishaji wetu uko chini mno, sasa unajiuliza, mashamba yote haya kwa nini hayazalishi ng’ombe. Mheshimiwa Waziri mwenyewe katika hotuba yake amekiri kwamba maziwa yamepungua kwa asilimia 2.3 na anasema kwamba moja ya matatizo ni kukosekana kwa malisho, kuna ukame na malisho yamepungua, ukweli ni kwamba hata uzalishaji wetu wa malisho ni kidogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Watanzania lazima tuangalie kwamba tunataka kufanya nini kwenye kilimo, tunataka kufanya nini kwenye mifugo. Mifugo ina uwezo wa kuwaajiri vijana wengi sana. Leo hii kuna watu wanalima nyasi wanasafirisha nje ya nchi, hivi hatuwezi kweli kuanzisha ma-block makubwa ya kulima nyasi na tukaweka vifaa vya kutosha na vijana wakafanya hizo kazi. Tatizo kubwa tulilonalo ni kwamba tunawaambia vijana waende shamba, kijana wa leo ameelimika hawezi kwenda kushika jembe kwa mkono, ni lazima tuhakikishe kwamba tunaweka vifaa na mazingira wezeshi ili vijana wale wasimamie hayo mashamba kwa urahisi, lakini tunavyosema tu waende shamba hawataweza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vijana wangeweza kulima nyasi za kutosha, wakazifungasha na wakazisafirisha, lakini vilevile wakapeleka maeneo mbalimbali ambayo yana uhaba wa nyasi na mifugo ikapata nyasi. Sisi tunazalisha nyasi viroba 684,000, viroba 600,000 ni nyasi za ng’ombe 900 kwa mwaka, sasa ng’ombe 900 watatupeleka wapi? Kwa hiyo, niiombe sana Serikali ilione hilo, ianze kuweka mpango maalum wa kuhakikisha tunakuwa na mashamba makubwa ya nyasi ambayo yatakuwa na vifaa vya kutosha kwa ajili ya mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile watendaji wa Mheshimiwa Waziri kidogo nao wameteleza. Katika ukurasa wa 106 wanaeleza kwamba kuna kiambatanisho cha viwanda vya maziwa, naomba waangalie hapo kwenye kielelezo hicho kama kinaelezea maziwa, maana yake kielelezo kilichopo katika ukurasa huo kinaeleza habari ya mbegu mama. Sasa sisi wenye interest na viwanda vya maziwa tunapata taabu sana kujua. Kwa hiyo, kama taarifa hizo zipo tunaomba watuletee tuweze kuziona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana, kwanza tuongeze uzalishaji wa mitamba hii lakini pia tuongeze ukubwa wa mashamba kwa ajili ya malisho. Kwa sababu tunazalisha mitamba michache sana kwa mwaka, mwaka ambao ilizalishwa mitamba mingi ni kati ya mwaka 2011 na 2017 ambapo ilizalishwa mitamba 800 kwa nchi nzima, nchi kubwa namna hii hatuwezi kuzalisha mitamba kiasi kidogo namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukija kwenye usindikaji wa maziwa lipo tatizo. Tatizo ambalo mimi naliona sasa hivi tumeingiza VAT kwenye mtindi. Sasa viwanda hivi, kwa mfano pale Njombe tuna Kiwanda cha maziwa kinaitwa CEFA, kiwanda kile ni cha wafugaji, ni kiwanda cha ushirika, tumeingiza VAT kwenye mtindi, matokeo yake wananchi wale hawapandishiwi bei ya maziwa kwa sababu kiwanda kinaingia gharama. Kwa hiyo, naomba Serikali iliangalie sana hilo kama kweli tuna nia ya kuwasaidia wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la kilimo, upimaji wa udongo; tunahangaika na mbolea sawa, mbolea ni muhimu sana kwa ajili ya kilimo na nini lakini lipo suala la msingi zaidi, ni lazima udongo wetu ujulikane, kwa sababu mbolea ni dawa, kwa hiyo tunatibu nini katika udongo wakati hatujui kwamba udongo unaumwa nini. Kwa hiyo, ni vizuri sana Serikali ikaona kwamba, ni kwa namna gani sasa kila halmashauri lazima iwe na kifaa cha kupimia udongo, hata kifaa kile kidogo tu ili kusaidia kupima udongo. Wataalam wamesema chokaa ya kilimo ndiyo chokaa inayoweza kusaidia kurekebisha udongo, hapa Dodoma kuna mgodi lakini sijaona kama Serikali iko serious na ule Mgodi wa Chokaa ya Kilimo. Chokaa hii tuichukue tuisambaze kwa wakulima ili waweze kuongeza mapato yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zana za kilimo; hatuwezi kwenda kwa jembe la mkono, hata siku moja, lakini hata haya matrekta yenyewe ambayo tunayapata, ubora wake ukoje. Leo hii ukienda hapo Kilimo Kwanza, ukiyaona yale matrekta labda yana miaka mitatu au minne jinsi yalivyomomonyoka yanatia huruma. Unaona kabisa kwamba hata kama kuna uzembe katika matumizi lakini hata ubora uko chini. Naomba sana, wanaoshughulika na matrekta wahakikishe kwamba matrekta yanakuwa bora na wananchi wanaweza wakayapata matrekta hayo wakayatumia kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, mikopo ya matrekta na yenyewe siyo rafiki kwa wakulima. Unamwambia mkulima alipe asilimia 50 halafu asilimia 50 iliyobakia ndani ya mwaka mmoja, ni mkulima gani atakayeweza namna hiyo, kwa hiyo hilo nalo ni jambo gumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kuhusu suala la mbolea. Naipongeza sana Serikali kwa mpango inayokuja nao. Angalizo ambalo naomba niiambie Serikali yangu ni kwamba, lipo tatizo, sasa hivi wenye mbolea (importers wa mbolea) tayari wana mbolea kwenye ma-godown. Serikali itakaposema mbolea kwa utaratibu huu ambao inaelekeza sasa watakwambia hiyo mbolea inayokuja Mheshimiwa Waziri tunaomba tuiuze mwakani kwa sababu sasa hivi stock imejaa. Kwa hiyo bei itabaki palepale na wananchi wataendelea kuumia. Kwa hiyo, niombe sana, kama kweli mchakato huu upo, umekaa vizuri, fanyeni haraka inavyowezekana ili wananchi waweze kupata mbolea kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tozo, Mheshimiwa Waziri ameondoa tozo nyingi sana, kweli zinaonekana zina manufaa, lakini nimwombe sana sisi tunaotoka maeneo yanayolima chai wameondoa tozo ya Vyama vya Msingi vya Wakulima ya Sh.500/= kwa kilo. Hii tozo aliyoondoa haimnufaishi mkulima na wala haitakaa irudi kwa mkulima, hii ni tozo ya majani makavu kiwandani. Ilikuwa ni tozo ambayo viwanda vilikuwa vinarudisha kwenye Vyama vya Msingi ili kusudi vyama vile viweze kujiendesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa unahitimisha hotuba yake atuambie hii Sh.5/= aliyotoa, je, Vyama hivi vya Msingi vitaendeleaje kufanya kazi kwa sababu hotuba ya Kamati imesisitiza kuimarisha ushirika, anapouondolea ushirika tozo hii anaufanya ushirika ukose uwezo wa kujiendesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana.